Kwa nini Mungu alituumba? Je, amekuwa na lengo fulani katika akili Zake tangu mwanzo? Je, hakujua kwamba kila mtu angemwasi? Je, hakuona matokeo ya uasi wetu – mateso yote na huzuni ambavyo vimewapata binadamu tokea hapo? Kama ndivyo, alimwumba mwanadamu wa nini basi?
Biblia inatujibu maswali hayo. Inatuambia kwamba, kabla ya Mungu kumwumba Adamu na Hawa alijua kwamba wao na wengine baada yao wangetenda dhambi. Cha ajabu ni kwamba alikwisha panga mpango wa kuwakomboa binadamu walioanguka, kwa njia ya Yesu. Paulo ameandika hivi kuhusu huo mpango wa Mungu kabla ya uumbaji wa vyote:
Kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele (2Timo. 1:8b, 9. Maneno mepesi kukazia).
Sisi tulipewa neema ya Mungu katika Kristo tangu milele, sio kwa milele tu. Hiyo inaonyesha kwamba kifo cha Yesu cha kujitoa sadaka ni kitua mbacho Mungu alipanga tokea milele iliyopita.
Pia, Paulo ameandika hivi katika barua yake kwa Waefeso:
Kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu (Waefeso 3:11. Maneno mepesi kukazia).
Kifo cha Yesu msalabani hakikuwa wazo la haraka au mpango ulioandaliwa upesi-upesi ili kutengeneza kitu ambacho Mungu hakuwa amekiona.
Si kwamba Mungu alikuwa na kusudi la milele kutupa sisi neema Yake tangu milele, bali pia alifahamu tangu milele iliyopita, nani wangechagua kupokea neema Yake, naye akaandika hata majina yao katika kitabu.
Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo [Yesu], aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia (Ufunuo 13:8. Maneno mepesi kukazia).
Anguko la Adamu halikumshtua Mungu. Hata wewe unapoanguka au mimi ninapoanguka, Mungu hashangazwi. Mungu alijua tutatenda dhambi, naye pia alijua atakayetubu na kumwamini Bwana Yesu.
Swali Linalofuata
Ikiwa Mungu alijua kwamba wengine wangemwamini Yesu na wengine wangemkataa, kwa nini aliumba watu ambao alijua wangemkataa? Mbona asirahisishe tu mambo kwa kuwaumba wale aliojua kwamba watatubu na kumwamini Yesu?
Jibu la swali hilo ni gumu kidogo kuelewa, lakini linaweza kueleweka.
Cha kwanza tunachopaswa kuelewa ni kwamba Mungu alituumba tukiwa na hiari. Yaani, sisi sote tuna fursa ya kujiamulia wenyewe ikiwa tutamfuata Mungu au hapana. Maamuzi yetu ya kutii au kutotii, kutubu au kutotubu, Mungu hajatupangia. Ni uchaguzi wetu wenyewe.
Kwa kuwa ni hivyo, lazima wote tupimwe. Ni kweli kwamba Mungu alijua tutakachofanya kabla hatujakifanya, lakini ilitubidi sisi tufanye kitu hicho wakati fulani ili Yeye akijue kabla.
Tutazame mfano. Mungu anajua matokeo ya kila mchezo wa mpira kabla haujachezwa, lakini lazima kuwe na michezo ya mpira na matokeo yake kama Mungu atajua. Ni kwamba Mungu hawezi kujua kabla matokeo ya michezo ya mpira ambayo haichezwi kwa sababu hakuna matokeo ya kujulikana.
Vivyo hivyo, Mungu anaweza kujua kabla matokeo ya watu wenye hiari, kama hao watu watapewa nafasi ya kufanya maamuzi hayo, na kuyafanya. Lazima wapimwe. Na hiyo ndiyo sababu Mungu hakuumba watu ambao Yeye alijua kabla kwamba watatubu na kumwamini Yesu peke yao.
Swali Lingine
Tunaweza pia kuuliza hivi: “Kama Mungu wanataka watu watiifu tu, kwa nini alituumba tukiwa na hiari? Mbona hakuumba mashine za robot ambazo ni tiifu zinazoishi milele?”
Jibu ni hili: Ni kwa sababu Mungu ni Baba. Anataka kuwa na uhusiano wa baba na mtoto pamoja nasi, na haiwezekani ukawepo kama tutakuwa mashine. Shauku ya Mungu ni kuwa na familia ya milele ya watoto ambao wamechagua, kwa hiari yao wenyewe, kumpenda. Huo ndiyo uliokuwa mpango Wake kulingana na Maandiko.
Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake (Waefeso 1:4b, 5. Maneno mepesi kukazia).
Ukitaka kujua raha ambayo Mungu angepata kutoka kwa mashine za robot, hebu chukua mwanasesere mkononi, umwambie akwambie kwamba anakupenda! Ukweli ni kwamba hutasikia raha moyoni mwako! Maana, huyo mwanasesere atakwambia kile unachomfanya aseme. Hakupendi kwa kweli.
Kinachofanya upendo kuwa maalum sana ni kwa sababu umejengwa kwenye uchaguzi wa mtu mwenye hiari. Wanasesere na mashine za robot hawajui chochote kuhusu upendo kwa sababu hawawezi kuamua chochote wao wenyewe.
Kwa kuwa Mungu alitaka familia ya watoto ambao wangechagua kumpenda na kumfuata kutoka mioyoni mwao, ilibidi aumbe watu wenye hiari. Uamuzi huo ulihusisha Yeye kukubali kwamba kuna uwezekano wa baadhi ya hao watu wenye hiari kuamua hawatampenda au kumfuata. Na hao, baada ya kuishi maisha ya kumpinga Mungu anayejidhihirisha na kuwavuta watu wote kwa njia ya uumbaji Wake, na dhamiri zao na wito wa Injili, wangekabiliwa na hukumu yao halali kabisa, baada ya kujithibitisha kwamba wanastahili hasira ya Mungu.
Hakuna mtu kuzimu atakayeweza kumnyooshea Mungu kidole cha lawama kwa haki, kwa sababu Mungu alitoa njia ya kila mtu kuepukana na adhabu ya dhambi zake. Mungu anataka kila mtu aokolewe (ona 1Timo. 2:4; 2Petro 3:9) lakini kila mtu lazima ajiamulie mwenyewe.
Kuchaguliwa Kabla KiBiblia
Lakini, vipi kuhusu maandiko katika Agano Jipya yanayosema kwamba Mungu alituchagua sisi kabla ya kuwekwa misingi ya dunia?
Kwa bahati mbaya, kuna wengine wanaodhani kwamba Mungu amewachagua watu fulani kuokoka, na wengine kulaaniwa, na msingi wa kuamua Kwake si chochote ambacho watu hao wamefanya. Yaani, Mungu amekwisha chagua wale watakao-okoka au kupotea. Wazo hili linaondoa dhana ya hiari ya mtu, na wala halifundishwi na Maandiko. Hebu tutazame Biblia inafundisha nini kuhusu kuchaguliwa kabla.
Ni kweli Biblia inafundisha kwamba Mungu ametuchagua, lakini lazima kutolewa maelezo. Tangu dunia ilipowekwa misingi, Mungu amechagua kuwakomboa watu ambao aliwajua kabla kwamba wangetubu na kuiamini Injili kutokana na ushawishi Wake, lakini kwa hiari yao wewenyewe. Hebu angalia maneno ya mtume Paulo kuhusu watu ambao Mungu huwachagua.
Mungu hakuwasukumia mbali watu wake waliowajua tokea awali. Au hamjui yale yaliyonenwa na maandiko juu ya Eliya? Jinsi anavyowashitaki Waisraeli mbele za Mungu, ‘Bwana! Wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami nimesalia peke yangu, nao wananitafuta roho yangu. Lakini ile jawabu ya Mungu yamwambiaje? ‘Nimejisazia watu elfu saba wasiopiga goti mbele ya Baali’. Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema (Warumi 11:2-5. Maneno mepesi kukazia).
Ona kwamba Mungu alimwambia Eliya “amejisazia watu elfu saba,” lakini hao watu elfu saba kwanza walikuwa wamekwisha fanya uchaguzi “kutompigia Baali goti”. Paulo akasema, vivyo hivyo, walikuwepo pia mabaki ya Wayahudi waaminio waliochaguliwa na Mungu. Basi, tunaweza kusema hivi: Ndiyo, Mungu ametuchagua, lakini amewachagua wale ambao kwanza wamefanya uchaguzi sahihi wao wenyewe. Mungu amechagua kuwaokoa wote wenye kumwamini Yesu, na huo ulikuwa mpango Wake hata kabla ya kuumba dunia.
Mungu Kujua Mambo Kabla
Kwa hali hiyo hiyo, Maandiko pia yanafundisha kwamba Mungu aliwajua kabla wale wote ambao wangechagua kufanya uchaguzi sahihi. Kwa mfano: Petro aliandika hivi:
Wakaao hali ya ugeni … kama vile Mungu Baba alivyotangulia kuwajua (1Petro 1:1-2a. Maneno mepesi kukazia).
Tumechaguliwa kulingana na uwezo wa Mungu kujua mambo kabla. Hata Paulo naye aliandika kuhusu waamini waliojulikana na Mungu kabla.
Maana wale aliowajua tangu asili [sisi], aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye [Yesu] awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza (Warumi 8:29-30).
Mungu alitujua kabla sisi sote ambao tungechagua kumwamini Yesu, Naye akatuchagua tufananishwe na mfano wa Mwna Wake, yaani, tuzaliwe na kuwa watoto wa Mungu katika familia Yake kubwa. Kulingana na mpango huo wa milele, alituita kwa njia ya Injili, akatuhesabia haki na hatimaye atatutukuza katika ufalme Wake wa milele.
Katika barua nyingine, Paulo aliandika hivi:
Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu yesu Kristo, aliyetubarikmi kwa baraka zote za rohoni katika ulimwengu wa roho ndani yake Kristo; kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo. Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake. Na usifiwe utukufu wa neema yake, ambayo ametuneemesha katika huyo Mpendwa (Waefeso 1:3-6. Maneno mepesi kukazia).
Kweli hiyo hiyo inatajwa hapa – Mungu alituchagua sisi (ambao alijua kabla kwamba tungetubu na kuamini) kabla ya misingi ya ulimwengu ili tuwe watoto Wake watakatifu kwa njia ya Yesu Kristo.
Kama tulivyokwisha sema, kuna wanaopotosha maana ya mistari kama hiyo kwa kupuuzia mengine yote yanayofundishwa na Biblia, na kudai kwamba sisi hatukuwa na uchaguzi wowote kwa habari ya wokovu wetu – Mungu ndiye mwenye neno la mwisho. Fundisho hili wanaliita “kuchaguliwa pasipo masharti”. Lakini, nani amewahi kusikia juu ya kitu cha aina hiyo – yaani, uchaguzi usiokuwa na masharti fulani? Katika nchi huru, tunachagua wagombea wanasiasa kulingana na wao kutosheleza masharti tuliyo nayo akilini mwetu. Tunawachagua wenzi kulingana na masharti watakayotimiza, sifa zao zinazowafanya wakubalike kwetu. Lakini wanatheolojia wengine wanataka tuamini kwamba uchaguzi wa Mungu kwamba nani aokoke na nani asiokoke “hauna masharti” – hautegemeani na masharti fulani ambayo hao watu wameyatimiza! Kwa hali hiyo, wokovu wa watu ni kwa bahati tu, ni atakavyoamua anayeitwa Mungu, ambaye ni mkatili, asiye na haki, mnafiki na asiyekuwa na akili – kwa mawazo yao! Neno lenyewe – “kuchaguliwa pasipo masharti” linapingana, maana uchaguzi unaonyesha masharti. Kama ni “kuchaguliwa pasipo masharti” hakuna uchaguzi hapo; huko ni kubahatisha.
Picha Kubwa
Sasa tunaiona picha yote kwa ukamilifu. Mungu alijua sisi sote tungetenda dhambi, lakini alifanya mpango wa kutukomboa kabla yeyote kati yetu hajazaliwa. Mpango huo ungedhihirisha upendo Wake wa ajabu sana na haki, maana ingebidi Mwana Wake asiye na dhambi afe kwa ajili ya dhambi zetu, kwa niaba yetu. Tena, Mungu hakutupangia sisi tutakaotubu na kuamini tu msamaha, bali pia kwamba tungekuwa kama Mwana Wake, Yesu. Ndiyo sababu Paulo akasema, “Si mimi ninayeishi, bali Kristo ndani yangu” (Wagal. 2:20).
Sisi ambao ni wana wa Mungu tuliozaliwa mara ya pili tutapewa miili isiyoharibika siku moja, nasi tutaishi katika jamii kamilifu, tukimtumikia, na kumpenda na kushirikianana Baba yetu wa ajabu wa mbinguni! Tutaishi katika dunia mpya, katika Yerusalemu Mpya. Hayo yote yatakuwa yamefanikiwa kwa sababu ya kifo chakujitolea sadaka cha Yesu! Mungu asifiwe kwa ajili ya mpango Wake wa milele!
Maisha Ya Sasa
Tukiisha kuelewa mpango wa Mungu wa milele, tunaweza kufahamu zaidi maana ya maisha haya. Kimsingi ni kwamba, maisha ya sasa ni kama kipimo au mtihani kwa ajili ya kila mtu. Uchaguzi wa kila mtu huamua kama atafurahia fursa ya pekee ya kuwa mtoto mmojawapo wa Mungu, atakayeishi pamoja na Baba milele. Wale wanaojinyenyekeza wenyewe, wanaokubaliana na mvuto wa Mungu, na kutubu na kuamini, watatukuzwa (ona Luka 18:14). Maisha haya ni kipimo kwa ajili ya maisha ya wakati ujao.
Hii pia hutusaidia kuelewa baadhi ya mambo ya siri katika maisha haya ya sasa. Kwa mfano: Wengi wamejiuliza hivi: “Kwa nini Shetani na mapepo yake wanaruhusiwa kuendelea kuwajaribu watu?” Au, “Wakati Shetani alipotupwa kutoka mbinguni, kwa nini aliruhusiwa kufika duniani?”
Twaweza kuona kwamba hata sasa Shetani anatimiza kusudi fulani katika mpango wa Mungu. Kimsingi, Shetani ndiyo kama uchaguzi mwingine kwa ajili yabinadamu. Kama uchaguzi pekee ungekuwa ni kumfuata Yesu, basi kila mtu angemfuata Yesu apende, asipende.
Ingekuwa sawa na kuwepo na uchaguzi ambao kila mtu anatakiwa kupiga kura, lakini mgombea ni mmoja tu. Huyo mgombea bila shaka angepita bila kupingwa, lakini asingekuwa na imani kwamba anapendwa na waliomchagua! Hawakuwa na uchaguzi – ilibidi wampigie kura! Mungu Naye angekuwa katika hali kama hiyo kama kusingekuwepo na yeyote anayeshindana Naye ili kupata mioyo ya watu.
Hebu tufikiri hivi: Ingekuwaje kama Mungu angewaweka Adamu na Hawa katika bustani ambayo hakuna kilichokatazwa? Ingekuwa hivi: Adamu na Hawa wangekuwa mashine za robot kutokana na mazingira. Wasingeweza kusema, “Tumeamua kumtii Mungu” kwa sababu wasingekuwa na nafasi ya kutokumtii.
Cha muhimu zaidi ni hiki: Mungu asingeweza kusema, “Ninajua Adamu na Hawa wananipenda” kwa sababu Adamu na Hawa wasingekuwa na nafasi ya kutii na kuthibitisha upendo wao kwa Mungu. Mungu lazima atoe nafasi ya kutotii kwa watu wenye hiari ili Yeye aamue kama wanataka kumtii. Mungu hamjaribu mtu (ona Yakobo 1:13), lakini humpima kila mtu (ona Zaburi 11:5; Mithali 17:3). Njia moja ya kuwapima ni kuwaruhusu wajaribiwe na Shetani, ambaye kwa njia hiyo anatekeleza kusudi maalum katika mpango wa Mungu wa milele.
Mfano Mzuri
Tunasoma hivi katika Kumbukumbu la Torati 13:1-3:-
Kukizuka katikati yako nabii au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu, ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, ‘Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo’; wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa BWANA, Mungu wenu, yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda BWANA, Mungu wenu, kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote (Maneno mepesi kukazia).
Inaonekana ni halali kabisa kuamua kwamba si Mungu aliyemwezesha huyo nabii wa uongo kufanya ishara au maajabu – bila shaka ni Shetani. Lakini Mungu anaruhusu na anatumia jaribu la Shetani kama kipimo Chake mwenyewe ili kugundua kilichomo ndani ya mioyo ya watu Wake.
Kanuni hiyo hiyo inaonekana katika Waamuzi 2:21 hadi 3:8 wakati Mungu aliporuhusu Israeli kujaribiwa na mataifa yaliyowazunguka ili kuamua ikiwa wangemtii au hapana. Yesu pia aliongozwa na Roho nyikani kwa kusudi la kujaribiwa na Shetani (ona Mathayo 4:1) na kwa njia hiyo kupimwa na Mungu. Ilibidi athibitishwe kwamba hana dhambi, na njia ya pekee ya kuthibitishwa kwamba hana dhambi ilikuwa kwa kujaribiwa.
Shetani Hastahili Lawama Zote
Tayari Shetani amedanganya watu wengi sana duniani kwa kupofusha mawazo yao kwa kweli ya Injili, lakini lazima tutambue kwamba Shetani hawezi kumpofusha mtu yeyote tu. Anaweza kuwadanganya wale watakaokubali kudanganywa, yaani, watu wanaokataa ukweli.
Paulo alitangaza kwamba wasioamini “wametiwa giza katika ufahamu wao” (Waefeso 4:18) na wale wasiojua, lakini pia amedhihirisha kiini cha ufahamu wao kutiwa giza, na kutokujua kwao.
Tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao, akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani (Waefeso 4:17b – 19. Maneno mepesi kukazia).
Watu ambao hawajaokoka si wenye bahati mbaya ambao wamedanganywa na Shetani. Ni wenye dhambi waasi ambao kwa makusudi, hawataki kujua, na ambao wanataka kudumu katika hali hiyo kwa sababu mioyo yao ni mgumu sana.
Hakuna mtu anayetakiwa kudumu katika kudanganywa, kama maisha yako wewe yanavyothibitisha! Ulipolainisha moyo wako na kumwelekea Mungu, Shetani hakuweza kuendelea kukudanganya.
Mwishoni, Shetani atafungwa katika kipindi cha utawala wa Kristo kwa miaka elfu moja, naye hatakuwa na ushawishi kwa mtu yeyote.
[Malaika] Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache (Ufunuo 20:2, 3).
Ona kwamba kabla ya kufungwa kwake, Shetani “alidaganya mataifa,” lakini atakapofungwa hataweza kuwadanganya tena. Ila, akifunguliwa, atawadanganya tena.
Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake; naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi … kuwakusanya kwa vita … Wakapanda juu ya upana wan chi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala (Ufunuo 20:7-9. Maneno mepesi kukazia).
Kwa nini Mungu amfungue Shetani kwa muda huo mfupi? Sababu ni kwamba wote wanaomchukia Kristo katika mioyo yao waliokuwa wanajifanya kumtii wakati wa utawala Wake, watadhihirika. Ndipo wataweza kuhukumiwa kihalali. Kitakuwa kipimo cha mwisho hicho.
Kwa sababu hiyo hiyo, Shetani anaruhusiwa kufanya kazi duniani wakati huu – ili wale wanaomchukia Kristo mioyoni mwao waweze kudhihirishwa na hatimaye kuhukumiwa. Mara tu Mungu atakapokuwa hana kazi na Shetani katika kutimiza makusudi Yake ya milele, huyo mdanganyaji atatupwa katika ziwa la moto ili ateswe huko milele (ona Ufunuo 20:10).
Kujiandaa Kwa Ajili Ya Ulimwengu Ujao
Kama umetubu na kuiamini Injili, umekwisha faulu mtihani – kipimo – wa msingi na muhimu sana katika maisha haya. Lakini, usifikiri kwamba hutaendelea kupimwa ili Mungu aweze kuendelea kuona uaminifu wako na msimamo wako unaoendelea. Ni wale tu watakao”dumu katika imani” ndiyo watakaosimama mbele za Mungu “watakatifu, na bila lawama” (Wakolosai 1:22, 23).
Zaidi ya hayo, Maandiko yanaonyesha wazi kwamba sisi sote siku moja tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu, na hapo tutapewa thawabu kibinafsi kulingana na utii wetu duniani. Basi, bado tunapimwa ili kujua kustahili kwetu kupokea thawabu maalum za baadaye katika ufalme wa Mungu. Paulo aliandika hivi:
Lakini wewe je! Mbona wamhukumu ndugu yako? Au wewe je! Mbona wamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, ‘Kama niishivyo, anena Bwana, kila goti litapigwa mbele zangu; na kila ulimi utamkiri Mungu.’ Basi ni hivyo, kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu (Warumi 14:10-12. Maneno mepesi kukazia).
Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya (2Wakor. 5:10).
Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu (1Wakor. 4:5. Maneno mepesi kukazia).
Thawabu Zitakuwa Nini?
Sasa – hizo thawabu zitakazotolewa kwa wale watakaothibitisha upendo wao kwa Yesu ni zipi?
Maandiko yanaonyesha aina mbili ya thawabu – kusifiwa na Mungu, na nafasi zaidi ya kumtumikia. Zote zinadhihirishwa katika mfano wa Yesu kuhusu kabaila mmoja.
Basi akasema, “Mtu mmoja, kabaila, alisafiri kwenda nchi ya mbali, ili ajipatie ufalme na kurudi. Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, ‘Fanyeni biashara hata nitakapokuja.’ Lakini watu wa mji wake walimchukia, wakatuma wajumbe kumfuata na kusema, ‘Hatumtai huyu atutawale.’ Ikawa aliporudi, ameupata ufalme wake, aliamuru waitwe wale watumwa aliowapa fedha, ili ajue faida aliyopata kila mtu kwa biashara yake. Akaja wa kwanza akasema, ‘Bwana! Fungu lako limeleta faida ya mafungu kumi zaidi.’ Akamwambia, ‘Vema, mtumwa mwema; kwa vile ulivyokuwa mwaminifu katika neno lililo dogo, uwe na mamlaka juu ya miji kumi.’ Akaja wa pili akasema, ‘Bwana! Fungu lako limeleta mafungu matano faida.’ Akamwambia huyu naye, ‘Wewe uwe juu ya miji mitano.’ Akaja mwingine akasema, ‘Bwana! Hili ndilo fungu lako, ambalo nililiweka akiba katika leso. Kwa maana nilikuogopa kwa kuwa u mtu mgumu; waondoa usichoweka, wavuna usichopanda.’ Akamwambia, ‘Nitakuhukumu kwa kinywa chako, mtumwa mwovu wewe. Ulinijua kuwa ni mtu mgumu, niondoaye nisichoweka na kuvuna nisichopanda. Basi, mbona hukuiweka fedha yangu kwa watoao riba, ili nijapo niipate pamoja na faida yake?’ Akawaambia waliosimama karibu, ‘Mnyang’anyeni hilo fungu, mkampe yule mwenye mafungu kumi.’ Wakamwambia, ‘Bwana! Anayo mafungu kumi.’ Nawaambia, ‘Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang’anywa hata alicho nacho. Tena wale adui zangu, wasiotaka niwatawale, waleteni hapa mwachinje mbele yangu’.” (Luka 19:12 – 27).
Bila shaka Yesu anawakilishwa na yule kabaila ambaye hakuwepo, na baadaye akarudi. Wakati Yesu atakaporudi, itabidi tutoe hesabu ya yale tuliyofanya na karama, uwezo, huduma na nafasi alizotupa Yeye, ambazo zinawakilishwa na fungu ambalo kila mtumwa alipewa katika mfano tuliosoma hapo juu. Kama tumekuwa waaminifu, tutapewa thawabu kwa kusifiwa Naye na kupewa mamlaka ya kumsaidia kutawala juu ya nchi (ona 2Timo. 2:12; Ufunuo 2:26, 27; 5:10; 20:6), kama ambavyo kila mtumishi mwaminifu alivyopewa kutawala miji katika mfano tuliosoma.
Jinsi Hukumu Yetu Ya Baadaye Itakavyokuwa Ya Haki
Mfano mwingine ambao Yesu alitoa unaonyesha haki kamilifu ya hukumu yetu ya baadaye.
Kwa maana ufalme wa mbinguni umefananana mtu mwenye nyumba aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; na hao nao akawaambia, ‘Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa.’ Wakaenda. Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama. Akawaambia, ‘Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi?’ Wakamwambia, ‘Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri.’ Akawaambia, ‘Enendeni nanyi katika shamba la mizabibu.’ Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, ‘Waite wakulima uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza.’ Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari. Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari. Basi wakiisha kuipokea, wakamnung’unikia mwenye nyumba wakisema, ‘Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa.’ Naye akamjibu mmoja wao akamwambia, ‘Rafiki! Sikudhulumu. Hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema?’ Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho (Mathayo 20:1-16).
Hapa, Yesu hakuwa anafundisha kwamba watumishi wote wa Mungu watapokea thawabu ile ile, maana hilo si haki, na pia lingekuwa kinyume cha maandiko mengine mengi (kwa mfano, Luka 19:12-27; 1Wakor. 3:8).
Hapa, Yesu alikuwa anafundisha kwamba kila mtumishi wa Mungu atapata thawabu, si kwa kutegemea alichofanya kwa ajili ya Yesu tu, bali pia kutegemeana na nafasi kiasi gani aliyopewa na Yesu. Watenda kazi kwa muda wa saa moja katika mfano wa Kristo wangefanya kazi kutwa nzima kama wangepewa nafasi ya mwenye shamba. Hivyo, wale waliotumia vizuri nafasi yao ya saa moja walipewa sawa na wale waliopewa nafasi ya kutwa nzima.
Basi – Mungu naye hutoa nafasi tofauti tofauti kwa kila mtumishi Wake. Kwa wengine anawapa nafasi kubwa sana za kutumikia na kubariki maelfu ya watu kwa kutumia karama za ajabu sana alizowapa. Kwa wengine, anatoa nafasi chache nak arama chache pia, lakini wao nao wanaweza kupokea thawabu ile ile mwishoni kama watakuwa waaminifu pia kwa kile ambacho Mungu amewapa.[1]
Hitimisho
Hakuna kitu chamaana kuliko kumtii Mungu, na siku moja kila mtu atajua hilo. Wenye hekima wanajua hilo sasa, na wanafanya kama inavyotakiwa!
Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri Zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya (Mhubiri 12:13, 14).
Mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi humtii Mungu kwa moyo wake wote, na anafanya kila anachoweza kuwahamasisha wanafunzi wake kufanya hivyo hivyo!
Ili kujifunza zaidi kuhusu mada hii muhimu ya hukumu yetu ya baadaye, ona maandiko yafuatayo: Mathayo 6:1-6, 16-18; 10:41, 42; 12:36, 37; 19:28, 29; 25:14-30; Luka 12:2, 3; 14:12-14; 16:10-13; 1Wakor. 3:5-15; 2Timo. 2:12; 1Petro 1:17; Ufunuo 2:26, 27; 5:10; 20:6.
[1] Vile vile huu mfano haufundishi kwamba wale wanaotubu wakiwa na umri mdogo na kuwa waaminifu kwa miaka mingi watapewa thawabu sawa na wale wanaotubu mwaka wa mwisho wa maisha yao na kumfuata Mungu kwa mwaka mmoja tu. Hiyo isingekuwa halali, na isingetegemea nafasi ambazo Mungu alimpa kila mmoja, maana Mungu alitoa kwa kila mmoja nafasi ya kutubu maishani mwao. Basi, wale wanaofanya kazi zaidi watapokea thawabu zaidi kuliko wale wanaofanya kazi kwa muda mfupi.