Hello Visitor   |  Login  |   Create an account!

Yaliyomo | Sura Iliyopita | Mwisho wa Ukurasa | Pa Kuanzia

Unaruhusiwa kuchapa, kunakili, kugawa au kusambaza haya kwa njia yoyote ile, mradi tu usibadili chochote wala kukata chochote. Vile vile hairuhusiwi kuuza maelezo haya. © Haki zote zimehifadhiwa David Servant

SURA YA KUMI NA MBILI
Lini Uamsho?

Nimepokea barua kutoka kwa mtu aliyenisikia nikipinga mafundisho ya wanaopinga kushika sheria kwenye redio. Anasema ni barua yake ya kwanza kuandika baada ya miaka kumi na mbili.

Alikiri kwamba yeye alikuwa shoga mtendaji. Kwa muda mrefu alikuwa akijihesabia haki kwamba, kama alikuwa anatenda matendo mema na kuamini kuhusu Yesu, alikuwa salama. Lakini akanisikia nikisema jinsi Biblia inavyosema kuhusu neema ya Mungu inayobadilisha, ipatikanayo kwa ajili ya wenye dhambi, ikiwa ni pamoja na walawiti. Alinisikia nikisoma Maandiko yasemayo kwamba hakuna mlawiti atakayeurithi ufalme wa Mungu. Baada ya kutambua kwamba imani yake iliyokufa inampeleka jehanamu, alitubu. Ameniandikia kuniambia kwamba yeye si mlawiti tena, na kwa herufi kubwa akakariri maneno machache ya 1Wakorintho 6:11, kwamba: “NA BAADHI YETU TULIKUWA HIVYO.” Ameokolewa kwa neema ya Mungu na kubadilishwa.

Kama wanaofundisha kwamba kushika sheria ni makosa wangefanikiwa, huyu mtu angedumu kuwa mlawiti mtendaji, anayekwenda jehanamu milele. Lakini – sifa kwa neema ya Mungu – aliskia kweli na kuiamini. Kama Yesu alivyoahidi katika Yohana 8:32, ukweli umemweka huru.

Je, Huru Kutokutii?

Pengine hakuna andiko ambalo limetumiwa vibaya na wale wanaopinga kushika sheria kama Yohana 8:32. Wao wanazungumzia jinsi kweli inavyotuweka huru kutokana na kile wanachokiita “utumwa wa Torati”, lakini kinachoitwa na Biblia utii kwa amri zilizo wazi kabisa za Mungu. Wakati Yesu alipozungumza kuhusu kweli kutuweka huru, alikuwa anazungumza juu ya uhuru kutoka dhambini.

Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, ‘Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.’ Wakamjibu, ‘Sisi tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu wakati wowote; nawe wasemaje Mtawekwa huru?’ Yesu akawajibu, ‘Amin amin nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli (Yohana 8:31-36. Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Huu ndiyo ujumbe wa neema ya Mungu inayobadilisha. Hiyo ndiyo Injili. Yesu husamehe na kuwaweka wamwaminio huru kutoka dhambi. Wale wanaomwamini Yeye kweli watadumu – wataishi – katika Neno Lake, wakijithibitisha kwamba ni wanafunzi Wake.

Uamsho Wa Kishetani

Sasa hivi ni wakati wa giza. Jamii yetu ni kama gari moshi la mizigo ambalo halina breki, na linaongeza mwendo. Litaendelea kwa muda gani kabla ya kuondoka kwenye reli? Lakini, tunawezaje kulia kuhusu kuporomoka kwa hali ya kiroho ya taifa letu na wakati huo huo tunatoa injili ambayo haina nguvu zozote za kubadilisha maisha – injili ambayo si kitu zaidi ya nafasi ya watu kutenda dhambi? Tunawezaje kutazamia uamsho wakati neema ya Mungu inageuzwa kuwa kibali cha ufisadi?

Muda wote ambao lengo letu litakuwa kujaza viti kwa jina la “kukuza kanisa” badala ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi, hautakuwepo uamsho wa kweli. Tutakapoendelea kuwaona watu kwamba “hawaendi kanisani” badala ya kuwaona kwamba hawajaokoka, hautakuwepo uamsho wa kweli. Muda wote ambapo wachungaji na wainjilisti wanajali zaidi kuwapendeza watu badala ya kumpendeza Mungu, uamsho wa kweli hautakuja. Uamsho wa kweli hauwezi kuwepo mpaka kanisa litakaporudisha ile Injili ya Biblia, na kuwa na sifa ya utakatifu mpaka liwe tofauti na dunia. Kabla ya hapo, uamsho wa pekee utakuwa ule unaoendelea kwa sasa wa Kishetani, wenye kuchochewa na neema bandia, imani bandia na wokovu bandia. Wakitumia bango la uhuru kiroho, wainjilisti wake (Shetani) wataendelea kumwaga uongo wake kwa maandishi, kwenye redio na televisheni za Kikristo, na kutoka kwenye mimbari makanisani. “Nendeni mkatende dhambi. Hamtakufa.”

Kweli, wakati ni wa giza. Makundi ya waalimu maarufu wanatangaza kwamba kama mtu anamwamini Yesu hata kwa nukta kumi tu maishani mwake, kisha aiache imani na kurudia maisha ya kutenda dhambi, ameokoka, na ni salama milele. Kumbuka kwamba mtu huyo tunayemfikiri tu anaweza kuwa kahaba anayeendelea na ukahaba wake, au mbakaji mpaka wakati wa kifo chake. Bado atakwenda mbinguni. Atakachopoteza ni thawabu fulani huko mbinguni ambazo angeweza kupata kama angekuwa Mkristo bora zaidi kidogo! Je, huko sio kugeuza neema ya Mungu kuwa ufisadi? Je, mahubiri aina hiyo kweli yataleta uamsho? Lakini, Biblia bado inasema hivi:

Ni neno la kuaminiwa:
Kwa maana, kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia.
Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye. Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi. Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa maana hawezi kujikana mwenyewe (2Timo. 2:11-13. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Je, mstari huu unafasiriwaje na waalimu wa kisasa wa neema bandia? Wakipuuza au kupindua mistari ile mitatu ya kwanza, wao wanakaza kwamba mstari wa nne unathibitisha hoja yao. Wanasema hivi: “Hata kama sisi hatuamini, tukiacha imani yetu, yeye hudumu kuwa mwaminifu wa kutuokoa.”

Lakini, hiyo ndiyo maana yake? Hapana kamwe!

2Timotheo 2:11-13 Inafundisha Nini?

Kwanza: Paulo anasema, “Kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia.” Kuishi kwetu pamoja Naye kunategemeana na kufa kwetu pamoja Naye. Maandiko yanafundisha kwamba wote wanaomwamini Yesu kweli wamekufa na kufanywa hai ndani ya Kristo. Huko ndiko kuzaliwa mara ya pili, kwa njia ya Roho Mtakatifu. Ni badiliko kubwa sana.

Pili: Paulo anasema, “Tukistahimili, tutamiliki pamoja naye.” Hapa si kwamba anatoa ahadi ya thawabu maalum ya kutawala wakati ujao kwa kundi maalum la Wakristo watakaostahimili. Anaahidi kitu kinachomngojea kila mwamini wa kweli ambaye imani yake itastahimili. Maandiko yanafundisha kwamba si kundi maalum la Wakristo litakalotawala pamoja na Yesu. Wote walionunuliwa kwa damu Yake watatawala pamoja Naye.

Nao waimba wimbo mpya wakisema, ‘Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi’ (Ufunuo 5:9-10. Maneno mepesi kutilia mkazo. Pia ona 20:6; 22:3-5).

Waamini wale watakaostahimili katika imani ya kweli wanayo ahadi ya kutawala pamoja na Yesu. Ni lazima tudumu katika imani ili tuokoke mwishoni, na kama tutafanya hivyo, tutatawala pamoja na Yesu.

Tatu: Paulo anatoa onyo kuhusu kutostahimili. “Tukimkana, yeye naye atatukana sisi.” Hayo ni maneno yaliyokaririwa kutoka kwa Bwana Yesu Mwenyewe. Alisema hivi:

“Basi kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu yeyote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni “ (Mathayo 10:32-33. Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Hapo Yesu – bila ya kutafuna maneno – aliahidi kwamba kama tukimkana, Naye atatukana. Ni onyo kwa yeyote anayefikiria kuacha imani yake, au kutostahimili kwa sababu ya mawazo ya watu au watakachomfanyia. Je, watu ambao Yesu atawakana mbele za Baba Yake wataruhusiwa kuingia mbinguni? Je, tukimkana Yesu kwa kusema, “Simjui” mbele ya watu, na Yeye atukane mbele za Baba akisema, “Simjui”, tutaokoka? Jibu unalo wewe.

Mwisho Paulo anasema, “Tusipomwamini, Yeye anadumu kuwa wa kuaminika; maana hawezi kujikana mwenyewe.” Ni maendeleo ya kile alichosema kuhusu kumkana Yesu. Hata ingawa tunaweza kushindwa kutimiza ahadi yetu ya kumfuata, Yesu atatimiza ahadi Zake zote kila wakati. Aliahidi kutukana ikiwa tutamkana, Naye atafanya hivyo. (Tukirejea kwa toba na imani, atatunza ahadi Yake ya kutupokea.)

Ona kwamba katika tamko la nne Paulo hakusema hivi: “Tusipoamini na tukimkana, Yeye atadumu kuwa mwaminifu, na hatatukana.” Hiyo ingekuwa kinyume kabisa na alichokisema katika tamko la tatu!

Hapana. Mungu daima ni mwaminifu japo watu sio. Yeye kila mara anatimiza ahadi Zake pamoja na hukumu Zake. Hebu fikiri wanavyosema Musa na Yoshua kuhusu uaminifu wa Mungu.

Basi jueni ya kuwa BWANA Mungu wenu ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake hata vizazi elfu; naye huwalipa wamchukiao mbele ya uso wao, kuwaangamiza. Hatakuwa mlegevu kwake yeye amchukiaye, atamlipa mbele ya uso wake (Kumbu. 7:9-10. Maneno mepesi kutilia mkazo).

Kisha itakuwa, kama yalivyowafikilia yale mambo mema yote, BWANA Mungu wenu aliyowaahidia ninyi, kadhalika BWANA atawafikilizia mabaya yote, hata atakapokuwa amewaangamiza katika nchi hii njema, BWANA Mungu wenu aliyowapa (Yoshua 23:15 – Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).

Hayo yakiwa bado akilini mwetu, hebu tuone jinsi ambavyo mmoja katika waalimu maarufu sana wanaopinga kushika sheria, ambaye jina lake linajulikana sana, anavyotafsiri 2Timotheo 2:11-13. Anasema hivi:

Kama ambavyo walio waaminifu watakavyotambuliwa na kupokelewa na Baba, ndivyo na wasio waaminifu watakavyokosa kutambuliwa … Mwamini asiye mwaminifu hatapata nafasi maalum katika ufalme wa Kristo kama wale watakaobahatika kuruhusiwa kutawala pamoja naye. … Maana ya mtume ni dhahiri, kwamba: Hata kama mwamini atafanyika asiyeamini – kwa hali yoyote ile – wokovu wake hauko hatarini. Kristo atadumu kuwa mwaminifu (Maneno mepesi ni kutilia mkazo).

Wakati kanisa – tena kwa furaha – linapomeza mafundisho yenye kubadilisha kabisa maana ya Maandiko, kuna haja ya kuuliza ni kwa nini hakuna uamsho? Ujumbe mtakatifu wa Mungu umehaririwa, umetolewa kila sababu ya mtu yeyote kutubu dhambi na kumfuata Yesu Kristo. Watu wasiomwamini Yesu sasa wanaweza kufika mbinguni, hakika kabisa. Mtu anaweza kuwa asiyeamini kwamba kuna Mungu, au Mbuda, au Mwislamu au mwenye kumwabudu Shetani na bado aende mbinguni, mradi ametamka kwamba anamwamini Yesu kwa nukta chache tu katika maisha yake. Na uongo huu unatangazwa na waalimu walio maarufu katika imani ya kiinjili katika duniani.

Sasa?

Kama ulikuwa huelewi Injili ya kweli kabla ya kuanza kusoma kitabu hiki, bila shaka sana unaielewa. Labda uamsho umeanza maishani mwako. Kwani, uamsho mkubwa ni kitu gani kama siyo watu wengi binafsi wakihuishwa? Unaweza na unatakiwa kuwaambia wengine kile unachojua mpaka sasa. Sawa na mimi, wewe sasa una wajibu mtakatifu wa kueneza ukweli, bila kujali gharama. Ujumbe wetu ni ule ule uliotangazwa na Yesu, na Yuda, na Petro, na Paulo, na Yakobo na Yohana, na mamilioni ya waamini wa kweli waliotutangulia. Tusije tukaionea “haya injili, ni uweza wa Mungu uletao wokovu kwa kila aaminiye” (Warumi 1:16).

Je, utakuwepo uamsho wa kweli? Ndiyo – katika maisha ya kila atakayesikia na kujali Injili ya kweli. Wale walioamshwa kweli kweli wataomba na kujitahidi ili wengine waweze kushiriki furaha yao. Wazo hilo likiwa akilini mwako, naomba nimalizie kwa mfano ambao Bwana alinipa, unaonijaza matumaini makubwa sana ………

Mfano Wa Uamsho …

Nilipokuwa nafunga na kuomba kuhusu hitaji la uamsho na kazi ya Roho Mtakatifu, nilipokea ufunuo ulionisaidia kuelewa ni kitu gani kinachotokea na kitakachotokea kwa kanisa. Hayakuwa maono niliyoona kwa macho yangu, bali ufunuo “niliouona” katika moyo wangu. Naomba niseme kwamba mimi si mtu “wa mafunuo,” na hii ilikuwa mara ya kwanza kwa kitu kama hicho kunitokea. Hebu nieleze nilichoona.

KWANZA: Niliona makundi ya watu. Mengine yalikuwa makubwa sana, mengine ya wastani, mengine madogo sana. Makundi yale makubwa yalikuwa na watu maelfu. Makundi yale madogo sana yalikuwa na watu kichele – wachache tu. Watu wa kila kundi walisogeleana na kujikunyata pamoja ili wapate joto, maana kulikuwa baridi sana sana. Wote walikuwa wanatetemeka, na mtu aliposema kitu, ungeweza kuona pumzi yake ikitokea. Tena, wengi katika makundi hayo walikuwa wachafu. Kuna waliokuwa wachafu kuliko wengine, kana kwamba walikuwa wafanyakazi katika machimbo ya makaa ya mawe, wamefunikwa na majivu na masizi toka kichwani hadi vidoleni. Hao walikuwa wananuka pia, kama takataka. Wengine hawakuwa wachafu hivyo, lakini wengi walihitaji kusafishwa.

Watu wote hao walikuwa wamesimama chini ya bwawa kubwa sana lililokuwa na maji mengi mno. Lilikuwa refu sana – futi mia nyingi kwenda juu – na lilikuwa pana, kiasi cha upeo wa macho kwenda pande zote. Maji yaliyokuwemo ndani yake yalikuwa mengi sana.

Nilipotazama kwa karibu zaidi, niliona kwamba lilikuwa limejengwa kwa kutumia matofali. Kuna maneno yaliyokuwa yameandikwa kwenye kila tofali, nami nilipoanza kuyasoma, niligundua kwamba yote yanafanana, maana kilichoandikwa kilikuwa dhambi fulani. Kwa mfano: Tofali moja lilikuwa limeandikwa “Msengenyaji”, na lingine, “Mwenye Tamaa”. Pia, chini ya kila dhambi lilikuwepo jina la mtu. Kwa mfano: Tofali lililoandikwa “Mwongo” lilikuwa na jina la mtu chini yake: “Sauli”. Yalikuwepo matofali mengi yaliyokuwa yameandikwa dhambi ile ile moja, na majina mengi ya watu yalikuwa yameandikwa kwenye tofali zaidi ya moja.

Nikawatazama tena wale watu wengi – wachafu, wanatetemeka kwa baridi. Karibu wote walikuwa wamesimama, ila mmoja-mmoja katika kundi angepiga magoti, au angeanguka kifudifudi na kuanza kuomboleza na kutubu dhambi zake na kumwomba Mungu amsafishe. Kila mtu anapofanya hivyo, tofali moja lingechomoka kutoka mahali pake kwa nguvu ya maji, na likichomoka hivyo, linapasuka-pasuka na kuwa vumbi, kisha linatoweka. Kisha, maji yangetokea hapo lilipotoka tofali na kuanza kuelekea kwa huyo aliyepiga magoti, na kumsafisha uchafu wake wote. Wakati mwingine matofali zaidi ya moja yangechomoka kutoka kwenye ukuta huo – ama yote kwa pamoja au mojamoja kwa kitambo fulani – mradi yule mtu aliendelea kupiga magoti na kuomba. Maji yote yaliyotokea kwenye nafasi hizo yangemwangukia kwa nguvu sana yule mtu mmoja aliyekuwa amepiga magoti akiomba, na badiliko katika jinsi alivyokuwa anaonekana lilikuwa kubwa. Baadhi ya waliokuwa wachafu zaidi wakawa ndiyo wasafi kuliko wengine, katika kipindi kifupi tu.

Pia nikaona, yale maji yaliyotoka kwenye lile bwawa yalikuwa na joto. Yalipowapiga wale waliopiga magoti, si tu kwamba yaliwasafisha bali pia yaliwapa joto kabisa. Wangecheka kwa furaha na kuimba wakati wakisafishwa.

Wale wengine waliokuwa wamesimama na kuwatazama waliopiga magoti walikuwa na maitikio tofauti. Mara nyingi, wale waliokuwa karibu na mwenye kupiga magoti walikuwa wanasogea, wasitake kulowa. Wakati mwingine, kundi zima lingerudi nyuma mbali, na yule aliyepiga magoti angebaki peke yake katika maji yake yanayomwagika.

Ila pia, mara kadhaa wengine katika waliosimama karibu na aliyepiga magoti wangepiga magoti hata wao, wakitubu dhambi zao. Hapo tena matofali yangechomoka kutoka kwenye ule ukuta na maji yangewamwagikia, yakiwasafisha na kuwapa joto.

Wakati mwingine idadi kubwa tu ya waliokuwa wamesimama katika kundi moja mmoja baada ya mwingine wangeanza kupiga magoti au kuinama na kuanza kuomboleza kwa ajili ya dhambi zao, na nguvu ya yale maji mengi yaliyowafikia zingekuwa kubwa na nyingi, na kuleta baraka kubwa sana, upako wenye nguvu na karama nyingi. Lakini, sikuona kundi lolote ambapo kila mmoja aliyekuwemo alipiga magoti. Mara nyingi niliona wale waliokuwa wamesimama katika makundi ambayo wengi walipiga magoti wakiondoka na kujiunga na kundi lingine ambalo wengi walikuwa bado wamesimama. Pia, wakati mwingine niliona mtu akipiga magoti kwa sababu wengine wengi walikuwa wamepiga magoti. Katika hali hiyo, hakuna tofali lililochomoka, hakuna maji yaliyomwagika kwake, na alibakia mchafu na baridi.

Niliona vitu vingine viwili: Mara kwa mara mmoja wa waliokuwa wamesimama alikuwa anatazama lile bwawa na kuona tofali lenye jina lake. Kwa sababu ya aibu, alikuwa anapanda ukuta ule na kujaribu kulichomoa kwa mikono yake. Hakuna yeyote aliyejaribu kufanya hivyo aliyefanikiwa, kwa sababu isingewezekana. Pia, mara kwa mara niliona mtu aliyekuwa amepiga magoti akisimama tena. Alipofanya hivyo, alijikuta amekuwa mchafu tena kwa njia fulani, na nguvu ya maji kumwangukia ikawa imepungua. Na kama angeanza kunyoosha kidole kwa wale ambao hawakupiga magoti, akiwalaumu kwa kinywa chake kwa maneno ya kiburi, maji yangekoma kumwagika juu yake, na akawa mchafu tena. Lakini, wengi katika waliokuwa wamepiga magoti wangesema kwa upendo na huruma nyingi sana na wale waliosimama wakiwazunguka, na kuwaambia, “Ni pazuri sana hapa kwenye maji haya yenye joto na kusafisha! Unaweza kuoshwa uchafu wako! Si uje ujiunge nami?”

Hebu nikwambie baadhi ya dhambi zilizokuwa zimeandikwa kwenye matofali hayo. Moja, lililokuwa na jina langu, lilikuwa limeandikwa hivi: “Mwenye Kuwaogopa Wanadamu.” Nilipoliona nilikiri mara moja hatia yangu mbele za Mungu na kuomba msamaha Wake na neema kwamba nisimwogope yeyote isipokuwa Mungu.

Kama mchungaji, nilionyeshwa matofali mengi tu ya watu katika kanisa langu. Yalikuwepo mengi ya dhambi zile zile. Mengine yalisema “Rafiki Na Dunia.” Mengi yalikuwa yameandikwa, “Vuguvugu”. Mengine, “Mpenda Kuhukumu Wengine.” Mengine: “Mwabudu sanamu,” ambayo maana yake ni kwamba unafanya vitu vingine maishani mwako kuwa vya maana kuliko Mungu. Watu wengi kanisani wanasisimka zaidi juu ya mambo yao ya ziada na starehe zao kuliko kwa ajili ya Mungu.

Mengine yalisema “Uchafu Katika Mahusiano Kimwili” ambao si uasherati tu, bali pia kuwa na mawazo machafu. Mengine yalisema “Hujistarehesha kwa kutazama watu wakifanya mambo machafu kwenye televisheni.” Lingine lilisema, “Anatazama Ngono kwenye internet”. Lingine lilikuwa limeandikwa “Hutafakari Matendo ya Ulawiti.” Lingine: “Kijana Anayejihusisha na Mahusiano Kimwili”.

Kwenye matofali mengine kuliandikwa hivi: “Uchungu juu ya mwingine,” “Anamnyanyasa Mke Wake,” na “Huwasema Ndugu.” Yalikuwepo yaliyosema “Mpenda Fedha,” “Mpenda Starehe” na “Anayejijali Mwenyewe.” Lilikuwepo linalosema “Hulipwa Bila Risiti Ili Akwepe Kodi,” “Msimamizi Mfujaji,” “Hutumia Fedha za Mungu Kutegemeza Mambo Ambayo Mungu Hataki” na “Asiyejali Maskini.” Mengi yalisema hivi: “Hata Zaka Hatoi” na yalikuwepo matofali mengi kuzunguka hayo yenye dhambi zenye kutetea dhambi hiyo.

Yalikuwepo yaliyoandikwa “Asiye Na Staha”, “Anayeamini Yuko Sawa Sikuzote”, na “Asiyemtii Mume Wake.” Pia niliona mengi yaliyosema, “Hajali Kuhusu Wale Ambao Hawajasikia Injili.”

Mengine yalisema, “Msengenyaji,” “Mfitini,” “Mkosoaji”, “Atumiaye lugha ya kukwaza”, na “Dini Isiyofaa – Hauzuii Ulimi Wake.” Tofali moja lilisema hivi: “Hawategemezi Watoto Wake wa Ndoa ya Kwanza.” Mengine yalisema, “Hawaheshimu Wazazi,” “Si mwaminifu kwa ahadi” na “Husikiliza muziki unaosifu mambo ambayo Mungu anachukia.”

Yalikuwepo yanayosema “Amejaa Kutokuamini,” “Tabia Mbaya na Kutawaliwa,” na “Mwenye Kujitosheleza.” Pia kulikuwa na “Kutokuomba,” “Hukosa Ibada kanisani,” na “Asiyetaka Kusoma Neno la Mungu.” Matofali mengi yalisema, “Hawafundishi watoto katika kicho cha Mungu.”

Yapo na mengine mengi ambayo sikuyataja, lakini yote yanapatikana katika Biblia – hiyo hiyo ambayo sote tunakiri kwamba tunaiamini kuwa ni Neno la Mungu. Hata matofali mengine yalikuwa yameandikwa hivi: “Hubadili Maandiko Kuyafanya Yaseme Kisichokuwepo,” na “Hutafsiri Amri Ili Zilingane na Maisha Yake.”

Sementi iliyokuwa imeshikilia yale matofali nayo ilikuwa imeandikwa maneno, kuonyesha dhambi nne zilizoshikilia zile nyingine zote. Hizo ni “Kiburi,” “Unafiki,” “Kutompenda Mungu au Kumpenda Kidogo Tu,” na “Dhambi Za Wachungaji.” Kabla ya hizo dhambi nyingine kuondolewa, hizo lazima zidhoofishwe kwanza. Kiburi kinatuzuia kukiri dhambi zetu. Unafiki – kutenda kwa njia moja kanisani na kwa nyingine mahali pengine – lazima utubiwe. Hizo zote ni ishara ya dhambi moja kubwa – “Kutompenda Mungu au Kumpenda Kidogo Tu” – maana, tungempenda kwa moyo wote, akili zote, nafsi yote na nguvu zote, tungemtumikia na kumtii kwa bidii sana. Yesu alisema, “Mkinipenda mtazishika amri zangu” (Yohana 14:15). Mwisho: Kama viongozi kanisani watakuwa mfano mbaya, wafuasi wao wana njia ya kujitetea kuendelea katika dhambi zao.

Turudi kwenye yale makundi ya watu. Nilipotazama, ilitokea mara moja moja kwamba mtu aliyekuwa amesimama angenyoosha kidole chake kwa kundi lililo karibu naye, ambamo watu walikuwa wanacheka na kuimba, huku wamepiga magoti chini ya maji yaliyokuwa yanawamwagikia, na kusema hivi: “Hayo maji hayawezi kutoka kwa Mungu, maana mafundisho yao si sawa katika maeneo fulani.” Lakini Bwana alinikumbusha kwamba Yeye hakusema ni wale tu wenye mafundisho safi ndiyo watakaomwona, bali wale wenye moyo safi (Mathayo 5:8). Yesu hakusema kwamba tutawatambua kwa mafundisho yao bali kwa matunda yao (Mathayo 7:20). Alisema kwamba alama ya wanafunzi Wake wa kweli si mafundisho makamilifu bali upendo kati yao (Yohana 13:35). Kwa kuwa mafundisho ya kundi fulani yana makosa katika maeneo fulani ambayo hata si muhimu haimaanishi kwamba Mungu hatawamwagia Roho Wake ikiwa watajinyenyekeza na kuanza kuwa na “njaa na kiu ya haki” (Mathayo 5:6). Baadhi ya matofali kwenye lile bwawa yalikuwa yameandikwa hivi: “Kujisifia Maarifa,” “Kujivunia Mafundisho,” na “Uaminifu kwa Dhehebu Zaidi ya Upendo kwa Mwili wa Kristo.”

Muda ulipoendelea kupita, wengi zaidi katika waliokuwa wamesimama walianza kupiga magoti, wakiomboleza na kuomba msamaha kwa dhambi zao na kutubu. Matofali yakachomoka kutoka kwenye lile bwawa mfano wa mahindi ya kuchoma, na maji zaidi yakamwagika kwa mlio wa nguvu na kishindo, mpaka pakawa kama Bwawa la Kidatu (ila, zaidi sana sana). Waliokuwa wamepiga magoti wakainua mikono yao, wakacheka, wakaimba na kuomba katika kitu ambacho kilikuja kuwa mto mkubwa uliobubujika hadi maeneo mengi makavu duniani. Mwishowe ukawa gharika mpaka wale waliokuwa wamepiga magoti ndani yake walisombwa na hayo maji, huku wakifurahi na kuimba nyimbo za sifa kwa Mungu wao.

Mwishoni maji yale yakaacha kutoka, maana lile bwawa lilikauka. Waliokuwa bado wamesimama walitazamana kwa majivuno ya kuridhika. Bado yale matofali yenye majina yao yalikuwepo, yameshikiliwa hapo hewani kwa kiburi cha mwanadamu tu. Mara – bila hata taarifa au ilani – kila tofali lililobaki kwenye ule ukuta lilianza kuanguka, likiungana na mengine yaliyokuwa na jina hilo hilo. Kwa hofu kubwa, waliokuwa wamesimama waliona matofali lundo yakiwaangukia kwa usahihi, kwanza yakiwaangusha chini, kisha yakiwaua na kuwaponda, mpaka kilichobakia kikawa ni malundo ya matofali tu. Nikakumbusha maneno aliyosema Yesu, kwamba “Kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa” (Luka 18:14). Vipi – wewe ni yupi kati ya hao?

Yaliyomo | Sura Iliyopita | Mwanzo wa Ukurasa | Pa Kuanzia

 

Provide a toilet for Makanka

Problem: Makanka is from Zimbabwe and she has Spina Bifida. Her family has a hole in their backyard they use for a toilet but it is too difficult for Makanka to use by herself.
Solution: An indoor Western-style toilet will allow Makanka to use the toilet by herself without injury.
Still Needed: $245. Any size
gift will help.

Popular Teaching Categories