Ibrahimu alipothibitisha hiari yake ya kumtoa Isaka mwanawe mpendwa, Mungu alimpa ahadi.
Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umeitii sauti Yangu (Mwanzo 22:18).
Mtume Paulo anaonyesha kwamba hiyo ahadi ilitolewa kwa Ibrahimu na uzao wake mmoja, si wengi – na huyo mmoja ni Kristo (ona Wagalatia 3:16). Mataifa yote – au kila kabila duniani – wangebarikiwa katika Kristo. Ahadi hii kwa Ibrahimu ilitabiri kuingizwa kwa maelfu ya makabila duniani kote katika baraka ya kuwa ndani ya Kristo. Makabila hayo yanatofautiana kwa sababu yanatokea maeneo tofauti kijiografia, ni makabila tofauti, yanafuata mila na tamaduni tofauti, na yanasema lugha tofauti. Mungu anataka wote hao wabarikiwe ndani ya Kristo, ambayo ndiyo sababu ya Yesu kufa kwa ajili ya dhambi za dunia yote (ona 1Yohana 2:2).
Ingawa Kristo alisema njia ni nyembamba iendayo uzimani, na ni wachache waionao (ktk Mathayo 7:14), mtume Yohana ametupa sababu nzuri tu ya kuamini kwamba watakuwepo wawakilishi kutoka makabila yote ya duniani katika ufalme wa Mungu baadaye.
Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo (Ufunuo 7:9, 10. Maneno mepesi kukazia).
Basi, wana wa Mungu wanatazamia sana kukutanika katika kusanyiko la makabila mbalimbali mbele za kiti cha enzi siku moja!
Wataalamu wengi wa umisheni wametilia mkazo mkubwa kwenye kuyafikia makabila yaliyofichika duniani, kwa matumaini ya kuanzisha kanisa hai lenye nguvu katika kila moja. Kweli, hilo ni jambo la kusifiwa, maana Yesu alituambia twende duniani kote na “kuwafanya mataifa yote (au basi, makabila) kuwa wanafunzi” (Mathayo 28:19). Ila, mipango ya wanadamu – hata ikiwa na nia njema kiasi gani – kama haina uongozi wa Roho Mtakatifu, mara nyingi huharibu kuliko kutengeneza. Ni muhimu tufuate hekima ya Mungu tunapojaribu kujenga ufalme Wake. Yeye ametupa habari zaidi na maagizo kuhusu tunavyoweza kufanya wanafunzi duniani kote, zaidi ya ile ipatikanayo katika Mathayo 28:19.
Labda kinachopuuzwa sana na wale wanaojaribu kutimiza Agizo Kuu ni hiki: Mungu ndiye mwinjilisti mkuu katika wote, nasi tunatakiwa kuwa watenda kazi pamoja Naye, si kutenda kazi kwa ajili Yake. Yeye anajali zaidi sana kuhusu kuufikia ulimwengu na Injili kuliko mwingine yeyote, Naye anafanya kazi kuhakikisha hilo linatimia, kwa bidii kuliko mwingine yeyote. Yeye alishughulikia jambo hilo, na bado analishughulikia kwa bidii sana mpaka akafa kwa ajili yake! Alilishughulikia kabla hajaumba yeyote, na bado anafanya hivyo mpaka sasa. Huko ni kujitoa hasa!
“Kuufikia Ulimwengu Kwa Ajili Ya Kristo”
Ni kitu cha kushangaza kwamba, tunaposoma nyaraka za Agano Jipya, hatusomi sana himizo (kama ilivyo siku hizi) kwa waamini “kwenda na kuufikia ulimwengu kwa ajili ya Kristo”! Wakristo wa kwanza na viongozi wao walitambua kwamba Mungu alikuwa anafanya kazi kwa bidii sana kuukomboa ulimwengu, na kwamba kazi yao ilikuwa kushirikiana Naye kadiri alivyowaongoza. Kama kuna aliyejua hicho sana, mtume Paulo alikijua, ambaye “hakuletwa kwa Bwana” na mtu yeyote. Yeye aliokoka kwa tendo la moja kwa moja la Mungu, alipokuwa anasafiri kwenda Dameski. Na katika kitabuchote cha Matendo, tunaliona kanisa likikua kwa sababu watu waliojaa na kuongozwa na Roho, walishirikiana na Roho Mtakatifu. Kitabu cha Matendo, japo mara nyingi kinaitwa “Matendo ya Mitume” kinafaa kuitwa “Matendo ya Mungu.” Katika utangulizi wa Luka kwa Matendo, alitaja kwamba maelezo yake ya kwanza (yaani Injili yenye jina lake) yalikuwa taarifa ya “mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha” (Matendo 1:1. Maneno mepesi kukazia). Bila shaka Luka aliamini kwamba kitabu cha Matendo ni maelezo ya mambo ambayo Yesu aliendelea kufanya na kufundisha. Yeye alifanya kazi kupitia watu waliotiwa mafuta na kuongozwa na Roho, walioshirikiana Naye.
Kama Wakristo wa kwanza hawakutiwa moyo “kutoka na kwenda kuwashuhudia jirani zao ili ulimwengu umjie Kristo,” wajibu wao ulikuwa nini kwa habari ya kuujenga ufalme wa Mungu? Wale ambao hawakuwa na wito maalum na kupewa karama za kutangaza Injili hadharani (yaani, mitume na wainjilisti) waliitwa kuishi maisha matakatifu ya kumtii Mungu, na kuwa tayari kumjibu yeyote ambaye angewadhihaki au kuwauliza maswali. Kwa mfano: Petro aliandika hivi:
Lakini mjapoteswa kwa sababu ya haki mna heri. Msiogope kutisha kwao, wala msifadhaike; bali mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu. Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu. Nanyi mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo (1Petro 3:14-16).
Ona hapo kwamba Wakristo walioandikiwa na Petro walikuwa wanavumilia mateso. Ila, Wakristo wasipokuwa tofauti na dunia, dunia haiwezi kuwatesa. Hii ndiyo sababu moja kubwa ya kutokuwepo na mateso mengi ya Wakristo katika sehemu nyingi siku hizi – ni kwa sababu wanaojiita Wakristo hawana tofauti na wengine. Si Wakristo kwa kweli, hivyo, hakuna anayewatesa. Lakini, “Wakristo” aina hii wanahimizwa kila Jumapili “kuwashuhudia jirani zao habari ya imani yao.” Wanapowashuhudia jirani zao, hao jirani wanashangaa kujua kwamba wao ni Wakristo waliozaliwa mara ya pili. Kibaya zaidi ni kwamba, “injili” wanayowaambia jirani zao ni kiasi kidogo tu cha “habari njema” kwamba wamekosea ikiwa wanadhani kwamba matendo mema au kumtii Mungu ni sehemu ya wokovu. Cha muhimu ni “kumkubali Yesu kama Mwokozi binafsi”.
Ukilinganisha na kanisa la kwanza, Wakristo wale (ambao kweli Yesu alikuwa Bwana kwao) walikuwa wanaonekana kama taa gizani, hivyo, hawakuwa na haja ya kujifunza jinsi ya kushuhudia au kutafuta ujasiri wa kuwaeleza jirani zao kwamba ni wafuasi wa Kristo. Walikuwa na nafasi nyingi tu za kushuhudia maana waliulizwa maswali kwa sababu ya haki yao, au walidhihakiwa. Wao – kama Petro alivyowaambia – walimtakasa tu Bwana mioyoni mwao na kuwa tayari kutoa majibu.
Pengine tofauti kubwa kati ya Wakristo wa kisasa na wale wa kwanza ni hii: Wakristo wa kisasa wanadhani kwamba Mkristo hutokana na kile anachojua na kuamini – huitwa “itikadi”. Basi sisi hulenga juhudi zetu kwenye kujifunza. Kinyume chake ni hivi: Wakristo wa kwanza waliamini kwamba Mkristo alijulikana kwa matendo yake. Basi, walitilia mkazo kutii amri za Kristo. Ni ajabu kutambua kwamba kihalisi kabisa, kwa karne kumi na nne za kwanza hakuna Mkristo aliyekuwa na Biblia yake binafsi – hivyo haikuwezekana kwake “kujisomea Biblia yake kila siku” – kitu ambacho kimekuwa kama sheria kuu na wajibu wa siku hizi wa Mkristo. Si kwamba Wakristo wa siku hizi hawapaswi kusoma Biblia zao kila siku. Ni kwamba Wakristo wengi wamefanya kusoma Biblia kila siku kuwa muhimu kuliko kuitii. Hatimaye tunajisifu kwamba sisi tuna itikadi sahihi (kinyume na wale washirika wa madhehebu mengine elfu ishirini na tisa, mia tisa tisini na tisa ambao hawajafikia kiwango chetu), ila bado tunasengenya, tunadanganya na kujiwekea hazina duniani.
Kama tunatazamia kulainisha mioyo ya watu ili waweze kupokea Injili kwa urahisi zaidi, itawezekana kwa matendo yetu kuliko kwa itikadi zetu!
Mungu – Mwinjilisti Mkuu
Hebu sasa tutazame kwa upana zaidi kazi ya Mungu katika kujenga ufalme Wake. Tukielewa vizuri utendaji Wake, tutashirikiana Naye kwa ubora zaidi.
Watu wanapomwamini Yesu, ni kitu kifanyikacho mioyoni mwao (ona Warumi 10:9, 10). Wanamwamini Bwana Yesu, na wanatubu. Wanaondoa mapenzi yao kwenye kiti cha enzi na kumweka Yesu kwenye kiti cha enzi cha nia zao. Kuamini ni badiliko la moyo.
Pia, watu wanapokuwa hawamwamini Yesu, ni kitu wanachofanya kwa mioyo yao. Wanampinga Mungu, hivyo hawatubu. Kwa uamuzi wa hiari kabisa, wanamwondoa Yesu kwenye kiti cha enzi cha mioy yao. Kutokuamini ni uamuzi unaoendelea wa kutobadili moyo.
Yesu alionyesha kwamba mioyo ya watu wote ni migumu kiasi cha kwamba hakuna awezaye kumwendea, asipovutwa na Baba (ona Yohana 6:44). Mungu ni mwenye rehema na anaendelea kuwavuta watu wote wamjie Yesu kwa namna mbalimbali, ambazo zote hugusa mioyo yao, na ambazo zinawalazimisha kuchagua kulainisha mioyo yao au kuifanya migumu.
Je, Mungu hutumia nini ili kugusa mioyo ya watu kwa matumaini ya kuwavutakwa Yesu?
Kwanza – Anatumia uumbaji Wake. Paulo aliandika hivi:
Kwa maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu. Kwa kuwa mambo ya Mungu yanayojulikana yamekuwa dhahiri ndani yao, kwa maana Mungu aliwadhihirishia. Kwa sababu mambo yake yasiyo-onekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana na kufahamika kwa kazi zake; yaani; uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru (Warumi 1:18-20. Maneno mepesi kukazia).
Ona hapo kwamba Paulo anasema, watu “huuzuia ukweli” ulio “dhahiri ndani yao.” Yaani, ukweli hutokeza ndani yao na kuwakabili, lakini wanausukumizia chini, kisha wanapingana na huo ushuhuda wa ndani.
Hiyo kweli iliyoko ndani ya kila mtu, na iliyo dhahiri, ni ipi? Paulo alisema ni kweli kuhusu “mambo yasiyo-onekana – uweza Wake wa milele na Uungu Wake,” yanayodhihirishwa “kwa kazi Zake”. Kwa ndani, watu wanajua wanapotazama uumbaji wa Mungu kwamba yupo bila shaka,[1] na kwamba ana uwezo sana, ni mbunifu katika uumbaji Wake, ana hekima sana na ufahamu – kwa uchache tu.
Hitimisho la Paulo ni kwamba watu kama hao “hawana udhuru,” naye anasema sawa. Mungu kila mara anampazia kila mtu sauti, akijifunua Mwenyewe na kujaribu kuwafanya walainishe mioyo yao, lakini wengi hufunga masikio yao, wasimsikilize Mungu. Ila Yeye haachi kupaza sauti Yake maisha yao yote, kwa kuwaonyesha miujiza mara kwa mara – kwa njia ya maua, ndege, watoto, theluji, ndizi, maembe, na vitu milioni nyingi vingine.
Kama Mungu yupo, Naye ni mkuu kama uumbaji Wake unavyoonyesha, bila shaka watu wanapaswa kumtii. Huo ufunuo wa ndani unapaza sauti na kutoa ujumbe mmoja tu mkubwa: Tubu! Kwa sababu hiyo, Paulo anasema kwamba kila mtu amekwisha sikia mwito wa Mungu wa toba.
Lakini nasema, Je! Wao hawakusikia? Naam, wamesikia. Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu (Warumi 10:18).
Hapo Paulo alikuwa anarudia maneno maarufu ya Zaburi ya 19, inayosema hivi kwa ukamilifu zaidi:
Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa. Hakuna lugha wala maneno, sauti yao haisikilikani. Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu (Zaburi 19:1-4a. Maneno mafupi kukazia).
Hii tena huonyesha kwamba Mungu anazungumza na kila mtu, mchana na usiku, kupitia uumbaji Wake. Kama watu wangeitikia ipasavyo ujumbe wa Mungu katika uumbaji, wangeanguka kifudi-fudi na kusema hivi: “Ee Muumbaji Mkuu! Umeniumba mimi, na bila shaka uliniumba nifanye mapenzi Yako. Basi, nakukubali Wewe!”
Njia Nyingine Mungu Anayotumia Kuzungumza
Pamoja na huo ufunuo wa nje na ndani, kuna ufunuo mwingine wa ndani, ambao nao unatoka kwa Mungu, na ambao hautegemeani na mtu kuona miujiza ya uumbaji. Huo ufunuo wa ndani ni dhamiri ya kila mtu, ambayo ni sauti yenye kudhihirisha sheria ya Mungu kwa kuendelea. Paulo aliandika hivi juu yake:
Kwa maana watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yalyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kw anafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya Torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe, yakiwashtaki au kuwatetea; katika siku ile Mungu atakapozihukumu siri za wanadamu, sawasawa na injili yangu, kwa Kristo Yesu (Warumi 2:14-16).
Basi, kila mtu anajua kilicho sawa, na kilicho kosa. Au – kwa lugha nzito zaidi – kila mtu anajua kinachompendeza Mungu, na kisichompendeza Mungu. Na Mungu atamtaka kila mtu kujieleza siku ya hukumu, kwa kufanya kile alichojua kwamba hakimpendezi Yeye. Watu wanapozeeka, wanakuwa mafundi wa kutetea dhambi zao na kupuuza sauti ya dhamiri zao, lakini Mungu haachi kutamka Sheria Yake ndani yao.
Njia Ya Tatu
Si hayo tu. Mungu – mwinjilisti mkuu – anayefanya juhudi ili kumleta kila mtu kwenye toba, husema na watu kwa njia nyingine tena. Tunasoma tena maneno ya Paulo.
Kwa maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu, waipingao kweli kwa uovu (Warumi 1:18. Maneno mepesi kukazia).
Ona Paulo anachosema – ghadhabu ya Mungu imefunuliwa, si kwamba tafunuliwa siku moja. Ghadhabu ya Mungu ni dhahiri kwa kila mtu katika matukio mengi ya kusikitisha na kutisha – makubwa na madogo – yenye kukabili binadamu. Kama Mungu ana nguvu zote, mwenye uwezo wa kufanya chochote na kuzuia chochote, ni kwamba mambo hayo, yanapowapiga wale wanaompuuza, ni madhihirisho ya ghadhabu Yake tu. Ni wanatheolojia wasio na akili nzuri na wanafalsafa wa aina hiyo ndiyo wameshindwa kutambua hilo jambo. Lakini, hata katika ghadhabu Yake, rehema za Mungu na upendo Wake vinadhihirishwa, kwa sababu wale wanaolengwa na hasira Yake mara nyingi hawapati ghadhabu kama inavyostahili. Basi, kwa upendo wanaonywa juu ya ghadhabu ya milele inayowasubiri wasiotubu baada ya kifo chao. Hii ni njia nyingine ambayo Mungu huitumia ili kuwafanya watu wanaohitaji kutubu wasikie sauti Yake.
Namna Ya Nne
Hatimaye – Mungu sit u kwamba anajaribu kuwavuta watu kwa njia ya uumbaji, dhamiri na majanga, bali pia hutumia wito wa Injili. Watumishi Wake wanapomtii na kutangaza habari njema, ujumbe ule ule utolewao na uumbaji, dhamiri na majanga unarudiwa kwa mara nyingine tena: Tubuni!
Unaweza sasa kuona kile tunachofanya sisi katika uinjilisti, ukilinganisha na kile Mungu anachofanya. Yeye daima anamshuhudia kila mtu kila dakika ya kila siku ya maisha yake, wakati ambapo hata mwinjilisti yule maarufu sana wa kibinadamu ataweza kusema na watu laki kadhaa katika kipindi cha miongo kadhaa. Na hao wainjilisti kwa kawaida huwahubiria watu wa kundi fulani mara moja tu kwa kipindi fulani pia. Ukweli ni kwamba, hiyo nafasi moja tu ndiyo wanayopewa wainjilisti wa aina hiyo ili kuwapa watu nafasi ya kufuta mavumbi ya miguu yao, popote wasipokaribishwa mjini au kijijini, kulingana na agizo la Yesu (ktk Mathayo 10:14). Tunachosema hapa ni kwamba, ukilinganisha uinjilisti wa Mungu usiokoma, wa ulimwengu wote, wa vitendo, wenye kusema na mtu ndani, na uinjilisti wetu sisi wenye mipaka sana, hakuna hata cha kulinganisha!
Mtazamo huu unatusaidia kuelewa vizuri wajibu wetu katika uinjilisti, na katika kujenga ufalme wa Mungu. Lakini, kabla ya kutazama nafasi au kazi yetu sisi, kuna jambo lingine muhimu sana ambalo tunapaswa tusilisahau.
Kama tulivyoona mapema, kutubu na kuamini ni vitu vinavyofanywa na watu katika mioyo yao. Mungu anatamani kwamba kila mtu ajinyenyekeze, alainishe moyo wake, atubu na kumwamini Bwana Yesu. Kutimiza lengo hilo, Mungu daima anashughulika na mioyo ya watu kwa njia zile nyingi tulizokwisha taja.
Ila – Mungu pia anajua hali ya moyo wa kila mtu. Anajua ni mioyo gani inalainika, na ipi inakuwa migumu zaidi. Anajua nani anasikiliza jumbe Zake zisizokoma, na mwenye kuzipuuza. Anajua mioyo ya nani imefikia mahali ambapo janga fulani litaifungua na kupelekea kutubu. Anajua mioyo gani imekuwa migumu kiasi kwamba hakuna matumaini ya toba yao. (Kwa mfano: Alimwamia Yeremia mara tatu kwamba asiombee Israeli kwa sababu mioyo yao ilikuwa imepita mahali pa kutubu – Yeremia 7:16; 11:14; 14:11).[2] Anaifahamu hata mioyo inayoendelea kulainika kiasi kwamba kushawishiwa kidogo tu na Roho Wake kutaleta toba.
Tukizingatia hayo yote, tunajifunza nini basi kuhusu wajibu wa makanisa katika kutangaza Injili na kujenga ufalme wa Mungu?
Kanuni Ya Kwanza
Kwanza – Ni sahihi kudhani kwamba bila shaka Mungu – Mwinjilisti Mkuu – anayefanya asilimia 95 ya kazi ya msingi, na ambaye amekuwa akipaza sauti Yake kwa kila mtu kila siku, atawatuma watumishi Wake kwenda kuitangaza Injili kwa wale ambao mioyo yao iko tayari kupokea zaidi kuliko kwa wale ambao mioyo yao haiku tayari kupokea.
Bila shaka inawezekana kwamba Mungu – Mwinjilisti Mkuu – ambaye amekuwa akiwahubiri watu wote kila dakika ya maisha yao, aamue kutokutuma Injili kwa wale ambao wamekuwa wakipuuza kila kitu ambacho amekuwa akiwaambia miaka na miaka. Kwa nini apoteze juhudi Zake kuwaambia watu asilimia 5 ya mwisho ya kile ambacho angetaka wajue, kama wamekuwa wakipuuza kabisa asilimia 95 ya kile cha kwanza ambacho amekuwa akijaribu kuwaambia? Nadhani Mungu angetuma hukumu kwa watu wa aina hiyo, kwa matumaini kwamba watalainisha mioyo yao. Ikitokea hivyo, basi baadaye ndipo angetuma watumishi Wake kuitangaza Injili.
Wengine watasema kwamba Mungu atawatuma watumishi Wake kutangaza Injili kwa wale anaojua hawatatubu ili wasiwe na udhuru watakaposimama mbele Yake kuhukumiwa. Kumbuka kwamba, kulingana na Maandiko, watu aina hiyo hawana udhuru tayari mbele za Mungu, kwa sababu ya mafunuo Yake kwao, yasiyokoma, kupitia uumbaji Wake (Ona Warumi 1:20). Hivyo basi, kama Mungu akimtuma mtumishi Wake mmoja kwenda kwa watu hao, haitakuwa ili wasiwe na udhuru, bali ili wasipate jinsi ya kujitetea kabisa!
Kama ni kweli kwamba Mungu atawaongoza watumishi Wake kwa watu wenye kusikiliza zaidi, basi sisi, watumishi Wake, tunapaswa kumwomba hekima Yake ili tuweze kuongozwa kwa wale anaojua Yeye kwamba wako tayari kwa mavuno.
Mfano Wa Maandiko
Kanuni hii inaonyeshwa vizuri sana katika huduma ya Filipo mwinjilisti, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Matendo. Filipo alikuwa amehubiri mkutano kwa watu waliokuwa wasikivu sana huko Samaria, lakini baadaye akaongozwa na malaika kusafiri kwenda njia fulani. Huko akaongozwa kwa mtu mwenye kutafuta, aliyekuwa tayari kabisa.
Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza, nayo ni jangwa. Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu. Akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelewa hayo unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili:
Aliongozwa kwenda machonjoni kama kondoo, na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhli kwake hukumu yake iliondolewa, ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi.
Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu; asema maneno haya kwa habari ya nani: ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu. Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe? Filipo akasema, Ukiamini kwa moyo wako wote, inawezekana. Akajibu akanena, Naamini ya kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu. Akaamuru lile gari lisimame; wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza. Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi (Matendo 8:26-39).
Filipo aliongozwa na Mungu kwenda kumhudumia mtu ambaye alikuwa na njaa kiroho kiasi cha kusafiri kutoka Afrika kwenda Yerusalemu kumwabudu Mungu, na ambaye alinunua kipande cha gombo la unabii wa Isaya. Alipokuwa anajisomea sura ya 53 ya Isaya – andiko wazi kabisa katika Agano la Kale lenye kueleza habari za sadaka ya kujitoa ya Kristo – na alipokuwa akijiuliza Isaya aliandika juu ya nani, Filipo akawa amefika, tayari kueleza alichokuwa anasoma! Alikuwa tayari kuokoka huyo! Mungu aliujua moyo wake, na akamtuma Filipo.
Njia Bora Zaidi
Kuna matokeo zaidi kuongozwa na Roho kwa watu walio tayari, kuliko kujichagulia tu au kupanga mpango wa kusema na watu ambao hawako tayari kupokea kwa sababu tunadhani kwamba tutakuwa na hatia wasipofikiwa. Usisahau – kila mtu unayekutana naye anashuhudiwa sana na Mungu Mwenyewe. Itakuwa vizuri zaidi kama tutawauliza watu dhamiri yao inasemaje ili kuamua kama wako tayari kumsikiliza Mungu au hapana, maana kila mtu anashughulika na hatia kwa namna fulani.
Mfano mwingine wa kanuni hii ni kuokoka kwa nyumba nzima ya Kornelio katika huduma ya Petro, ambaye aliongozwa na Mungu kwenda kuhubiri Injili kwa kundi hilo la watu wa Mataifa, lililokuwa tayari. Kornelio alikuwa mtu mwenye kusikiliza dhamiri yake na kumtafuta Mungu, kama inavyo-onekana kwa utoaji wake sadaka na uombaji wake (ktk Matendo 10:2). Mungu alimwunganisha na Petro, naye alisikiliza mahubiri ya Petro kwa moyo ulio wazi, akaokoka kabisa.
Tungekuwa na busara zaidi kama tungemwomba Roho Mtakatifu atuongoze kwa wale ambao mioyo yao iko wazi badala ya kupanga mipango mikubwa yenye kupoteza wakati ya kuigawa miji yetu katika visehemu na kuunda vikundi vya ushuhudiaji ili kutembelea kila nyumba. Kama Petro angekuwa anahudhuria mkutano kuhusu mbinu au mikakati ya umishenari huko Yerusalemu, au kama Filipo angeendelea kuhubiri huko Samaria, nyumba ya Kornelio na yule towashi wa Kushi wasingefikiwa.
Mitume na wainjilisti wataongozwa kutangaza Injili kwa makundi ya watu mchanganyiko – walio tayari na wasio tayari. Lakini hata wao wanapaswa kumtafuta Bwana kwa habari ya ni wapi anapotaka wakahubiri. Tena, taarifa ipatikanayo katika kitabu cha Matendo inawahusu watu waliojaa na kuongozwa na Roho wakishirikiana Naye katika ujenzi wa ufalme wa Mungu. Mbinu za kanisa la kwanza zilikuwa tofauti kabisa na mbinu za kanisa la siku hizi. Hata matokeo ni tofauti! Mbona tusiige kitu kinachofaulu?
Kanuni Ya Pili
Je, zile kanuni za Biblia tulizotazama mwanzoni mwa sura hii zinatusaidiaje tena kuelewa nafasi yetu katika uinjilisti na kujenga ufalme wa Mungu?
Kama Mungu amepanga kwamba uumbaji, dhamiri na majanga ni miito kwa binadamu kutubu, basi wale wanaohubiri Injili wanahitaji kuwa na uhakika kwamba hawatangazi ujumbe tofauti. Lakini, wengi wao wanatangaza ujumbe tofauti! Mahubiri yao yanapingana kabisa na kila kitu ambacho Mungu anajaribu kuwaambia wenye dhambi! Ujumbe wao wa neema isiyokuwa ya Biblia unakuza wazo kwamba utakatifu na kutii si muhimu kwa ajili ya kupata uzima wa milele. Kwa kutokutaja umuhimu wa toba kwa wokovu, kwa kukazia kwamba wokovu si wa matendo (ambavyo ni tofauti na jinsi Paulo alitaka kusema), wao wanafanya kazi kinyume cha Mungu, wakiwaongoza watu katika udanganyifu mkubwa zaidi ambao mara nyingi huwaingiza katika upotevu wa milele, kwa sababu wanakuwa na hakika kwamba wameokoka, kumbe bado. Ni sikitiko kubwa sana wakati wajumbe wa Mungu wanaofanya kazi kinyume na Mungu wanayedai wanamwakilisha!
Yesu alituagiza kuhubiri “toba kwa ajili ya ondoleo la dhambi” (ktk Luka 24:47). Ujumbe huo unathibitisha tena kile ambacho Mungu amekuwa akimwambia mwenye dhambi maisha yake yote. Mahubiri ya Injili huwachoma watu mioyo yao na kuwakwaza wale ambao mioyo yao ni migumu. Lakini, Injili ya siku hizi, laini kabisa, yenye kuwaambia watu jinsi ambavyo Mungu anawapenda sana (kitu ambacho hakuna mtume yeyote aliyewahi kutaja wakati akihubiri Injili katika kitabu cha Matendo), huwafanya wafikiri kwa makosa kwamba Mungu hajakasirika nao, wala hajachukizwa nao. Mara nyingi wanaambiwa kwamba wanahitaji “kumkubali yesu” tu. Lakini Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana hahitaji kukubaliwa na sisi. Swali kubwa si: “Je, unamkubali Yesu?” bali ni, “Je, Yesu anakukubali wewe?” Jibu lake ni hili: Usipotubu na kuanza kumfuata, unamchukiza, na rehema Zake tu ndiyo zinachelewesha kuingia kwao jehanamu.
Kutokana na injili ya kisasa yenye kurahisisha mno neema ya Mungu, inashangaza ni kwa nini mataifa mengi, yenye kuongozwa na watu ambao wamepewa mamlaka yao na Mungu (na hilo si jambo la kubishania – ona Danieli 4:17, 25, 32; 15:21; Yohana 19:11; Matendo 12:23; Warumi 13:1) yalivyoamua kufunga milango yao kabisa kwa wamishenari wa Magharibi. Je, yawezekana ikawa ni kwa sababu Mungu anataka kuzuia hiyo injili ya uongo isifike huko?
Kanuni Ya Tatu
Kanuni zilizotazamwa mapema katika sura hii pia zinatusaidia kuelewa jinsi Mungu anavyowaona watu wanaofuata dini za uongo. Je, ni wapumbavu wa kuhurumiwa kwa kuwa hawajawahi kusikia ukweli? Je, lawama zote juu yao ni kwa kanisa, ambalo halijafanya uinjilisti kikamilifu ili kuwafikia?
Hapana. Watu aina hiyo wanajua ukweli. Wanaweza wasijue kila kitu ambacho Mkristo mwenye kuamini Biblia anakijua, lakini wanajua kila kitu ambacho Mungu anadhihirisha juuYake Mwenyewe kwa njia ya uumbaji, dhamiri na majanga. Hao ni watu ambao Mungu amekuwa akiwaita watubu maisha yao yote, hata kama hawajawahi kumwona Mkristo wala kusikia Injili. Tena, aidha wamekuwa wakifanya mioyo yao kuwa laini kumwelekea Mungu, au wameifanya kuwa migumu.
Paulo aliandika hivi juu ya ujinga wa wasioamini, na kuifunua sababu yake.
Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao; akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani (Waefeso 4:17-19).
Ona kwamba sababu ya Mataifa kutokujua ni “kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao.” Paulo pia alitangaza kwamba “wamekufa ganzi”. Bila shaka alikuwa anasema juu ya hali ya mioyo yao. Sugu hutokea kwenye mikono ya watu kutokana na saa zote kushika kitu ambacho ni kigumu kwa ngozi laini. Ngozi yenye sugu hupoteza uwezo wake wa kusikia. Vivyo hivyo, kadiri watu wanavyoendelea kupinga mwito wa Mungu kupitia uumbaji, dhamiri na majanga, mioyo yao hupata sugu, na kuwafanya kuendelea kutosikia mwito wa Mungu. Hii ndiyo sababu takwimu zinaonyesha kwamba watu hupunguza kusikia na kupokea Injili wanapozidi kuwa watu wazima kiumri. Kadiri mtu anavyozidi kuzeeka, si rahisi kwake kutubu. Wainjilisti wenye hekima huwalenga zaidi vijana.
Hatia Ya Wasioamini
Uthibitisho zaidi kwamba Mungu huwahesabia watu hatia hata kama hawajawahi kumsikia mwinjilisti Mkristo ni ukweli kwamba Yeye huwahukumu mara kwa mara. Kama Mungu angekuwa hawahesabu kuwa na hatia kwa ajili ya dhambi zao, asingewaadhibu. Ka kuwa anawaadhibu, ni hakika kabisa kwamba anawahesabu kuwa na hatia, na kama ni hivyo, lazima wajue kwamba wanachokifanya hakimpendezi Yeye.
Njia moja ambayo Mungu hutumia kuwaadhibu wale wanaopingana na mwito Wake wa toba ni “kuwachilia” waingie katika tamaa zao mbaya ili wazidi kuwa watumwa, na kuharibikiwa zaidi. Paulo aliandika hivi juu ya jambo hilo:
Kwa sababu, walipomjua Mungu, hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza. Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aiye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo.
Kwa ajili ya hayo, Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao. Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba anayehimidiwa milele. Amina.
Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana t amaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.
Na kama walivyokataa kuwa na Mungui katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa. Wamejawa na udhalimu wa kila namna, uovu na tamaa na ubaya; wamejawa na husuda, na uuaji, na fitina, na hadaa; watu wa nia mbaya, wenye kusengenya, wenye kusingizia, wenye kumchukia Mungu, wenye jeuri, wenye kutakabari, wenye majivuno, wenye kutunga mabaya, wasiowatii wazazi wao, wasio na ufahamu, wenye kuvunja maagano, wasiopenda jamaa zao, wasio na rehema; ambao wakijua sana hukumu ya haki ya Mungu, ya kwamba wayatendao hayo wamestahili mauti, wanatenda hayo, wala si hivyo tu, bali wanakubaliana nao wayatendao (Warumi 1:21-32. Maneno mepesi kukazia).
Ona jinsi Paulo anavyotilia mkazo kweli za hatia ya binadamu na kuwajibika kwake mbele za Mungu. Wasiozaliwa mara ya pili “walimjua Mungu,” lakini “hawakumtukuza kama Mungu, wala kumshukuru.” Walibadilisha “kweli ya Mungu kuwa uongo,” kwa hiyo bila shaka walikutana na kweli ya Mungu. Hivyo, Mungu “akawaacha” waingie katika uharibifu unaoendelea, mpaka kufikia mahali ambapo watu hufanya mambo ya ajabu, ya kutisha, na ya aibu sana, kadiri wanavyoendelea kufungwa na dhambi. Mungu anachosema ni hiki: “Je, mnataka kutumikia dhambi kama ambavyo mngenitumikia? Haya basi! Endeleeni. Sitawazuia, nanyi mtazidi kufungwa kwa huyo mungu mnayempenda.”
Nadhani aina hii ya hukumu inaweza kuonekana kama rehema za Mungu pia, kwa sababu ni sahihi kufikiri kwamba kadiri watu wanavyozidi kuharibika na kuwa wenye dhambi, watatambua na kuamka. Mtu anashangaa sababu ya walawiti wengi kutokujiuliza hivi: “Mbona navutwa kwa watu ambao ni wa jinsia kama yangu, ambao siwezi kuwa na mahusiano kamili ya kimwili nao? Hii inashangaza!” Kwa namna fulani yawezekana kufikiri kwamba kweli Mungu “aliwaumba hivyo” (kama wenyewe wanavyojitetea katika kuhalalisha uharibifu wao), lakini ni kwa kuwaruhusu tu, na ni kwa sababu anakusudia kuwaamsha ili waweze kutubu na kujua rehema Zake za ajabu au kushangaza.
Si walawiti tu wanaopaswa kujiuliza maswali kama hayo. Paulo aliorodhesha dhambi nyingi tu zenye kumfunga mtu ambazo ni ushahidi wa hukumu ya Mungu juu ya wale wanaokataa kumtumikia. Mabilioni ya watu wangejiuliza juu ya tabia zao za ajabu. “Kwa nini ninaichukua familia yangu?” “Kwa nini nitosheke na kueneza uvumi?” “Kwa nini sitosheki na vitu nilivyo navyo?” “Kwa nini ninasukumwa kutazama picha za ngono zaidi na zaidi?” Mungu amewatoa hao wote ili wafungwe na kuwa watumwa wa mungu wao.
Ikifikia hapo, yeyote katika mahali popote anaweza kulainisha moyo wake, akatubu na kumwamini Yesu. Baadhi ya wenye dhambi wagumu zaidi duniani wamefanya hivyo, na Mungu amewasafisha na kuwaweka huru kutokana na dhambi zao! Mradi watu bado wanapumua, Mungu bado anawapa wao nafasi ya kutubu.
Hakuna Udhuru
Kulingana na Paulo, wenye dhambi hawana udhuru. Wanadhihirisha kwamba wanajua kilicho sawa na kilicho kosa wanapowahukumu wengine, na basi wanastahili hukumu ya Mungu hata wao.
Kwa hiyo, wewe mtu uwaye yote uhukumuye, huna udhuru; kwa maana katika hayo umhukumuyo mwingine wajihukumu mwenyewe kuwa na hatia; kwa maana wewe umhukumye unafanya yale yale. Nasi twajua ya kuwa hukumu ya Mungu ni ya kweli juu yao wafanyao hayo. Wwe binadamu, uwahukumuye wale wafanyao hayo na kutenda yayo hayo mwenyewe, je, wadhani ya kwamba utajiepusha na hukumu ya Mungu? Au waudharau wingi wa wema wake na ustahimili wake na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu? (Warumi 2:1-4).
Paulo anasema sababu ya uvumilivu wa Mungu na ustahimilivu Wake ni ili kuwapa watu nafasi ya kutubu. Tena, alipoendelea Paulo, alidhihirisha kwamba wale wanaotubu na kuishi maisha matakatifu ndiyo watakaoingia katika ufalme wa Mungu.
Bali kwa kadiri ya ugumu wako, na kwa moyo wako usio na toba, wajiwekea akiba ya hasira kwa siku ile ya hasira na ufunuo wa hukumu ya haki ya Mungu, atakayemlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake; wale ambao kwa saburi katika kutenda mema wanatafuta utukufu na heshima na kutokuharibika, watapewa uzima wa milele; na wale wenye fitina, wasioitii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu; dhiki na shida juu ya kila nafsi ya mwanadamu atendaye uovu, Myahudi kwanza na Myunani pia; bali utukufu na heshima na amani kwa kila mtu atendaye mema, Myahudi kwanza na Myunani pia (Warumi 2:5-10).
Ni wazi kwamba Paulo asingekubaliana na wale wenye kufundisha kwamba watu “humpokea Yesu kama Mwokozi tu” na kuhakikishiwa uzima wa milele. Ni wale wenye kutubu, na ambao kwa “uvumilivu katika kutenda mema hutafuta utukufu na heshima na uzima wa milele”.
Lakini je, hii haionyeshi kwamba watu wanaweza kuendelea kufuata dini zingine ambazo si Ukristo na waokoke, mradi tu watubu na kumtii Mungu?
Hapana – hakuna wokovu nje ya Yesu kwa sababu nyingi tu, mojawapo ikiwa ukweli kwamba ni Yesu tu awezaye kuwaweka watu huru kutokana na utumwa wa dhambi.
Lakini sasa – wakitaka kutubu, watajuaje jinsi ya kumwita Yesu ambaye hawajawahi kumsikia?
Mungu – anayeijua mioyo ya watu wote – atajifunua Mwenyewe kwa yeyote ambaye anatafuta kwa dhati. Yesu aliahidi hivi: “Tafuteni nanyi mtaona” (Mathayo 7:7), na Mungu anamtazamiakila mmoja kumtafuta (ona Matendo 17:26, 27). Anapomwona mtu ambaye moyo wake unamwitikia katika uinjilisti Wake, atatuma injili kwa mtu huyo, sawa na alivyofanya kwa yule towashi wa Kushi na nyumba ya Kornelio. Wala Mungu hafungwi na kujihusisha kwa kanisa, kama alivyothibitisha katika kumwokoa Sauli wa Tarso. Kama hakuna mtu yeyote wa kupeleka Injili kwa mtafutaji wa dhati, Mungu atakwenda Mwenyewe! Nimepata kusikia matukio ya siku hizi ambapo watu wanaoishi katika nchi zilizofungwa Injili isiiingie walivyookolewa kwa maono ya Yesu.
Sababu Ya Watu Kuwa Wa Dini
Ukweli ni kwamba wengi wa watu wanaofuata dini za uongo si watafutaji wa kweli kwa dhati. Ila, ni watu wa dini kwa sababu wanatafuta kitu cha kuhalalisha au kufunika dhambi zao. Na wanapozidi kuharibu dhamiri zao, wanajificha nyuma ya dini. Kwa kujifanya ni watu wa dini, wanajishawishi kwamba hawastahili kwenda jehanamu. Ndivyo ilivyo hata kwa “Wakristo” wa dini (pamoja na Wakristo wenye kuamini injili lakini wenye kurahisisha neema), kama ilivyo kwa wenye kufuata imani ya Buda, Waislamu na Wahindu. Wanapotenda matendo ya dini yao, dhamiri zao huwashtaki na kuwahukumu.
Wakati mfuasi wa dini ya Buda anapoinama kwa heshima kabisa mbele ya sanamu zake, au mbele ya watawa wanaoketi kwa kiburi mbele yake, dhamiri yake inamwambia anafanya makosa. Wakati mfuasi wa dini ya Hindu anapotetea utovu wake wa huruma kwa mwombaji mgonjwa mtaani, akiamini kwamba huyo mwombaji anapata mateso kwa sababu ya dhambi zake alizotenda katika maisha aliyoishi kabla ya haya, dhamiri yake inamshtaki na kumhukumu. Wakati Mwislamu wa siasa kali anapomkata “kafiri” kichwa katika jina la Allah, dhamiri yake inampigia kelele kwa sababu ya unafiki wake wenye kuua. Wakati “Mkristo” mwenye kuamini injili anapojiwekea hazina duniani, na kutazama vipindi vya ngono kwenye televisheni kila mara, na kuwasengenya washirika wenzake, akiamini kwamba ameokolewa kwa neema, moyo wake unamhukumu. Hiyo yote ni mifano ya watu wanaotaka kuendelea kutenda dhambi na ambao wamegundua uongo katika dini, wenye kuwafanya waamini kwamba wanaweza kuendelea kutenda dhambi. “Haki” ya watu ambao hawajaokoka japo wana dini hupungua kabisa kabisa kwenye matarajio ya Mungu.
Yote haya ni kusema kwamba Mungu hawahesabu watu wanaofuata dini za uongo kwamba ni wajinga wa kuhurumiwa kwa kuwa hawajawahi kusikia ukweli. Wala lawama ya ujinga wao haiwekwi miguuni pa kanisa kwa kutowafikishia Injili ipasavyo.
Japo tunajua kwamba Mungu anataka kanisa lihubiri Injili duniani kote, tunapaswa kufuata uongozi wa Roho Wake ili kwenda “mashamba yalipo tayari kwa mavuno” (ona Yohana 4:35), yaani, mahali ambapo watu wako tayari kwa sababu wamekuwa wakilainisha mioyo yao kukubali juhudi za Mungu zisizoshindwa za kuwafikia.
Kanuni Ya Nne
Kanuni moja ya mwisho tunayoweza kujifunza kutokana na kweli za Biblia tulizotazama mapema ni hii: Kama Mungu anaendelea kuwahukumu wenye dhambi kwa matumaini kwamba watalainisha mioyo yao, sisi tutazamie kwamba, baadhi yao, baada ya kupitia hukumu ya Mungu au kuwaona wenzao wakipitia, watalainisha mioyo yao. Basi, baada ya majanga, kuna nafasi za kuwafikia watu ambao walikuwa hawafikiki kabla ya hapo.
Wakristo watafute nafasi za kueleza Injili katika maeneo ambapo watu wanateseka. Wale ambao wamepoteza wapendwa wao siku za karibuni, wanaweza kuwa wazi zaidi kusikiliza kile ambacho Mungu anataka wasikie. Nilipokuwa mchungaji, nilikuwa natumia nafasi za maziko kusema Injili, nikikumbuka lile andiko lisemalo, “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kw amaana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake (Mhubiri 7:2. Maneno mepesi kukazia).
Watu wakiwa wagonjwa, wakipata hasara kifedha, mahusiano yanapoharibika, majanga ya kawaida yanapotokea na matokeo mengi ya dhambi na hukumu juu ya dhambi yanapowapata, wanahitaji kujua kwamba mateso yao ni mwito kwao, waamke. Kupitia mateso ya muda Mungu anajaribu kuwaokoa wenye dhambi wasiende kwenye hukumu ya milele.
Hitimisho
Mungu hufanya sehemu kubwa ya kazi ya kuujenga ufalme Wake. Wajibu wetu ni kushirikiana Naye kwa akili na kwa uzuri.
Waamini wote wanapaswa kuishi maisha matakatifu na yenye kumtii Mungu, yanayovuta usikivu wa walio gizani. Tena, wawe tayari wakati wote kujibu kuhusu tumaini lililo ndani yao.
Siku zote Mungu anafanya kazi ya kuwahamasisha watu wote kulainisha mioyo yao na kutubu, akizungumza nao kila wakati kupitia uumbaji, dhamiri na majanga, na wakati mwingine kwa njia ya mwito wa Injili.
Wenye dhambi wanajua kwamba wanamwasi Mungu, na wanawajibika Kwake hata kama hawataisikia Injili. Dhambi yao ni ushahidi wa ugumu wa mioyo yao. Kuharibikiwa kwao zaidi na zaidi na utumwa katika dhambi ni ishara ya ghadhabu ya Mungu kwao.
Watu wa dini si kwamba wanatafuta ukweli. Sana sana wanatafuta uhalali wa dhambi yao kwa kuamini uongo wa dini zao.
Mungu anaijua mioyo ya kila mtu. Ingawa anaweza kutuongoza tukawaambie Injili watu ambao hawako tayari wala hawapokei, anaweza kutuongoza zaidi kwa wale ambao wako tayari kusikia na kupokea Injili.
Mungu anapofanya kazi ya kulainisha mioyo ya watu kwa njia ya mateso yao, tunapaswa kutumia nafasi hizo kuhubiri Injili.
Mungu anataka tupeleke Injili duniani kote, lakini anataka tumfuate Roho Wake, tunapotafuta kutimiza Agizo Kuu. Tunaona mfano katika Kitabu cha Matendo.
Mungu atajifunua Mwenyewe kwa yeyote anayetaka kumjua kwa dhati.
Mungu anataka ujumbe wetu ukubaliane na ujumbe Wake.
Siku moja watakuwepo wawakilishi kutoka kila kabila, wakiabudu mbele za kiti cha enzi cha Mungu, nasi tunapaswa kufanya kila tuwezacho kushirikiana na Mungu kufanikisha hilo. Hivyo, watu wote wa Mungu wanapaswa kuonyesha upendo wa Kristo kwa watu kutoka kila kila kabila wanaokutana nao. Mungu anaweza kuwaongoza baadhi ya watumishi Wake kulenga watu wa utamaduni fulani, kwa kutuma na kuwategemeza watu wa kuanzisha makanisa, au kwa kwenda wenyewe. Wale wanaokwenda wafanye watu kuwa wanafunzi, wakijithibitisha kuwa watumishi wafanyao wengine kuwa wanafunzi!
Maneno Ya Kumalizia
Namshukuru Mungu sana kwa kuniwezesha kuchapa kitabu hiki katika lugha yako, na kukuwezesha kupata nakala yako ujisomee. Natumaini kimekuwa baraka kwako. Kama ni hivyo, waweza kuniandikia? Mimi naelewa Kiingereza tu, hivyo itabidi kuniandikia kwa Kiingereza au barua yako itafsiriwe kwa Kiingereza kabla hujanitumia!
Njia hakika kabisa ya kunifikia ni kwa barua pepe, na anwani yangu ya barua pepe ni: contact us. Kama huwezi kutumia barua pepe, niandikie kwa anwani yangu ya huduma, ambayo ni: Shepherd Serve, P.O. Box 12854, Pittsburgh, PA 15241, U.S.A.
[1] Ndiyo maana Maandiko yanaseama, “Mpumbavu amesema moyoni mwake, Hakuna Mungu” (ktk Zaburi 14:1. Maneno mepesi kukazia). Wanaoweza kuzuia ukweli wazi kama huo ni wapumbavu tu.
[2] Zaidi ya hayo, Maandiko yanafundisha kwamba Mungu anaweza hata kufanya migumu mioyo ya wale wanaoendelea kuifanya migumu mioyo yao kinyume Chake (kama Farao vile). Hapo ni kwamba hakuna matumaini kwa watu aina hio kutubu.