Tulipojifunza Mahubiri ya Yesu pale Mlimani katika sura fulani iliyotangulia, tulijifunza jinsi ilivyo muhimu kwamba tuwasamehe wale wanaotukosea. Tusipowasamehe, Yesu alisema wazi kwamba Mungu hatatusamehe (ona Mathayo 6:14, 15).
Sasa basi – nini maana ya kumsamehe mtu? Hebu tutazame Maandiko yanavyofundisha.
Yesu alifananisha msamaha na tendo la kumfutia mtu deni lake (ona Mathayo 18:23-35). Hebu fikiri: Una mtu unayemdai, kisha unamfungua, kwamba asikulipe. Unapasua karatasi iliyokuwa imeandikwa deni lake. Hutazamii kulipwa tena, nawe umeacha hasira na mdeni wako. Unamwona kitofauti kuliko ilivyokuwa wakati bado unamdai.
Tutaelewa vizuri tena maana ya kusamehe kama tutatafakari maana ya kusamehewa na Mungu. Wakati Yeye anapotusamehe sisi dhambi fulani, hatuhesabu kuhusika tena kwa kile tulichofanya, kilichomchukiza. Haendelei kuwa na hasira nasi kwa sababu ya dhambi ile. Hatatuadhibu wala kutuhukumu kwa tulichofanya. Tunakuwa tumepatanishwa Naye.
Vivyo hivyo basi, kama kweli nitamsamehe mtu fulani, ninamweka huru mtu huyo moyoni mwangu, nikishinda shauku ya kutafuta haki au kisasi kwa kuonyesha rehema. Sina hasira tena na mtu aliyenitenda dhambi. Tunakuwa tumepatanishwa. Kama ninaweka hasira au uchungu dhidi ya mtu fulani, ni kwamba sijamsamehe.
Mara nyingi Wakristo hujidanganya wenyewe katika swala hili. Wanasema wamemsamehe mtu, wakijua kwamba hivyo ndivyo wanavyotakiwa kufanya, lakini bado wana kitu ndani yao kuhusu aliyewakosea. Wanamkwepa mkosaji kwa sababu inasababisha ile hasira iliyofunikwa kutokea tena. Ninajua hayo maana ha ta mimi nimewahi kufanya hivyo. Tusijidanganye. Kumbuka kwamba Yesu anatukataza hata kumkasirikia mwamini mwenzetu (ona Mathayo 5:22).
Sasa – Tujiulize swali hili: Ni yupi aliye rahisi kusamehe – ni mkosaji anayeomba msamaha au ni mkosaji asiyeomba msamaha? Bila shaka sote tutakubaliana kwamba ni rahisi zaidi kumsamehe mkosaji anayekiri kosa lake na kuomba msamaha. Ni ukweli kwamba ni rahisi zaidi sana kumsamehe mtu anayeomba msamaha kuliko mtu ambaye haombi. Kumsamehe mtu asiyetaka kusamehewa huonekana kama kitu kisichowezekana.
Hebu tulitazame kwa upande mwingine. Kama kukataa kumsamehe mkosaji anayetubu na kama kukataa kumsamehe mkosaji asiyetubu ni makosa, dhambi kuu zaidi hapo ni ipi? Nadhani tutakubaliana kwamba kama vyote viwili ni kosa, basi kukataa kumsamehe mkosaji anayetubu ni uovu mkubwa zaidi.
Cha Kushangaza Kutoka Maandiko
Hayo yaliyotangulia yanasababisha swali lingine – Je, Munguanatazamia tumsamehe kila mtua nayetukosea, hata wale wasiojinyenyekeza na kukiri dhambi yao na kuomba msamaha?
Tukitazama Maandiko kwa karibu tutagundua kwamba jibu ni “Hapana.” Wakristo wengi watashangaa kujua kwamba, Maandiko yanaweka wazi kuwa ingawa tunaagizwa kumpenda kila mtu, hatutakiwi kumsamehe kila mtu.
Kwa mfano: Je, Yesu anatazamia sisi tumsamehe mwamini mwenzetu anayetukosea? Hapana. Vinginevyo, asingetuambia kufuata zile hatua nne za upatanisho zilizo katika Mathayo 18:15-17, ambazo mwisho wake ni kutengwa, kama mkosaji hatatubu.
Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye wewe na yeye peke yenu. Akikusikia, umempata nduguyo. La kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa, na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru.
Ni kwamba, ikiwa hatua ya nne itafikiwa (ya kutengwa), msamaha hautolewi kwa mkosaji, maana msamaha na kutengwa ni vitu visivyoambatana. Ingekuwa kitu cha ajabu kumsikia mtu akisema hivi: “Tulimsamehe, kisha tukamtenga.” Maana, kusamehe huishia kwenye upatanisho, sio kutengana. (Jiulize: Ungefikiriaje kama Mungu angesema, “Ninakusamehe, lakini hatuna mahusiano na wewe kuanzia leo”?) Yesu alituambia huyo aliyetengwa awe kama “mtu wa Mataifa na mtoza ushuru,” aina mbili za watu ambao Wayahudi hawakushirikiana nao kabisa, tena waliwakwepa.
Katika zile hatua nne ambazo Yesu alitaja, msamaha hautolewi katika hatua ya kwanza, ya pili au ya tatu mpaka mkosaji atubu. Asipotubu baada ya kila hatua, anapelekwa hatua inayofuata, akiwa bado anahesabiwa kama mkosaji asiyetubu. Tunaambiwa kwamba “akikusikia” (yaani, akitubu), ndipo “umempata nduguyo” (yaani, mmepatanishwa tena).
Kusudi la kukabiliana na mtu ni ili msamaha utolewe. Ila, msamaha unategemeana na toba ya mkosaji. Basi, (1) tunamkabili mtu kwa matumini kwamba kama mkosaji, yeye ata (2) tubu ili sisi tuweze (3) kumsamehe.
Pamoja na hayo yote, tunaweza kusema kwa hakika kwamba Mungu hatutazamii sisi kuwasamehe waamini wenzetu kirahisi tu ambao wametukosea, na ambao hawana toba, hata baada ya kukabiliwa. Lakini pia, hii haitupi sisi haki ya kumchukia mwamini aliyekosea. Kinyume ni kwmaba tunamkabili kwa sababu tunampenda mkosaji, na tungetaka kumsamehe na kupatanishwa naye.
Ila, baada ya kila juhudi kufanyika kufuata zile hatua tatu ambazo Yesu alitaja, hat ua ya nne inakomesha mahusiano yetu, kama tutatii maneno ya Kristo.[1] Kama ambavyo hatupaswi kushirikiana na wanaojiita Wakristo ambao ni wazinzi, walevi, walawiti na kadhalika (ona 1Wakor. 5:11), hatupaswi kushirikiana na wanaojiita Wakristo ambao wanakataa kutubu kulingana na makubaliano ya kusanyiko lote. Watu kama hao wanathibitisha kwamba si wafuasi wa kweli wa Kristo, nao wanaleta aibu kwa kanisa Lake.
Mfano Wa Mungu
Tunapoendelea kutafakari wajibu wetu wa kuwasamehe wengine, tunaweza pia kujiuliza hivi: Kwa nini Mungu atazamie sisi tufanye kitu ambacho Yeye Mwenyewe hafanyi? Hakika Mungu anawapenda wakosaji, na anawanyooshea mikono Yake ya rehema katika toleo la kuwasamehe. Anazuia hasira Yake na kuwapa muda wa kutubu. Lakini kusamehewa kwao hutegemeana na kutubu kwao. Mungu hasamehi wenye hatia wasipotubu kwanza. Basi, mbona sisi tudhanie kwamba ana matazamio makubwa zaidi kwetu?
Pamoja na hayo – hivi haiwezekani kwamba dhambi ya kutosamehe ambayo ni mbaya sana machoni pa Mungu ni ile dhambi ya kutowasamehe wale wanaotuomba msamaha? Mara tu baada ya Yesu kutaja zile hatua nne za kutoa adhabu kanisani, Petro aliuliza hivi:
Bwana! Ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? (Mathayo 18:21, 22).
Je, Petro alifikiri kwamba Yesu alikuwa anamtazamia kumsamehe ndugu asiyetubu mara mia nyingi kwa ajili ya dhambi mia nyingi, wakati Yesu alikuwa amemwambia tu muda mfupi uliopita kwamba amhesabu ndugu asiyetubu kama mtu wa Mataifa au mtoza ushuru kwa sababu ya dhambi moja tu? Haiwezi kuwa hivyo. Tunarudia tena: huwezi kumtenga mtu au kumhesabu asiyefaa kushirikiana naye kama umemsamehe.
Swali lingine la kutufanya tufikiri ni hili: Kama Yesu anatutazamia kumsamehe mwamini mara mia nyingi kwa sababu ya dhambi mia nyingi ambazo hatubu, ili kudumisha uhusiano wetu, mbona anaturuhusu kuvunja ndoa kwa sababu ya dhambi moja tu kinyume chetu – dhambi ya uasherati – kama mwenzetu katika ndoa hatatubu (ona Mathayo 5:32)?[2] Hili halionekani kuwa na mantiki.
Ufafanuzi Zaidi
Mara tu baada ya Yesu kumwambia Petro amsamehe ndugu mara mia arobaini na tisa, alisimulia mfano ili kumsaidia Petro aelewe maana yake.
Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. [Kiwango hicho ni sawa na mshahara wa zaidi ya miaka elfu tano kwa kibarua katika siku za Yesu.] Naye alipokosa cha kulipa, Bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa hule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake aliyemwia dinari mia [sawa na mshahara wa siku mia moja]. Akamkamata, akamshika koo akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka. Akaenda, akamtupa kifungoni hata atakapoilipa ile deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu! Nalikusamehe wewe deni ile yote uliponisihi. Nawe je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake (Mathayo 18:23-35).
Ona kwamba yule mtumwa wa kwanza alisamehewa kwa sababu alimwomba bwana wake msamaha. Kisha, ona kwamba yule wa pili naye alimwomba msamaha yule mtumwa wa kwanza kwa unyenyekevu sana. Yule wa kwanza hakumpa yule wa pili kile alichokuwa amepewa yeye, na hicho ndicho kilichomkasirisha sana bwana wake. Kama ni hivyo, kweli Petro angedhani kwamba Yesu anamtazamia amsamehe ndugu asiyetubu, ambaye hakuomba msamaha? Kitu hicho hakionekani katika mfano wa Yesu. Basi, haiwezekani, na zaidi sana, kwa sababu Yesu alikuwa amekwisha tangulia kumwambia jinsi ya kufanya na ndugu asiyetubu baada ya kukabiliwa ipasavyo – awe kwake kama mtu wa Mataifa, na mtoza ushuru.
Haiwezekani kwamba Petro alidhani alitazamia kumsamehe ndugu asiyetubu kwa sababu ya hukumu ambayo Yesu alituabudi kama ha tutawsamehe ndugu zetu kutoka mioyoni mwetu. Yesu aliahidi kurudisha deni lote tulilokuwa tumesamehewa kwanza, na kutukabidhi kwa watesaji mpaka tulipe kile tusichoweza kulipa. Je, hiyo ingekuwa ni adhabu halali kwa ndugu Mkristo asiyemsamehe ndugu, ndugu ambaye hata Mungu hatamsamehe? Kama ndugu akinikosea, anamkosea Mungu, na Mungu hatamsamehe mpaka atubu. Je, Mungu ataniadhibu mimi kwa haki kwa kutomsamehe mtu ambaye hata Yeye hamsamehi?
Ufupisho
Matarajio ya Yesu kwetu kumsamehe mwamini mwenzetu yanatajwa katika maneno Yake yanayopatikana katika Luka 17:3-4.
Jilindeni! Kama ndugu yako akikosa, mwonye. Akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe (Maneno mepesi kukazia).
Tunataka iwe wazi kuliko hivyo? Yesu anatutazamia kuwasamehe waamini wenzetu, wakati wanapotubu. TUnapoomba na kusema, “Utusamehe deni zetu kama nasi tunavyowasamehe wadeni wetu” tunamwomba Mungu atutendee kama ambavyo na sisi tumewatendea wengine. Hatutazamii Yeye atusamehe kama hatutaomba. Basi, mbona sisi tudhani kwamba anatutazamia kuwasamehe wale wasio-omba?
Hapo tena, hayo yote hayatupi sisi kibali cha kuwa na chuki kinyume cha ndugu au dada katika Kristo aliyetukosea. Tunaagizwa kupendana. Hiyo ndiyo sababu tunaagizwa kumkabili mwamini anayetenda dhambi kinyume chetu, ili kuwepo na upatanisho kati yetu, na ili naye aweze kupatanishwa na Mungu, ambaye anakuwa amemkosea pia. Upendo ungefanya hivyo. Lakini mara nyingi, Wakristo watasema wamemsamehe mwamini mwanzao aliyekosea, lakini utagundua kwamba ni njia tu ya kuepuka kukabiliana naye. Ukweli ni kwamba hawasamehi, na inaonekana kwa matendo yao. Wanamkwepa mkosaji kwa gharama yoyote, na mara nyingi wanasema jinsi walivyoumizwa. Hakuna upatanisho hapo.
Tunapofanya dhambi, Mungu hutukabili kwa Roho Wake Mtakatifu ndani yetu kwa sababu anatupenda na anataka kutusamehe. Tunapaswa kumwiga Yeye, tukiwakabili kwa upendo waamini wenzetu wanaotenda dhambi kinyume chetu ili kuwepo toba, msamaha na kupatana.
Mungu kila mara amewatazamia watu Wake kupendana kwa upendo wa kweli – upendo unaoruhusu kukemea, lakini usioruhusu kuwa na kinyongo. Katika Torati ya Musa utakuta sheria ifuatayo:
Usimchukie ndugu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake. Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako, bali umpende jirani yako kama nafsi yako. Mimi ndimi BWANA (Walawi 19:17, 18. Maneno mepesi kukazia).
Pingamizi
Lakini – vipi kuhusu maneno ya Yesu katika Marko 11:25, 26? Je, hayaonyeshi kwamba lazima tuwasamehe wote kwa kila kitu, bila kujali kwamba ameomba msamaha au hapana?
Nanyi kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu, ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. [Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.]
Huu mstari mmoja haukanushi mistari ile mingine yote ambayo tumemkwisha tazama kuhusu mada hii. Tunajua tayari kwamba, kilicho kibaya zaidi sana kwa Mungu ni sisi kukataa kumsamehe mtu anayetuomba msamaha. Basi, tunaweza kutafsiri mstari huu kulingana na kweli hiyo thabiti. Yesu hapa anatilia mkazo tu kwmaba lazima tuwasamehe wengine kama tunataka msamaha wa Mungu. Hatuambii utaratibu ili tusamehewe, na kitu ambacho mtu anapaswa kufanya ili kuupokea kutoka kwa mwingine.
Ona pia kwamba Yesu hasemi hapa kwamba lazima tumwombe Mungu msamaha ili tuweze kuupokea kutoka kwake. Kama ni hivyo, ina maana tupuuze kila kitu kingine ambacho Maandiko yanafundisha juu ya msamaha wa Mungu kutegemea sisi kumwomba (ona Mathayo 6:12; 1Yohana 1:9)? Je, tudhanie tu kwamba hatuhitaji kuomba Mungu atusamehe tunapotend adhambi kwa sababu Yesu hasemi hilo hapa? Hapo ni kutokuwa na busara, kulingana na tunachojifunza katika Maandiko. Pia, si busara kupuuza kila kitu kingine ambacho Maandiko yanafundisha kuhusu sisi kuwsamehe wengine kuwa kumejengwa juu ya wao kuomba msamaha.
Pingamizi Nyingine
Je, Yesu hakuwaombea wale askari waliokuwa wanagawana mavazi yao kwamba, “Baba! Uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo” (ktk Luka 23:34)? Je, hiyo haionyeshi kwamba Mungu huwasamehe watu bila wao kumwomba?
Ndiyo, kwa kiwango fulani tu. Inaonyesha kwamba Mungu huwahurumia watu wasiojua – ni kiwango fulani cha msamaha. Kwa kuwa Mungu ni mwenye haki kabisa, anawawajibisha watu wakati wanapojua kwamba wanatenda dhambi.
Sala ya Yesu kwa ajili ya wale askari haikuwahakikishia kuingia mbinguni. Iliwalinda tu wasiwajibishwe kwa ajili ya kugawana mavazi ya Mwana wa Mungu, na ni kwa sababu wao hawakumjua Yeye ni nani. Walimhesabu kuwa ni mhalifu mwingine tu anayestahili kuuawa. Basi, Mungu aliwahurumia kwa tendo ambalo lingestahili hukumu ya hakika, kama wangejua walichokuwa wanafanya.
Vivyo hivyo, sisi tunapaswa kuwaonea huruma watu wasiojua kile walichotutendea, kama wale askari wasioamini na wasiojua, waliogawana mavazi ya Yesu. Yesu anatutazamia kuwaonyesha wasioamini rehema ya ajabu sana, na kuwapenda adui zetu, na kuwatendea mema wale wanaotuchukia, na kuwabariki wale wanaotulaani na kuwaombea wale wanaotutendea mabaya (ona Luka 6:27, 28). Tunapaswa kujaribu kuyeyusha chuki yao kwa upendo wetu, na kushinda ubaya kwa wema. Jambo hili lilielezwa hata katika Torati ya Musa, kama ifuatavyo:
Ukimwona ng’ombe wa adui wako au punda wake amepotea, sharti umrudishie mwenyewe tena. Ukimwona punda wake huyu akuchukiaye hali ameanguka chini yamzigo wake, nawe untejizuia usimsaidie, lazima umsaidie (Kutoka 23:4, 5).
Adui yako akiwa ana njaa, mpe chakula. Tena akiwa ana kiu, mpe maji ya kunywa. Maana utatia makaa ya moto kichwani pake; na BWANA atakupa thawabu (Mithali 25:21, 22).
Inashangaza kwamba, ingawa Yesu alituamuru tuwapende adui zetu, tuwatendee mema wanaotuchukia, tuwabariki wanaotulaani, na tuwaombee wanaotuonea (ona Luka 6:27, 28), hakutuambia tuwasamehe. Tunaweza kuwapenda watu bila kuwasamehe – sawa tu na ambavyo Mungu anawapenda watu bila kuwasamehe. Si tu kwamba tunaweza kuwapenda, tunapaswa kuwapenda, maana ni amri ya Mungu kwamba tufanye hivyo. Na upendo wetu kwao unapaswa kuonekana kwa matendo yetu.
Kwa kuwa Yesu alimwomba Baba Yake awasamehe wale askari waliokuwa wanagawana nguo zake, si uthibitisho kwamba tunapaswa kupuzia kila kitu kingine tulichojifunza kutoka Maandiko kwa habari ya mada hii, na kumsamehe kila mtu aliyetukosea. Tunachojifunza hapo ni kwamba tunapaswa kuwasamehe bila kusita wale wasiojua dhambi yao dhidi yetu, na kuonyesha rehema na huruma ya ajabu sana kwa wasioamini.
Kutenda Mathayo 18:15-17
Ingawa zile hatua nne za upatanisho zilizotajwa na Yesu ni rahisi kueleweka, zinaweza kuwa ngumu kutekeleza. Wakati Yesu alipozitaja hizo hatua nne, alifanya hivyo kutokana na mtazamo wa ndugu A kuwamini – sawasawa kabisa – kwamba ndugu B amemkosea. Ila, kihalisi, Ndugu A anaweza kuwa amekosea. Hebu basi tubuni hali ambayo kila uwezekano unatazamwa.
Kama ndugu A anaamini kwamba ndugu B amemkosea, anatakiwa kwanza ahakikishe kwamba haingii kwenye kulaumu sana, akitafuta kibanzi katika jicho la ndugu B. Makosa mengine madogo yanapaswa kupuuzwa tu na huruma kuonyeshwa (ona Mathayo 7:3-5). Ila, kama ndugu A akijisikia kuudhika na ndugu B kwa sababu ya kosa kubwa la maana, basi amkabili.
Anapaswa kufanya hivyo kibinafsi, akitii agizo la Yesu, na kuonyesha upendo wake kwa ndugu B. Kusudi lake liwe upendo na lengo lake upatanisho. Hapaswi kumwambia mtu mwingine yeyote juu ya kosa hilo. “Upendo husitiri wingi wa dhambi” (1Petro 4:8). Tukimpenda mtu hatufunui dhambi zake; tunazisitiri.
Sasa – anapomkabili mwenzake, awe mpole, akionyesha pendo lake. Atumie maneno kama haya: “Ndugu B. Kweli nathamini sana uhusiano wetu. Lakini kuna kitu kimetokea ambacho kimejenga ukuta moyoni mwangu juu yako. Sitaki ukuta huo uwepo, na ndiyo maana nimeona ni vizuri nikwambia kwamba umenikosea, ili tuone tutafanyaje kupatana. Na kama mimi nimefanya chochote kilichochangia tatizo hilo kuwepo, naomba uniambie.” Kisha, amwambie ndugu B kwa upole kabisa kosa ni nini.
Mara nyingi utakuta kwamba ndugu B wala hakujua kwamba aalimkosea ndugu A, na mara baada ya kufahamu kwamba amemkosea, atamwomba msamaha. Kama itakuwa hivyo, ndugu A anapaswa kumsamehe ndugu B hapo hapo. Upatanisho umetokea.
Mfano mwingine ni kwamba ndugu B anaweza kujaribu kutetea dhambi yake dhidi ya ndugu A kwa kumwambia kwamba yeye alikuwa anaitikia kosa lililokuwa limekwisha tendwa na ndugu A. kama ni hivyo, ndugu B alitakiwa kuwa amekwisha mkabili ndugu A. Pamoja na hayo, tayari kuna mazungumzo na matumaini hapo ya kupatana.
Katika hali kama hiyo, wahusika wanapaswa kuzungumza yaliyotokea, wakubali makosa kila mmoja kulingana na hali halisi, kisha wapeane na kupokea msamaha kila mmoja toka kwa mwenzake. Tayari wamekwisha patana.
Mfano wa tatu ni A na B wameshindwa kupatana. Hapo wanahitaji msaada, na ni wakati wa kupiga hatua ya pili.
Hatua ya Pili
Itakuwa vizuri ndugu A na B wakubaliane juu ya nani aongezeke ili kuwasaidia kupatana. Inafaa ndugu C na D wawe wanaowajua na kuwapenda ndugu A na B, maana hiyo itahakikisha kwamba hakuna upendeleo. Tena, ndugu C na D waambiwe juu ya kutoelewana huko kwa sababu ya ndugu A na B kupendwa na kuheshimiwa tu.
Kama ndugu B hatatoa ushirikiano hapa, ni juu ya ndugu A kutafuta mtu mmoja au wawili wanaoweza kusaidia.
Kama ndugu C na D wana busara, hawatatoa uamuzi mpaka wasikie kutoka kwa A na B. Baada ya ndugu C na D kutoa uamuzi wao, A na B wanapaswa kukubaliana na uamuzi wao na kuomba msamaha na kufanya chochote kitakachopendekezwa kwa mmoja wao, au kwa wote.
Ndugu C na D hawapaswi kujionyesha kwamba hawapendelei upande wowote na kwamba hawataki kujihusisha kwa kutoa ushauri kwamba ndugu A na B wote wanahitaji kutubu, huku ni mmoja tu anayehitaji kutubu. Wanapaswa kujua kwamba kama ndugu A au B watakataa uamuzi wao, mambo yatafika mbele ya kanisa lote, na uamuzi wao wa uoga utadhihirika kwa kila mtu. Hili jaribu linalowakabili ndugu C na D kutaka kutunza urafiki na ndugu A na B kwa kukataa kusimamia ukweli ni sababu nzuri ya waamuzi wawili kuwa bora kuliko mmoja, maana watatiana nguvu katika ukweli. Tena, uamuzi wao utakuwa na uzito zaidi kwa ndugu A na B.
Hatua Ya Tatu
Ikiwa yeyote kati ya ndugu A na B atakataa uamuzi wa ndugu C na D, jambo hilo lifikishwe mbele ya kanisa zima. Hii hatua ya tatu haifanywi katika makanisa jengo – na ni kwa sababu nzuri tu – maana ingesababisha kanisa kugawanyika kutokana na watu kujiunga upande mmoja au mwingine. Yesu hakukusudia makanisa yawe makubwa kuliko nyumba za watu. Katika kusanyiko dogo kama familia ambapo kila mmoja anajua na kujali juu ya ndugu A na B ndipo hatua ya tatu inapokusudiwa. Katika kanisa kubwa lenye watu wengi, hatua ya tatu inatakiwa kuchukuliwa katika kundi dogo la watu wanaowajua ndugu A na B na kuwapenda. Kama ndugu A na B ni washirika wa makundi tofauti, basi kiasi fulani cha washirika wanaofaa kutoka makundi yote mawili wahusike kama baraza litakalofanya maamuzi.
Baada ya kanisa kutoa uamuzi wake, ndugu A na B wanapaswa kuukubali, wakijua matokeo ya kukataa. Samahani zitolewe, misamaha itolewe na upatanisho ufanywe.
Kama ndugu A au B atakataa kufanya inavyotakiwa, atengwe na kanisa, na mtu yeyote katika kanisa asishirikiane naye tena. Mara nyingi ikifikia hapo, mtu asiyetubu anakuwa amekwisha jiondoa mwenyewe kwa hiari yake, na labda anakuwa amefanya hivyo muda mrefu tu kabla, ikitokea kwamba hakupata alichotaka katika hatua yoyote. Hii huonyesha kutokuwa tayari kwake kujitoa kwa dhati kuipenda familia yake ya kiroho.
Tatizo La Kawaida
Katika makanisa makubwa, mara nyingi watu hutatua matatizo yao kwa kuhama kutoka kanisa moja hadi lingine – mahali ambapo mchungaji, anayetaka kujenga ufalme wake kwa gharama yoyote, na ambaye hana mahusiano halisi na wachungaji wengine, huwakaribisha watu kama hao na kuungana nao wanapomweleza hadithi zao za kusikitisha. Jambo hili huua kabisa nguvu za hatua za Yesu kuhusu upatanisho. Na kwa kawaida, baada ya miezi michache tu au miaka, yule mtu aliyekosewa ambaye hukaribishwa katika makanisa ya wachungaji aina hiyo, anahama tena, kwenda kutafuta kanisa lingine, maana huku nako amekosewa.
Yesu alitazamia kwamba makanisa yangekuwa madogo kiasi cha kutosha katika nyumba, na kwamba wachungaji wa mahali/wazee/waangalizi wangekuwa wanafanya kazi pamoja kwa ushirika katika mwili mmoja. Hivyo, kutengwa kwa mshirika mmoja katika kanisa moja kungekuwa ni kutengwa kwake katika makanisa yote. Ni wajibu wa kila mchungaji/mzee/mwangalizi kuwaomba Wakristo wote wahamiaji habari kuhusu makanisa waliyotoka, kisha kuwasiliana na uongozi wa makanisa hayo ili kuamua kama watu aina hiyo wakaribishwe au hapana.
Kusudi La Mungu – Kuwa Na Kanisa Takatifu
Tatizo lingine la kawaida la makanisa jengo ni kwamba washirika wao wengi ni watu wanaohudhuria tu kwa ajili ya mambo yanayofanywa hapo. Hawataki sana kuwajibika kwa yeyote kwa sababu mahusiano yao ni ya kijamii san asana. Basi, hakuna yeyote – hata wachungaji – anayejua jinsi wanavyoishi maisha yao – na watu wasiokuwa wataka tifu wanaendelea kuleta doa kwa makanisa wanayohudhuria. Watu wa nje huwapima watu wanaowaona kuwa Wakristo kuwa si tofauti na wasioamini kwa lolote.
Hili peke yake inapaswa kuwa uthibitisho wa kutosha kwa yeyote kwamba, mfumo wa makanisa kama shirika si kusudi la Mungu kwa ajili ya kanisa Lake takatifu. Watu wasiokuwa watakatifu na wanafiki hujificha daima katika makanisa makubwa, wakisababisha jina la Kristo kutukanwa. Lakini, kutokana na tuliyosoma katika Mathayo 18:15-17, Yesu alikusudia kanisa Lake kuwa lenye watu watakatifu, viungo waliojitolea kabisa wa mwili wenye kujitakasa. Dunia ingetazama kanisa na kumwona bibi arusi wa Kristo akiwa safi. Lakini siku hizi, tunaona kahaba mkuu, mke asiyekuwa mwaminifu kwa Mume wake.
Hii hali ya kujisafisha iliyokusudiwa na Mungu kwa ajili ya kanisa inaonyeshwa wazi wakati Paulo anaposhughulika na swala fulani zito katika kanisa la Korintho. Mshirika aliyekubaliwa katika kanisa hilo alikuwa anaishi na mke wa baba yake katika mahusiano ya uzinzi.
Habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo. Kwa maana kweli nisipokuwako kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu. … Naliwaandikia katika waka wangu kwamba msichangamane na wazinzi. Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii, au na wenye kutamani, au na wanyang’anyi, au na wenye kuabudu sanamu; maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia. Lakini mambo yalivyo, naliwaandikia kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. Maana yanihusu nini kuwahukumu wale walio nje? Ninyi hamwahukumu hao walio ndani? Lakini hao walio nje Mungu atawahukumu. Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu (1Wakor. 5:1-5; 9-13).
Hapakuwepo na haja ya kumpitisha mtu huyu katika zile hatua za upatanisho kwa sababu hakuwa mwamini wa kweli. Paulo anamwita “mtu aitwaye ndugu”, na “mbaya yule”. Halafu katika mistari michache baadaye aliandika hivi:
Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi (1Wakor. 6:9-10).
Ni wazi kwamba Paulo aliamini – na ni sahihi kabisa – kwamba wale wasiokuwa safi, kama yule mtu katika kanisa la Korintho, huonyesha jinsi wasivyokuwa watu wa imani. Watu kama hao wasitendewe kama ndugu na kupitishwa katika zile hatua nne za kupatanishwa. Wanapaswa kutengwa, “kukabidhiwa kwa Shetani,” ili kanisa lisije likakuza kujidanganya kwao, na wawe na tumaini la kuona haja yao ya kutubu ili kuweza “kuokolewa katika siku ya Bwana Yesu” (1Wakor. 5:5).
Katika makanisa makubwa duniani siku hizi, utakuwa watu mia kadhaa wanaojifanya kuwa Wakristo ambao, kwa viwango vya Manadiko si waamini, na wanapaswa kutengwa. Maandiko yanatuonyesha wazi wazi kabisa kwamba kanis alina wajibu wa kuwaondoa miongoni mwake wale ambao ni waasherati, wazinzi, walawiti, walevi na kadhalika. Lakini watu kama hao, chini ya bendera ya “neema” siku hizi wanakumbatia kwamba ni “waamini wanaojikongoja”, na kuwekwa katika makundi ya usaidizi, ambamo wanaweza kutiwa moyo na “waamini” wenzao wenye matatizo kama hayo. Hili ni tusi na kejeli kwa uwezo wa Injili ya Yesu Kristo, inayobadilisha maisha.
Viongozi Walioanguka
Mwisho: Je, kiongozi aliyetubu arudishwe mara moja kwenye nafasi yake, kama alikuwa katika dhambi kubwa sana (kama uasherati)? Ingawa Bwana atamsamehe mara moja huyo kiongozi mwenye kutubu (na kanisa linapaswa kufanya vivyo hivyo), kiongozi huyo anakuwa amekwisha poteza imani kwa wale anaowahudumia. Kuaminika ni kitu ambacho lazima kukifanyia kazi. Basi, viongozi walioanguka wajiondoe wenyewe kwenye nafasi zao za uongozi na kukaa chini ya uangalizi kiroho mpaka wathibitishe kuaminika kwao. Lazima waanze tena. Wale ambao hawako tayari kujinyenyekeza na kufanya shughuli ndogo ndogo ili kuweza kuaminika tena, wasikubalike kama viongozi na mtu yeyote katika kusanyiko.
Hitimisho
Kama watumishi wanaofanya wengine kuwa wanafunzi, walioitwa “kukaripia, kukemea na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho” (2Timo. 4:2), hebu tusiogope kutekeleza wito wetu. Hebu tufundishe wanafunzi wetu kupendana kweli kweli kwa kuvumiliana na kuchukuliana kwa huruma siku zote, kwa kukabiliana kwa upole ikibidi, na kukabiliana zaidi kwa msaada wa wengine inapobidi, na kwa kusamehe kila inapohitajika. Hivi ni vizuri zaidi kuliko msamaha wa uongo ambao hauleti uponyaji wa kweli katika mahusiano yaliyoharibika. Tena, tujitahidi sana kumtii Bwana katika kila eneo, ili kutunza kanisa Lake katika hali ya usafi na ut akatifu, ili liwe sifa kwa jina Lake!
Ukitaka kujifunza zaidi kuhusu makabiliano na nidhamu kanisani, soma maandiko yafuatayo: Warumi 16:17, 18; 2Wakor. 13:1-3; Wagalatia 2:11-14; 2Wathes. 3:6, 14, 15; 1Timo. 1:19, 20; 5:19, 20; Tito 3:10, 11; Yakobo 5:19, 20; 2Yohana ms. 10 na 11.
[1] Ni halali kusema kwamba, kama yule aliyetengwa atatubu baadaye, Yesu anatazamia msamaha utolewe kwake.
[2] Kama mwenzi mwasherati ni Mkristo, tunapaswa kumpitisha katika zile hatua tatu ambazo Yesu alizitoa kwa ajili ya upatanisho, kabla ya kufikia kwenye kuachana. Huyo mwenzi akitubu, tunatazamiwa kusamehe, kulingana na agizo la Yesu.