Mahubiri Makuu Ya Yesu Kuhusu Wokovu, 2

SURA YA SABA

 

Ni wachungaji wangapi wangeona wameheshimiwa sana kama mtu angewaita “mhubiri wa utakatifu”? Ni wangapi wanaojiita Wakristo wangetumia maneno hayo kwa njia ambayo si ya kudhihaki? Mbona utakatifu ni somo baya sana mawazoni mwa watu wengi wanaodai kuamini kitabu ambacho kina maneno mtakatifu au utakatifu zaidi ya mara mia sita, chenye kuwaahidi wakati ujao katika mji mtakatifu ambamo ndani yake anakaa “Aliye mtakatifu”, ambaye jina Lake ni mtakatifu, anayewapa Roho Wake Mtakatifu na ambaye kiti Chake cha enzi kitakatifu kimezungukwa na wenye uhai wanne wasioacha kusema usiku na mchana, “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Mungu Mwenyezi”? (ona Ufunuo 21:2; Isaya 40:25; Walawi 22:32; 1Wathes. 4:8; Zaburi 47:8; Ufunuo 4:8 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).

Kama sehemu ya kwanza ya Mahubiri ya Mlimani imetufundisha kitu, ni kwamba Yesu alikuwa mhubiri wa utakatifu. Hiyo ndiyo iliyokuwa mada Yake – utakatifu, na jinsi unavyohusiana na wokovu.

Mahubiri ya Mlimani yameandikwa katika Injili ya Mathayo sura ya 5, 6 na 7. Mpaka sasa tumetazama sura ya 5 tu. Hapo, katika zile “Heri” tulijifunza tabia au sifa za wanaokwenda mbinguni. Pia tuligundua kwamba Yesu hakuja kuibatilisha au kuiondoa Torati, na kwamba kushika sheria ni muhimu sana. Tulijifunza kwamba hatuwezi kuingia katika ufalme wa mbinguni kama haki yetu haitazidi ile ya waandishi na Mafarisayo, walioishika sheria kama ilivyokuwa ila wakapuuza maana yake.

Sehemu ya pili ya Mahubiri ya Mlimani – yaani Mathayo 6 na nusu ya kwanza ya sura ya 7 – ina amri zingine tena ambazo Kristo aliwapa wafuasi Wake. Je, kuzishika kunahusika kwa lolote na wokovu? Hakika kabisa. Sehemu ya mwisho ya sura ya saba inaonyesha jambo hilo waziwazi kabisa, kama tutakavyoweza kujionea.

Hebu tuendelee kusoma yale ambayo Yesu aliwaagiza wafuasi Wake wa kweli, ambao waliamini kwamba Yeye ni Mwana wa Mungu, ni Masiya. Tujiulize swali hili, zito kabisa: Ikiwa wasikilizaji wa Yesu hawakumwamini, walimtii kwa sababu gani? Mbona watake hata kusikiliza akifanya madai ambayo yangeathiri kila eneo la maisha yao? Jibu ni wazi: Kwa kuwa waliamini, walitaka kutii. Wangeonyesha imani yao kwa matendo yao.

Sura Ya Sita Inaanza

Ona katika sehemu hii ya kwanza Yesu anahesabu kwamba wafuasi Wake watatenda haki, naye anawaonya wahakikishe kwamba makusudi yao ni kumpendeza Mungu badala ya kuwapendeza watu.

“Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. Amin nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe ya siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi” (Mathayo 6:1-4 – Maneno mepesi kutilia mkazo).

Yesu alitazamia kabisa kwamba wafuasi Wake wangetoa sadaka kwa maskini (kama tulivyojifunza katika sura ya 3 ya kitabu hiki). Torati iliagiza hivyo (ona Kutoka 23:11; Walawi 19:10; 23:22; 25:35; Kumbu. 15:7-11), na waandishi na Mafarisayo walifanya hivyo kwa kupiga matarumbeta, kwa kusudi la kuwafanya watu maskini waone utoaji wao. Lakini – ni wangapi wanaojiita Wakristo (na hata makanisa ya Kikristo) wanaotoa chochote kwa maskini? Hawajafikia hata mahali pa kutaka kuchunguza makusudi yao ya utoaji zaka! Kama uchoyo na ubinafsi uliwasukuma waandishi na Mafarisayo kutangaza kutoa kwao sadaka, ni nini kinachowasukuma wanaojiita Wakristo kupuuza hali ya maskini? Je, haki yetu inazidi ile ya waandishi na Mafarisayo?

Kama ambavyo Paulo atarudia katika 1Wakorintho 3:10-15, tunaweza kufanya matendo mema ambayo hayatapata thawabu ikiwa nia na makusudi yetu si safi. Wafuasi wa kweli wa Kristo wanapaswa kuwa na nia safi katika kila tendo jema, lakini si wote walio nayo. Paulo aliandika kwamba inawezekana hata kuihubiri Injili kwa makusudi yasiyo safi (ona Wafilipi 1:15-17). Njia iliyo bora ya kuhakikisha kwamba kutoa kwetu kunasukumwa na makusudi safi ni kutoa kwa siri kiasi iwezekanavyo.

Yesu pia aliwatazamia wafuasi Wake waombe na kufunga. Hiyo ilikuwa lazima. Hakusema “Kama mtaomba”. Alisema “Mwombapo”. Hatari ilikuwa wangeweza kuyaruhusu makusudi yao kuchafuka, kama ilivyokuwa kwa makusudi ya wasioamini waliokuwa wanaomba na kufunga. Kama hayo yangetokea, wangepoteza thawabu ile ambayo wangepata kama makusudi yao yangekuwa safi. Basi aliwapa mashauri yafuatayo:

“Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi. Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayoyahitaji kabla ninyi hamjamwomba…”

“Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso, ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi” (Mathayo 6:5-8; 16-18).

Narudia tena: Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo ambao hawatumii muda wao mwingi katika maombi, na ambao hawajawahi kufunga kabisa? Haki yao inalinganishwaje na haki ya waandishi na Mafarisayo, ambao walifunga na kuomba (japo kwa sababu mbaya)?

Kuomba Kitakatifu

Yesu pia aliwaambia wanafunzi Wake jinsi walivyotakiwa kuomba. Maombi Yake mfano ni ufunuo wa hali ya juu sana kuhusu matazamio Yake kwa habari ya pendo lao, utii wao na vipaumbele.

“Basi ninyi salini hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu’.” (Mathayo 6:9-11)

Jambo la kwanza muhimu sana kwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu iwe jina la Mungu litukuzwe. Yaani, jina la Mungu liheshimiwe, liabudiwe na kutakatifuzwa.

Bila shaka wale wanaoomba kwamba jina la Mungu litukuzwe wanatakiwa wao wenyewe kuwa watakatifu, wanaolitukuza jina la Mungu. Itakuwa ni unafiki kufanya vinginevyo. Kwa hiyo, sala hii inaonyesha shauku yetu kwamba na wengine wajinyenyekeze kwa Mungu kama ambavyo sisi tumefanya. Na – kama nilivyouliza katika sura nyingine hapo nyuma – mtu anaonyeshaje kiwango cha shauku yake kwamba anataka jina la Mungu litakaswe kama anajistarehesha kwa kutazama picha ambazo zinachezwa na wachezaji wenye kutumia vibaya jina la Mungu na la Mwana Wake? Kulingana na uchunguzi wangu, hiki ni kitu ambacho wengi wanaojiita Wakristo hufanya mara kwa mara. Je, wewe ungechukizwa na sinema ambayo waigizaji wanatumia jina lako kama neno la kuapa au kushangaa?

Ombi la pili katika sala hiyo linafanana na la kwanza: “Ufalme wako uje.” Wazo la ufalme huonyesha kwamba kuna Mfalme anayetawala ufalme Wake. Mwanafunzi Mkristo anatamani kuona mfalme Wake – yule atawalaye maishani mwake – akitawala dunia nzima. Laiti kila mtu angepiga goti lake kwa Mfalme Yesu, katika imani tiifu!

Ombi la tatu linarudia yale mawili ya kwanza: “Mapenzi yako yafanyike hapa duniani kama huko mbinguni.” Hapa tena – tunawezaje kuomba kwa dhati ombi la namna hii bila sisi wenyewe kuwa tumejinyenyekeza chini ya mapenzi ya Mungu katika maisha yetu? Mwanafunzi wa kweli anatamani kwamba mapenzi ya Mungu yatafanyika duniani kama huko mbinguni – kikamilifu na kabisa.

Kwamba jina la Mungu litakaswe, na mapenzi Yake yafanyike, na ufalme Wake uje vinatakiwa kuwa muhimu zaidi kwetu kuliko chakula cha kutuhifadhi, au “riziki yetu”. Hili ombi la nne linawekwa hapo kwa sababu. Inaonyesha mpangilio mzuri wa mambo ya muhimu maishani mwetu, na hakuna dalili za uchoyo hapo. Huyu mwanafunzi anayeomba anamtumikia Mungu, si mali.

Sala ‘Mfano’ Inaendelea

Mpaka hapa mada ya utakatifu inatokezea katika kila ombi la sala hii. Na inaendelea kujitokeza katika mistari yake ya mwisho.

“ ‘Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele, Amina’. Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu” (Mathayo 6:2-15).

Mwanafunzi wa kweli wa Yesu anatamani kuwa mtakatifu, kwa hiyo, anapotenda dhambi, anasumbuliwa sana. Yeye hutambua kwamba kutokutii kwake kumemkwaza Mungu, na anajisikia aibu. Anataka doa la uchafu huo liondolewe, na shukrani ni kwamba, Baba yake wa mbinguni mwenye neema, yuko tayari kumsamehe. Lakini lazima aombe msamaha, ambalo ndiyo ombi la tano lipatikanalo katika sala ya Bwana.

Lakini, kusamehewa kwetu kunategemeana na sisi kuwasamehe wengine. Kwa sababu tumesamehewa vingi, tunawajibika kumsamehe kila mtu anayetuomba msamaha sisi, na kuwapenda wale ambao hawatuombi msamaha. Tukikataa kusamehe, Mungu hatatusamehe sisi.

Ombi la sita na la mwisho pia linahusiana na utakatifu, kwamba, “Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu [au, kutoka maovuni].” Mwanafunzi wa kweli anatamani utakatifu kiasi cha kwamba anamwomba Mungu hata asimwongoze katika hali ambapo anaweza kujaribiwa, asije akashindwa. Tena, anaomba kwamba Mungu amwokoe kutokana na uovu wowote unaoweza kumnasa. Hili ombi la mwisho katika sala ‘mfano’ ya Yesu si kitu kingine: ni kilio kwamba Mungu asaidie katika utakatifu.

Kwa nini maombi yote hayo sita katika sala hii yanayofaa? Mstari wa mwisho unatuambia: Mungu ni Mfalme mkuu anayetawala ufalme Wake, ambamo ndani yake sisi ni watumishi Wake. Ana nguvu zote, na hakuna anayetakiwa kuthubutu kupinga mapenzi Yake. Utukufu wote utakuwa Wake milele – “Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele” (Mathayo 6:13). Yeye ndiye wa kumtii, na anastahili hivyo.

Nini kiini kikuu cha sala ya Bwana? Utakatifu. Wanafunzi wa Kristo wanatamani kwamba jina la Mungu litakaswe, ufalme Wake uthibitishwe duniani, na kwamba mapenzi Yake yafanyike kila mahali kikamilifu. Hii ni muhimu sana kwao kuliko hata chakula chao cha kila siku. Wao wanataka kumpendeza, na wakishindwa, wanaomba msamaha kutoka Kwake. Kama watu waliosamehewa, wanawasamehe na wengine. Wanataka kuwa watakatifu na wakamilifu mpaka wanatamani waepuke majaribu, kwa sababu majaribu huongeza nafasi zao za kutenda dhambi.

Mwanafunzi Na Mali Zake

Mada ya pili katika Mahubiri ya Mlimani ndiyo inayosumbua zaidi kwa wanaojiita Wakristo, ambao lengo lao kubwa maishani ni kupata vitu au mali.

“Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako. Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo! Hakuna awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali” (Mathayo 6:19-24).

Yesu aliagiza kwamba tusijiwekee hazina duniani. Sasa, hazina ni nini? Hazina za kweli zinawekwa kwenye masanduku ya hazina na kuhifadhiwa mahali, wala hazitumiwi kwa chochote cha maana. Yesu alifafanua kwamba ni vitu vinavyosababisha nondo, kutu na wevi. Kwa maneno mengine, “visivyo kuwa vya lazima”. Nondo hula vile tunavyoweka katika stoo zetu na pande za ndani sana za makabati yetu, si zile nguo tunazovaa mara kwa mara. Kutu hula vitu vya kuchezea na “vifaa” ambavyo hatuvitumii, vilivyolundikwa katika pembe za vyumba, katika stoo na mahali pa kuhifadhi vitu. Wevi nao huvunja na kuiba vitu ambavyo watu wengi hawavihitaji: picha, vipodozi, vitu vya thamani, na kitu kinachoweza kuuzwa kwa urahisi na kwa haraka. Si mara nyingi waibe vitanda, majiko, vyakula au viatu vya raba au kanda mbili.

Cha kuona hapo ni kwamba sisi ni wa Mungu na vyote “tulivyo navyo”. Sisi ni mawakili wa fedha za Mungu. Basi, kila uamuzi wa kutumia fedha ni uamuzi wa kiroho. Tunachofanya na fedha zetu huonyesha nani anayetawala maisha yetu. Tunapolimbikiza “hazina”, kuficha fedha na kununua visivyo muhimu, tunadhihirisha kwamba si Yesu anayetawala, kwa sababu angekuwa anatawala, tungefanya vitu bora zaidi na fedha zile alizotukabidhi.

Hivyo vilivyo bora zaidi ni kama vitu gani? Yesu anatuagiza kuweka hazina mbinguni. Tunawezaje kufanya hivyo? Anatuambia katika Injili ya Luka: “Viuzeni mlivyo navyo, mtoe sadaka. Jifanyeni mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia mwivi, wala nondo haharibu” (Luka 12:33). Kwa kutoa ili kusaidia watu, tunajiwekea akiba mbinguni. Yesu anatuambia tuchukue kile ambacho hakika kitapoteza thamani tukiwekeze katika kitu ambacho hakitapoteza thamani kamwe. Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo wanaofanya hivyo? Ni kwa nini idadi kubwa ya wanaojiita Wakristo wa Marekani, ambao wanafurahia kiwango cha juu cha maisha kuliko wengine wote duniani, hawatoi hata kiasi cha asilimia kumi tu ya mapato yao, ambacho ndicho kiwango cha chini kabisa kilichodaiwa na Torati? Hebu niongeze tu kwamba hiyo sheria ya zaka ilikuwa katika Torati ile ambayo katika mahubiri haya haya, Bwana Yesu alisema hakuja kuitangua.

Jicho Bovu

Je, Yesu alikuwa na maana gani alipozungumza juu ya jicho kuwa “taa ya mwili”? Bila shaka maneno Yake yalihusu jinsi tunavyotazama fedha na vitu, kwa sababu hayo ndiyo aliyozungumzia kabla na baada ya kusema hilo.

Hapa tena, Yesu alikuwa analinganisha watu wa aina mbili: mmoja mwenye jicho safi, ambaye mwili wake wote umejaa nuru, na mwingine mwenye jicho bovu ambaye mwili wake wote umejaa giza. Katika mistari inayofuata, Yeye pia analinganisha watu aina mbili: waliookoka na wasiookoka – mmoja anamtumikia Mungu na mwingine anatumikia fedha. Basi, ni salama kuhitimisha kwa kusema kwamba yule mwenye jicho safi ni mtu anayemtumikia Mungu, na yule mwenye jicho bovu ni mtu anayetumikia fedha.

Mtu mwenye jicho safi ni mfano wa yule anayetafuta ukweli, naye anaruhusu nuru ya kweli kuingia ndani yake. Anamtumikia Mungu. Mtu mwenye jicho baya hufungia nje mwanga wa kweli usiingie ndani yake, kwa sababu anafikiri yeye anao ukweli tayari, na kwa njia hiyo anajaa giza maishani mwake, akiamini mambo ya uongo. Yeye anaamini kwamba kusudi la maisha yake ni kujitosheleza. Fedha ndiyo mungu wake.

Nini maana ya fedha kuwa mungu wako? Maana yake ni kwamba fedha inakuwa na nafasi maishani mwako ambayo inatakiwa kukaliwa na Mungu tu. Fedha inatawala maisha yako na kuyaongoza. Inakula nguvu zako zote, mawazo yako na muda wako wote. Ndiyo asili kuu ya furaha yako. Unaipenda. Ndiyo sababu Paulo alilinganisha tamaa (au choyo) na kuabudu sanamu, akisema kwamba hakuna mchoyo au mwenye tamaa yeyote atakayeurithi ufalme wa Mungu (ona Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5-6).

Mungu na fedha hutaka kuwa bwana katika maisha yetu, na Yesu alisema hatuwezi kutumikia wote wawili. Ona pia kwamba chaguo pekee linalotajwa kwa upande wa Mungu ni kumtumikia Yeye. Hakuna uchaguzi wa kumwamini Yeye bila kumtumikia au kumfuata. Kama tutamtumikia na kumfuata, atakuwa Bwana juu ya mali zetu. Hiyo si hatua ya kuchukuliwa siku zijazo wakati fulani “wa kujitoa zaidi”. Ni hatua inayochukuliwa wakati wa kuokoka kweli kweli.

Maskini Mwenye Tamaa

Kutaka sana kupata vitu si vibaya tu ikiwa vinavyotakiwa ni vitu vya anasa – yawezekana mtu kutaka sana vitu hata kama ni mahitaji ya msingi. Hicho nacho ni kitu kibaya. Yesu aliendelea hivi:

“Kwa sababu hiyo nawaambieni, ‘Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba jinsi yameavyo; hayafanyi kazi wala hayasokoti, nami nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojwapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni yaliyopo leo na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke basi mkisema, Tule nini? Au, Tunywe nini? Au, Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi, msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake’.” (Mathayo 6:25-34)

Wasomaji wengi wa kitabu hiki hawawezi kujifananisha na wale watu ambao Yesu alikuwa anazungumza nao. Jiulize hivi: Mara ya mwisho ulipokuwa na wasiwasi juu ya kuwa na chakula, kinywaji au mavazi ni lini?

Lakini, maneno ya Yesu yanatuhusu hata sisi. Kama ni makosa kuhangaika kwa sababu ya mambo ya lazima maishani, bila shaka ni makosa makubwa zaidi kuhangaika kwa sababu ya mambo yasiyokuwa ya lazima! Yesu anawatazamia wanafunzi Wake kujihusisha zaidi na kutafuta vitu viwili: ufalme Wake na haki Yake. Wakati mtu anayejiita Mkristo anaposhindwa kutoa zaka, lakini anaweza kununua chakula cha mbwa, na kulipia kodi ya kutumia televisheni, na kulipia gari jipya au fanicha alizokopa, na kununua nguo za mitindo mipya, au kununua chakula cha starehe – je, anaishi kulingana na kiwango cha Kristo cha kutafuta kwanza ufalme Wake na haki Yake? Hapana! Huyo anajidanganya tu kama anafikiri kwamba ni mfuasi wa Yesu.

Vibanzi Na Boriti

Amri zinazofuata za Yesu kwa wafuasi Wake zinahusu dhambi ya kuwahukumu wengine na kupata makosa kwa watu. Anasema hivi:

“Msihukumu, msije mkahukumiwa na ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho ndicho mtakachopimiwa. Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au utamwambiaje nduguyo, ‘Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako;’ na kumbe! Mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe! Itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako” (Mathayo 7:1-5).

Nini maana ya kumhukumu mtu mwingine? Hakimu ni mtu anayetafuta makosa katika watu wanaofikishwa mahakamani. Hiyo ndiyo kazi yake, na hakuna kosa kufanya hivyo, mradi tu afanye hukumu yake kulingana na kweli zilizothibitishwa. Mahakimu wanapaswa kuhukumu watu, wakiwapima kwa kiwango cha sheria ya nchi. Kama wasingekuwepo mahakimu, wahalifu wasingefikishwa kwenye sheria.

Lakini, watu wengi wanafikiri kwamba wamechaguliwa kuwa mahakimu. Basi, kila wakati wanachofanya ni kutafuta makosa kwa wengine. Hilo ni kosa. Tena, mara nyingi wanawahukumu watu kimakosa, pasipo kujua ukweli wote. Kibaya zaidi ni kwamba, hao mahakimu wa kujifanya mara nyingi huwapima watu kwa viwango ambavyo wao wenyewe hawaviwezi, na kujifanya wanafiki kwa tendo hilo. “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kutupa jiwe” (Yohana 8:7).

Tabia aina hiyo ndiyo Yesu alikuwa anazungumzia. Mtume Yakobo aliandika hivi: “Ndugu! Msinung’unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango” (Yakobo 5:9). Hii ni dhambi moja ambayo ni kubwa sana katika kanisa siku hizi, na wale ambao wana hatia ya kuwahukumu wengine hujiweka kwenye nafasi hatari ya kuhumiwa na wao. Tunapozungumza kinyume cha mwamini mwingine, tukionyesha makosa yake kwa wengine, tunajifanya mahakimu. Tunaivunja amri kuu kwa sababu, sisi hatupendi wengine watuseme vibaya tukiwa hatupo. Na tunapozungumza na mwamini mwingine juu ya makosa yake wakati sisi wenyewe tuna makosa makubwa zaidi tunakuwa sawa na yule mtu mwenye boriti katika jicho lake. Lawama kwa upendo na kwa kusudi la kujenga zinapaswa kutolewa na mtu ambaye hana matatizo kama au zaidi ya huyo anayesaidiwa. Watu wengi wa kiroho ninaowafahamu mimi hawatoi ushauri mwingi bila ya kuombwa, kwa sababu wanajua kwamba watu wengi hawataki kusikiliza ushauri. Pengine hiyo ndiyo maana ya Yesu katika maneno aliyosema katika mstari huu, kwamba:

“Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua” (Mathayo 7:6).

Pia, Mithali moja inasema: “Usimkaripie mwenye dharau, asije akakuchukia; mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda” (Mithali 9:8).

Himizo Kusali

Hatimaye tunafika kwenye sehemu ya mwisho ya mahubiri ya Yesu. Sehemu hii inaanza kwa ahadi za kutia moyo sana juu ya sala, kama ifuatavyo:

“Ombeni nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni nanyi mtafunguliwa. Kwa maana, kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu ambaye, mwanawe akimwomba mkate atampa jiwe? Au akiomba samaki atampa nyoka? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?” (Mathayo 7:7-11).

Kuna msomaji anasema, “Aha! Hii sehemu ya Mahubiri ya Mlimani haihusiki na mambo ya utakatifu.”

Inategemeana na kile tunachoomba, tunachobishia hodi na tunachotafuta katika sala. Sisi kama wenye “njaa na kiu ya haki” tunatamani kutii kila kitu ambacho Yesu ameagiza katika mahubiri yaliyotangulia, na shauku hiyo inaonekana katika sala zetu. Ukweli ni kwamba, ile sala ‘mfano’ ambayo Yesu alifundisha katika mahubiri Yake hapo nyuma ni maonyesho ya shauku kwamba mapenzi ya Mungu yafanyike, na utakatifu upatikane. Tena, tukisoma ahadi za sala kama zipatikanavyo katika Injili ya Luka, maneno yafuatayo ndiyo yanayomalizia: “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?” (Luka 11:13). Bila shaka Yesu hakuwa anafikiri juu ya magari ya kulala ndani au mitumbwi ya kustarehe wakati alipotuahidi “vipawa vyema”. Kwa mawazo Yake, Roho Mtakatifu ni “kipawa chema” kwa sababu Roho Mtakatifu hutufanya watakatifu na hutusaidia kueneza Injili inayowafanya wengine kuwa watakatifu. Na watakatifu wanakwenda mbinguni.

Hitimisho

Sasa tunafikia mstari ambao unaweza kuhesabika kuwa hitimisho la kila kitu ambacho Yesu amesema mpaka hapa. Wataalamu wengi wa Biblia wanashindwa kuuona, lakini ni muhimu sisi tusiukosee. Mstari huu bila shaka ni maneno ya kuhitimisha, maana unaanza kwa neno “basi”. Unaunganika na yale mafunzo yaliyotangulia, na swali ni hili: Je, unafanya majumuisho kiasi gani cha maneno ya Yesu? Tuusome na kufikiri juu yake.

“Basi yoyote mtakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii” (Mathayo 7:12).

Maneno hayo si hitimisho la mistari michache iliyotangulia – yenye kuzungumza juu ya sala – kwa sababu kama ni hivyo, haileti maana.

Kumbuka mapema kabisa katika mahubiri Yake kwamba Yesu alikuwa ameonya kuhusu kosa la kudhani kwamba amekuja kuibatilisha Torati na manabii (ona Mathayo 5:17). Tangu hapo mpaka mstari huu tunaotazama sasa, hajafanya kitu kingine chochote isipokuwa kuunga mkono, kufafanua na kueleza zaidi amri za Mungu katika Agano la Kale. Kwa hiyo, sasa anahitimisha kila kitu alichoamuru – yaani, vyote alivyotaja kutoka kwenye Torati na Manabii, hivi: “Basi yoyote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo Torati na manabii” (7:12). Maneno “Torati na Manabii” huunganisha kila kitu alichosema Yesu kati ya Mathayo 5:17 na 7:12.

Uhusiano kati ya wokovu na kushika kile tunachokijua sasa kuwa ni “Amri Kuu” unawekwa wazi katika mistari miwili inayofuata, inayosema hivi:

“Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache” (Mathayo 7:13-14).

Bila shaka mlango ule mwembamba na njia iendayo uzimani ambayo wachache wanaiona ni mfano wa wokovu. Mlango ule mpana na njia pana iendayo upotevuni, ambayo ni ya wengi, ni mfano wa kupotea. Kama kila kitu ambacho Yesu alisema kabla ya maneno haya kina maana, na kama mahubiri haya yanakwenda kwa mpangilio, na kama Yesu alikuwa msemaji mzuri mwenye kutumia ufahamu Wake, basi tafsiri ya kimsingi kabisa ni kwamba njia ile nyembamba ni njia ya kumfuata Yesu, kutii amri Zake. Njia ile pana ni tofauti ya hayo. Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo wanaopita kwenye ile njia nyembamba ambayo Yesu aliifunua katika Mathayo 5:17 hadi 7:12? Kama wewe ni mtu unayekwenda na wengi, ujue uko kwenye njia iliyo pana.

Inasumbua kwa wengi wanaojiita Wakristo kwamba Yesu hakusema chochote juu ya imani au kumwamini Yeye katika mahubiri haya ya wokovu. Lakini, wale ambao wanaelewa kwamba imani na mwenendo havitenganishwi hawapati shida na mahubiri haya. Watu wanaomtii Yesu huonyesha imani yao kwa matendo yao. Wale wasiomtii hawaamini kwamba ni Mwana wa Mungu. Tena, si wokovu tu ulio ishara ya neema ya Mungu kwetu, bali hata yale mabadiliko ambayo yametokea maishani mwetu. Kwa kweli, utakatifu wetu ni utakatifu Wake.

Jinsi Ya Kutambua Viongozi Wa Kidini Wa Bandia

Baada ya hayo, Bwana Yesu aliwaonya wasikilizaji Wake juu ya manabii wa uongo, viongozi wa kidini wenye kuwaongoza wasiofikiri kuifuata njia pana iendayo upotevuni. Kuna wale ambao ujumbe wao hautoki kwa Mungu kabisa, na waalimu wa uongo wanaangukia katika fungu hili pia. Wanawezaje kutambulika kwamba ni waongo? Kwa njia ile ile ya kuwatambua waamini wa bandia.

“Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo walakini kwa ndani ni mbwa mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao. Je! Watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua. Si kila mtu aniambiaye, ‘Bwana Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, ‘Bwana, Bwana! Hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?’ Ndipo nitawaambia dhahiri, ‘Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu ninyi mtendao maovu’.” (Mathayo 7:15-23).

Waalimu wa uongo ni wadanganyifu sana. Wana mambo ya nje yenye kuonyesha kwamba pengine ni watu sawa. Wanaweza kumwita Yesu Bwana wao, wanaweza kutoa unabii, wanaweza kutoa pepo na hata kutenda miujiza. Lakini yale “mavazi ya kondoo” yanaficha “mbwa-mwitu mkali.” Wao si kondoo kihalisi. Itajulikanaje kama ni wa kweli au si wa kweli? Tabia yao ya kweli itajulikana kwa kutazama “matunda” yao.

Je, hayo matunda anayozungumzia Yesu ni matunda gani? Ni matunda ya utii kwa kila kitu alichofundisha. Wale ambao ni wa kweli hufundisha na kufanya mapenzi ya Baba. Wale ambao si wa kweli hufundisha kisichokuwa kweli na hutenda “maovu” (7:23). Basi, wajibu wetu sisi ni kulinganisha maisha yao na mafundisho yao na kile ambacho Yesu alifundisha na kuamuru.

Waalimu wa uongo ni wengi sana siku hizi kanisani, nasi hatupaswi kushangaa kwa sababu Yesu pamoja na Paulo walituonya kwamba, kadiri siku za mwisho zinavyokaribia, tutazamie hayo (ona Mathayo 24:11; 2Timo. 4:3-4). Manabii wa uongo ambao ni maarufu katika siku zetu ni wale wenye kufundisha kwamba mbingu inawangojea wale ambao si watakatifu. Wao wanawajibika kwa kupotea kwa mamilioni ya watu. John Wesley – mhubiri maarufu wa siku zilizopita – aliandika hivi juu yao:

“Ni kitu kibaya sana wakati mabalozi wa Mungu wanapogeuka kuwa mawakala wa Shetani! Wakati wale walioagizwa kuwafundisha watu njia ya kwenda mbinguni wanapofundisha njia ya kwenda jehanamu. Nikiulizwa, ‘Nani wamewahi kufanya hivyo?’ jibu langu ni rahisi tu: ‘Makumi elfu ya wenye hekima na heshima kubwa; wale wote wa dhehebu lolote, wanaowatia moyo – wenye kiburi, wenye tamaa, wenye dhihaka, wenye kuipenda dunia, wanaopenda starehe na anasa, wasiokuwa wema, watu wa ovyo-ovyo, wasiojali, wasiodhuru, watu wasiopatikana na mateso kwa sababu ya haki – kwamba wako njiani kwenda mbinguni.’ Hao ni manabii wa uongo wa hali ya juu sana. Hao ni wasaliti, wa Mungu na mwanadamu. Wanawaelekeza watu kuingia katika dunia ya giza; na wakati wao utakapofika kuwafuata hao maskini waliowaangamiza, “kuzimu chini itataharuki” kuwalaki!”

Cha kupendeza ni kwamba Wesley alikuwa anafafanua kuhusu waalimu wa uongo ambao Yesu alionya juu yake katika Mathayo 7:15-23.

Ona tena kwamba Yesu anazungumza wazi kabisa – kinyume na jinsi waalimu wengi wa uongo wanavyotuambia siku hizi – kwamba wale wasiozaa matunda mazuri watatupwa jehanamu (ona 7:19). Hayo hayatawapata waalimu tu na manabii, bali kila mmoja. Yesu alisema, “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21). Niwie radhi nikirudia kusema tena kwamba haya ni mahubiri kuhusu mlingano kati ya wokovu na utakatifu. Watu ambao hawamtii Yesu wanakwenda jehanamu.

Pia ona Yesu alivyounganisha jinsi mtu alivyo ndani na jinsi alivyo nje. Miti “mizuri” huzaa matunda mazuri. Miti “mibaya” haiwezi kuzaa matunda mazuri. Chanzo cha matunda mazuri ambayo huonekana kwa nje ni asili ya mtu kwa ndani. Mungu amebadilisha asili ya wale watu ambao wamemwamini Yesu kweli kweli.

Kumalizia

Yesu anamalizia mahubiri Yake yote kwa mfano. Bila shaka ni mfano wenye kuonyesha mahusiano kati ya wokovu na utii.

“Basi, kila asikiaye hayo maneno yangu na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa” (Mathayo 7:24-27).

Mfano wa mwisho wa Yesu si “njia ya kufanikiwa maishani” kama wengine wanavyotumia. Mada siyo jinsi ya kufanikiwa kifedha wakati mambo ni magumu, kwa kuziamini ahadi za Yesu. Hili ni hitimisho la yote ambayo Bwana Yesu alisema katika Mahubiri Yake pale Mlimani. Wale wanaotenda aliyosema ni wenye hekima nao watadumu; hawana haja ya kuogopa ghadhabu au hasira ya Mungu. Wale wasiomtii Yeye ni wapumbavu na watateseka kweli, na kupata “adhabu ya kuangamia milele” (2Wathes. 1:9).

Kujibu Hoja Inayopinga

Je, haiwezekani kwamba Mahubiri ya Yesu pale Mlimani yaliwahusu wafuasi Wake walioishi kabla ya kifo Chake na kufufuka? Wao si walikuwa chini ya Torati, ambayo ilikuwa njia yao ya wokovu wakati huo, lakini baada ya Yesu kufa kwa ajili ya dhambi zao wakaokolewa kwa imani, kitu kilichobatilisha njia ile ya wokovu inayotajwa katika mahubiri haya?

Nadharia hiyo ni mbaya. Hakuna mtu yeyote ambaye amewahi kuokolewa kwa matendo yake wakati wowote. Kila mara imekuwa ni kwa imani – kabla ya Agano la Kale na hata wakati wa Agano la Kale. Paulo anaonyesha katika Warumi 4 kwamba Ibrahimu alihesabiwa haki kwa imani, sio kwa matendo.

Zaidi ya hapo, ilikuwa vigumu kabisa kwa yeyote katika wasikilizaji wa Yesu kuokolewa kwa matendo, maana wote walikuwa wametenda dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu (ona Warumi 3:23). Ni neema ya Mungu tu ndiyo ingewaokoa, na imani tu ndiyo yenye uwezo wa kupokea neema Yake.

Bahati mbaya sana ni kwamba, wengi katika kanisa siku hizi huziona zile amri zote za Yesu kwamba hazina kusudi lingine isipokuwa kutufanya tujisikie hatia, ili tuone jinsi isivyowezekana kupata wokovu kwa matendo. Sasa, kwa kuwa “tumepata ujumbe” na kuokolewa kwa imani, tunaweza kupuuzia amri Zake karibu zote. Isipokuwa kama tunataka wengine nao “waokoke”. Ndipo tunapoweza kuchomoa tena zile amri na kuwaonyesha watu jinsi walivyo wenye dhambi ili nao waweze kuokolewa kwa “imani” isiyo na matendo.

Yesu hakuwaambia wanafunzi Wake hivi: “Enendeni ulimwenguni mwote mkawafanye watu kuwa wanafunzi. Halafu, hakikisheni kwamba, wakisha jua wana hatia na kuokolewa kwa imani, amri Zangu zimemaliza makusudi yake maishani mwao.” Aliwaambia kama ifuatavyo: “Basi, enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi … na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi …” (Mathayo 28:19-20 – Maneno mepesi kutilia mkazo).