Mada ya vita ya kiroho imezidi kupendwa sana katika kanisa la siku hizi. Kwa bahati mbaya sana, mengi yanayofundishwa kuhusu jambo hili yanapingana na Maandiko. Matokeo ni kwamba duniani kote, watumishi wengi wanafundisha na kutenda aina ya vita ya kiroho ambayo Biblia haisemi. Kwa kweli – kuna vita ya kiroho kimaandiko, na hiyo ndiyo itakiwayo kufanywa.
Katika sura hii na inayofuata, tutatazama baadhi ya mawazo ya makosa ambayo yamezoeleka sana kuhusu Shetani na vita ya kiroho. Sura hizi ni ufupisho wa kitabu kizima kuhusu jambo hili, kiitwacho Mawazo Ya Kisasa Juu Ya Vita Ya Kiroho.
Hekaya Ya Kwanza: “Katika milele iliyopita, Mungu na Shetani walipigana vita kubwa. Siku hizi, bado kuna mapambano kati yao.”
Hekaya hii inakwenda kinyume na kweli moja thabiti na ya msingi sana kuhusu Mungu, inayofunuliwa katika Maandiko – kwamba Yeye ana nguvu zote.
Yesu alituambia kwamba yote yanawezekana kwa Mungu (ona Mathayo 19:26). Yeremia alithibitisha kwamba hakuna kilicho kigumu kwa Mungu (ona Yeremia 32:17). Hakuna mtu wala nguvu viwezavyo kumzuia kufanya mapenzi Yake (ona 2Nyakati 20:6; Ayubu 41:10; 42:2). Mungu anauliza hivi kupitia kwa Yeremia, “Ni nani aliye kama Mimi … awezaye kusimama kinyume changu?” (Yeremia 50:44). Jibu ni kwamba, hakuna, hata Shetani hawezi.
Kama Mungu kweli ana nguvu zote kama inavyosemekana katika Maandiko yote hapo juu, basi kusema kwamba Mungu na Shetani walikuwa katika vita au wako katika vita ni kudai kwamba hana nguvu zote. Kama Mungu aliwahi kushindwa hata mara moja, au alishindwa kidogo tu na Shetani, au kama ilimbidi kukabiliana naye na kupambana hata kwa muda mfupi, basi Yeye hana nguvu zote kama anavyojitangaza.
Maelezo Ya Kristo Kuhusu Nguvu Za Shetani
Wakati mmoja Yesu alisema kitu kuhusu kuanguka kwa Shetani kutoka mbinguni kitakachotusaidia kuelewa nguvu alizo nazo, ukimlinganisha na Mungu wetu.
Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha wakisema, ‘Bwana! Hata pepo wanatutii kwa jina lako.’ Akawaambia, ‘Nilimwona Shetani akianguka kutoka mbinguni kama umeme’ (Luka 10:17, 18).
Wakati Mungu mwenye nguvu zote alipoagiza Shetani afukuzwe mbinguni, Shetani hakuwa na uwezo wowote wa kupinga. Yesu alichagua lugha ya mfano ili kueleza jinsi Shetani alivyoanguka haraka – kama umeme. Yaani, alianguka kutoka huko juu haraka sana. Sekunde moja alikuwa mbinguni, na iliyofuata – PWAA! – amekwisha ondoka!
Kama Mungu anaweza kumfukuza Shetani mwenyewe haraka hivyo na kirahisi hivyo, haipaswi kuwa kitu cha ajabu kwamba watumishi Wake aliowapa agizo wanaweza kuwafukuza mapepo haraka sana na kwa urahisi sana. Shida ni kwamba, kama wanafunzi wa kwanza wa Kristo, wengi katika Wakristo wanaheshimu sana nguvu ya Shetani na bado hawajatambua kwamba nguvu za Mungu ni kubwa sana, sana, sana. Mungu ndiye Mwumbaji – Shetani ni kiumbe tu. Shetani hamwezi Mungu.
Vita Ambayo Haikuwepo
Ingawa itasikika kama kitu cha ajabu masikioni kwetu, tunahitaji kuelewa kwamba Mungu na Shetani hawako katika vita, wala hawajawahi kuwepo, na hawatakuwa katika vita. Ni kweli kwamba wana makusudi na malengo tofauti, na ni kweli kusema kwambva wanapingana. Lakini, watu wawili wanapopingana, na mmoja awe na nguvu zaidi sana kuliko mwingine, upinzani wao hauwezi kuitwa vita. Je, mdudu anaweza kupigana na tembo? Shetani – sawa na mdudu – alifanya juhudi za kinyonge sana kumpinga Yule mwenye nguvu sana sana. Upinzani wake ulishughulikiwa haraka sana, naye alifukuzwa kutoka mbinguni “kama umeme”. Hapakuwa na vita hapo – ni mtu alifukuzwa.
Kama Mungu ana nguvu zote, Shetani hana nafasi hata ndogo tu ya kumzuia Mungu kufanya anachotaka. Na kama Mungu anamruhusu Shetani kufanya kitu, mwisho wake kitu hicho ni kwa ajili ya kutimiza mapenzi Yake kama Mungu. Kweli hii itawekwa wazi zaidi tunapoendelea kuchunguza Maandiko kuhusu mada hii.
Kufungwa Kwa Shetani Katika Siku Zijazo
Mamlaka makuu ya Mungu juu ya Shetani hayakuonyeshwa katika umilele uliopita tu, bali pia yataonyeshwa katika siku za baadaye. Tunasoma katika Ufunuo kwamba malaika mmoja tu atamshika Shetani na kumfunga kwa miaka elfu moja (ona Ufunuo 20:1-3). Tukio hilo la wakati ujao haliwezi kusemekana ni vita kati ya Mungu na Shetani. Ona pia kwamba Shetani hatakuwa na nguvu za kutoka gerezani humo, bali atafunguliwa wakati Mungu atakapotaka, na itakapokuwa sawa katika mapenzi Yake (ona Ufunuo 20:7-9).
Vipi Kuhusu “Vita Mbinguni” Ya Siku Zijazo?
Kama ni kweli kwamba Mungu na Shetani hawako vitani, na hawajawahi kuwepo, na hawatakuwa wakati wowote, mbona katika kitabu cha Ufunuo tunasoma kuhusu vita mbinguni hapo baadaye, ambayo Shetani anahusika (ona Ufunuo 12:7-9)? Hilo ni swali zuri, na ni rahisi kulijibu.
Ona kwamba vita hii itakuwa kati ya Mikaeli na malaika zake, na Shetani na malaika zake. Mungu hatajwi kuhusika katika vita hii. Kama angehusika, isingeitwa vita kwa sababu, Mungu, akiwa na nguvu zote, angeweza kufinya upinzani wa aina yoyote kwa muda mfupi sana tu, kama alivyothibitisha tayari.
Malaika – pamoja na Mikaeli – hawana nguvu zote, na ndiyo sababu vita yao na Shetani na malaika zake inaitwa vita kwa sababu kutakuwepo na mapambano kwa muda fulani. Lakini – kwa kuwa wao wana nguvu zaidi, watamshinda Shetani na majeshi yake.
Mbona Mungu asijihusishe na vita hii, na badala yake anawaachia malaika zake? Jibu si rahisi. Bila shaka, Mungu, akijua kila kitu, alijua kwamba malaika Zake wangeshinda vita hiyo, na pengine ndiyo maana aliona hakuna haja Yeye ajihusishe.
Bila shaka Mungu angewamaliza wale Wakanaani waovu upesi na kwa urahisi kabisa katika siku za Yoshua, lakini aliamua kuwapa Waisraeli kazi hio. Kitu ambacho Mungu angefanya bila shida yoyote kwa nukta chache, aliamua kuwaachia wafanye kwa muda mrefu, tena kwa juhudi nyingi sana. Pengine hilo lilikuwa linampendeza Mungu zaidi kwa sababu lilidai imani kwa Waisraeli. Pengine ndiyo sababu hatahusika katika ile vita ya wakati ujao huko mbinguni. Labda. Ila, Biblia haisemi.
Sasa – kwa kuwa itakuwepo vita mbinguni huko baadaye kati ya Mikaeli na malaika zake na Shetani na malaika zake, hiyo isiwe sababu ya kudhani kwamba Mungu hana nguvu zote – sawa tu na jinsi ambavyo vita za Israeli huko Kanaani zisiwe sababu ya kutufanya kufikiri kwamba Mungu hana nguvu zote.
Je, Shetani Hakushindwa Na Yesu Pale Msalabani?
Mwisho – kwa habari ya hii mada ya kwanza kwamba Mungu na Shetani wanapigana vita, tuhitimishe kwa kutazama usemi huu uliozoeleka sana: Yesu alimshinda Shetani pale msalabani. Maandiko hayasemi kwamba Yesu alimshinda Shetani msalabani.
Tunaposema kwamba Yesu alimshinda Shetani, ni kana kwamba Shetani na Yesu walikuwa katika vita, na hilo linaonyesha kwamba Mungu hana nguvu zote, na kwamba Shetani hayuko chini ya mamlaka ya Mungu tayari. Kuna njia za KiBiblia za kueleza mambo yaliyompata Shetani wakati Yesu alipotoa maisha Yake pale Kalvari. Kwa mfano: Maandiko yanatuambia kwamba kwa njia ya kifo Chake, Yesu “alimdhoofisha yeye aliyekuwa na nguvu za mauti” (ona Waebrania 2:14, 15).
Je, Yesu alimdhoofisha Shetani kwa kiwango gani? Ni wazi kwamba Shetani ana nguvu, vinginevyo mtume Yohana asingeandika hivi: “Dunia yote iko katika nguvu za yule mwovu” (1Yohana 5:19. Maneno mepesi kukazia). Kulingana na Waebrania 2:14, 15, Shetani alidhoofishwa kwa habari ya “nguvu za mauti”. Nini maana yake?
Maandiko yanataja aina tatu za mauti: mauti ya kiroho, mauti ya mwili, na mauti ya pili.
Kama tulivyokwisha jifunza mapema, mauti ya pili (au, kifo cha milele) inatajwa katika Ufunuo 2:22; 20:6, 14; 21:8, nayo huelezwa kwamba ni wakati ambapo waamini watatupwa katika ziwa la moto.
Mauti ya mwili hutokea wakati roho ya mtu inapotoka katika mwili wake, na mwili wake unaacha kufanya kazi.
Mauti ya kiroho hueleza hali ya roho ya mwanadamu ambaye hajazaliwa mara ya pili kwa njia ya Roho Mtakatifu. Mtu aliyekufa kiroho ana roho ambayo imetengwa na Mungu, roho yenye asili ya dhambi, roho ambayo, kwa kiwango fulani, imeungana na Shetani. Katika Waefeso 2:1-3 kuna picha kwa ajili yetu, ya mtu aliyekufa kiroho.
Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.
Paulo aliandika kwamba Wakristo wa Efeso walikuwa wafu katika makosa na dhambi zao. Hakuwa anasema juu ya mauti ya mwili kwa sababu alikuwa anawaandikia watu walio hai. Basi, alikuwa anasema kwamba wamekufa, kwa jinsi ya kiroho.
Nini kilichowaua kiroho? Ni “makosa na dhambi zao”. Kumbuka Mungu alikuwa amemwambia Adamukwamba siku atakayoacha kutii, angekufa (ona Mwanzo 2:17). Mungu hakuwa anasema juu ya kifo cha kimwili bali cha kiroho, kwa sababu Adamu hakufa kimwili siku alipokula lile tunda alilokatazwa. Ila, alikufa kiroho siku hiyo, na hakufa kimwili mpaka miaka mia nyingi baadaye.
Paulo akaendelea kusema kwamba Waefeso hao, kama wafu kiroho, walikuwa wakienenda kulingana na makosa hayo na dhambi hizo, wakifuata “mtindo wa dunia” (yaani, wakifanya yote yaliyokuwa yanafanywa na kila mtu) na kumfuata “mfalme wa uwezo wa anga”.
Huyo “mfalme wa uwezo wa anga” ni nani? Ni Shetani, anayetawala ufalme wake wa giza kama amiri jeshi mkuu anayesimamia majeshi ya pepo wabaya wanaokaa angani. Hizo pepo chafu zinaorodheshwa kulingana na vyeo katika sura mojawapo ya Waefeso (ona Waefeso 6:12).
Paulo akasema kwamba huyo mfalme wa giza ni “roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi”. Maneno “wana wa kuasi” ni jina lingine tu la wasioamini wote, lenye kukazia kwamba asili yao ni ya dhambi. Baadaye Paulo anawataja kwamba “kwa tabia ni watoto wa hasira” (Waefeso 2:3. Maneno mepesi kukazia). Tena akaongezea na kusema kwamba Shetani alikuwa anafanya kazi ndani yao.
Shetani Kama Baba
Kama watu ambao hawajaokoka wanajua au hawajui, ni kwamba wao wanamfuata Shetani, na ni watu wake katika ufalme wa giza. Wana asili yake ovu na ya kibinafsi ndani ya roho zao zilizokwisha kufa. Ukweli ni kwamba Shetani ni bwana wao kiroho, na baba yao. Ndiyo sababu wakati mmoja Yesu aliwaambia viongozi wa dini ambao hawajaokoka, hivi: “Ninyi ni wa baba yenu Ibilisi, ndiyo maana mnataka kufanya mapenzi yake” (Yohana 8:44).
Hiyo ndiyo picha mbaya ya mtu ambaye hajazaliwa mara ya pili! Anaishi akiwa amekufa kiroho, akiwa amejawa na asili ya Shetani, akiwa anakwenda kwenye mauti ya mwili isiyoepukika anayoiogopa sana, na, atambue au asitambue, siku moja atapatikana na mauti mbaya zaidi sana – mauti ya milele – atakapotupwa katika ziwa la moto.
Ni muhimu sana tuelewe kwamba mauti ya kiroho, kimwili na milele ni madhihirisho ya hasira ya Mungu juu ya mwanadamu mwenye dhambi, na kwamba Shetani anahusika katika kila moja. Shetani ameruhusiwa na Mungu atawale ufalme wa giza na wote wenye “kulipenda giza” (Yohana 3:19). Yaani, ni kama Mungu alimwambia Shetani hivi: “Wewe watawale kwa nguvu zako wale wote ambao hawaninyenyekei mimi.” Shetani akawa chombo cha ghadhabu ya Mungu juu ya wanadamu waasi. Kwa kuwa wote wamefanya dhambi, wote wako chini ya nguvu za Shetani, wakijaa asili yake katika roho zao na kushikwa mateka ili kufanya mapenzi yake (ona 2Timo. 2:26).
Malipo Kwa Ajili Ya Kutekwa Kwetu
Lakini, tunaweza kumshukuru Mungu kwamba alikuwa na rehema juu ya binadamu, na kwa sababu ya huruma Zake, hakuna anayetakiwa kubaki katika hali hiyo mbaya. Kwa kuwa kifo cha Yesu badala yetu kilitosheleza madai ya haki ya Mungu, wale wote wanaomwamini Kristo wanaweza kuepukana na kifo cha kiroho na uteka wa Shetani kwa sababu hawako tena chini ya hasira ya Mungu. Tunapomwamini Yesu Kristo, Roho Mtakatifu huingia katika roho zetu na kufutilia mbali asili ya Shetani, na kuifanya roho zetu kuzaliwa mara ya pili (ona Yohana 3:1-16) na kuturuhusu kuwa washiriki wa asili ya Mungu (ona 2Petro 1:4).
Turudie swali tuliloanza nalo. Wakati mwandishi wa Waebrania anaposema kwamba Yesu, kwa njia ya kifo Chake, “alimdhoofisha yeye aliyekuwa na nguvu ya mauti, yaani Shetani” maana yake ni kwamba nguvu ya mauti ya kiroho, ambayo Shetani anayo juu ya kila mtu asiyeokoka, imevunjwa kwa wote walio “katika Kristo”. Sisi tunahuishwa kiroho kwa sababu ya Kristo; amekwisha lipa adhabu kwa ajili ya dhambi zetu.
Tena – kwa kuwa sisi hatujafa kiroho tena na hatuko tena chini ya utawala wa Shetani, hatuna haja ya kuogopa mauti ya mwili, kwa sababu tunajua kinachotungojea mbele – urithi wa utukufu mwingi, wa milele.
Mwisho – kwa sababu ya Yesu, tumekombolewa na mauti ya pili, yaani, kutupwa katika ziwa la moto.
Je, Yesu alimshinda Shetani pale msalabani? Hapana, kwa sababu hapakuwepo vita kati ya Yesu na Shetani. Ila, yesu alimdhoofisha Shetani kwa habari ya nguvu zake juu ya mauti ya kiroho, ambayo kwa hiyo anawashikilia wasio-okoka katika utumwa wa dhambi. Shetani bado ana nguvu za mauti ya kiroho juu ya watu ambao hawajaokoka, ila kwa habari ya wale walio katika Kristo, hana nguvu zozote juu yao!
Kuvuliwa Kwa Enzi Na Mamlaka
Hili pia linatusaidia kuelewa maana ya maneno ya Paulo, kwamba “enzi na mamlaka zilivuliwa uwezo wake” katika Wakolosai 2:13-15.
Na ninyi mliokuwa mmekufa [kiroho] kwa sababu ya makosa yenu …. Aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote; akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo (maneno mepesi kukazia).
Paulo anatumia lugha ya mfano, yenye kueleweka kirahisi, katika fungu hili. Katika sehemu ya kwanza, analinganisha hatia yetu na “hati ya madai”. Kile ambacho sisi hatukuweza kulipa tulilipiwa na Kristo, aliyechukua deni letu la dhambi mpaka msalabani.
Katika sehemu ya pili, kama ambavyo wafalme wa kale walivyokuwa wanawavua silaha wale waliokuwa wamewashinda vitani na kuwatembeza kwa ushindi katika mitaa ya miji yao, kifo cha Kristo kilikuwa ushindi juu ya “falme, enzi na mamlaka,” yaani, majeshi ya mapepo wa ngazi za chini ambao hutawala wanadamu waasi, na kuwashika mateka.
Sasa – kutokana na fungu hili, hatuwezi kusema kwamba Kristo alimshinda Shetani? Labda, lakini kwa kuongeza maelezo. Inatupasa kukumbuka kwamba, katika fungu hili, Paulo alikuwa anaandika kwa lugha ya mfano. Na kila mfano una mahali ambapo mlinganisho hubadilika na kupingana, kama tulivyojifunza katika sura juu ya kutafsiri maandiko.
Katika kutafsiri mifano ya Paulo katika Wakolosai 2:13-15, lazima tuwe makini. Ni wazi kwamba hapakuwepo na “hati ya mashtaka” iliyokuwa imeandikwa dhambi zetu zote, iliyogongomewa pale msalabani. Ila, ni mfano wa yale ambayo Yesu alifanikisha.
Vivyo hivyo, mapepo waliotawala wanadamu ambao hawajaokoka hawakunyang’anywa panga zao na ngao zao na kutembezwa na Yesu hadharani barabarani. Lugha anayotumia Paulo ni ya mfano tu kuonyesha kile ambacho Yesu alifanikisha kwa ajili yetu. Tulikuwa mateka wa pepo hizo. Lakini, kwa kufa kwa ajili ya dhambi zetu, Yesu alitufungua kutoka uteka wetu. Si kwamba alipambana ana kwa ana na hao pepo wabaya, wala hawakuwa vitani Naye. Wao, kwa kuruhusiwa na haki ya Mungu, walikuwa ametutawala kwa nguvu zao maisha yetu yote. “Silaha” zao hazikuwa zime-elekezwa kwa Kristo, bali kwetu. Lakini, Yesu “aliwanyang’anya silaha” zao. Hawana uwezo wa kutushika mateka tena.
Tusije tukafikiri kwamba kulikuwepo na vita ya miaka na miaka kati ya Yesu na mapepo wa Shetani, na hatimaye Yesu akashinda vita hiyo pale msalabani. Tukisema kwamba Yesu alimshinda Shetani, ni vizuri tuelewe kwamba alimshind Shetani kwa ajili yetu, si kwa ajili Yake Mwenyewe.
Wakati fulani nilifukuza mbwa mdogo aliyekuwa anamtishia binti yangu. Naweza kusema kwamba nilimshinda huyo mbwa, lakini usidhani kwamba huyo mbwa alikuwa kitisho kwangu. Alikuwa anamtishia binti yangu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Yesu na Shetani. Yesu alimfukuza mbwa aliyekuwa anatutishia sisi, si Yeye.
Alimfukuzaje huyo Shetani mbwa? Alifanya hivyo kwa kuchukua adhabu za dhambi zetu, na kwa njia hiyo kutuweka huru kutokana na hatia yetu mbele za Mungu. Kwa kufanya hivyo, alituweka huru kutokana na hasira ya Mungu, na hivyo, wale pepo wachafu ambao Mungu anawaruhusu kwa haki kabisa kuwatawala wanadamu waasi hawakuwa na haki tena ya kututawala sisi. Mungu asifiwe kwa hilo!
Tunafikia mahali panapofaa, kutazama hekaya ya pili.
Hekaya Ya Pili: “Zipo vita zinazoendelea katika ulimwengu wa roho, kati ya malaika wa Mungu na wa Shetani. Matokeo ya vita hizo hutegemeana na jinsi sisi tunavyopigana vita kiroho.”
Tayari tumejifunza kutoka kitabu cha Ufunuo kwamba siku moja itakuwepo vita mbinguni kati ya Mikaeli na malaika zake, na Shetani na malaika zake. Zaidi ya hapo, kuna vita nyingine moja kati ya malaika inayotajwa katika Maandiko, katika Danieli sura ya kumi.[1]
Danieli anatuambia alikuwa akiomboleza kwa majuma matatu katika mwaka wa tatu wa utawala wake Koreshi, mfalme wa Uajemi. Mara malaika akamtokea kando ya Mto Tigris. Kusudi la safari ya malaika lilikuwa kumpa yeye ufahamu juu ya wakati ujao wa taifa la Israeli, na tayari tumetazama kwa kifupi yale ambayo Danieli aliambiwa kuhusu Unyakuo na Nyakati za Mwisho katika sura iliyotangulia. Katika mazungumzo yao, malaika huyo ambaye hatajwi jina alimwambia Danieli hivi:
Usiogope, Danieli; kwa maana tangu siku ile ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno yako yalisikiwa; nami nimekuja kwa ajili ya maneno yako. Lakini mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja; bali, tazama, huyo Mikaeli, mmoja wa hao wakuu wa mbele, akaja kunisaidia; nami nikamwacha huko pamoja na wafalme wa Uajemi (Danieli 10:12, 13. Maneno mepesi kukazia).
Danieli akajua kwamba maombi yake yalikwisha sikiwa majuma matatu kabla ya kukutana na huyo malaika, lakini pia akajua kwamba malaika mwenyewe ametumia majuma matatu kumfikia. Sababu ya kuchelewa kwa malaika ni kwamba, “mkuu wa ufalme wa Uajemi” alimpinga. Ila, alifanikiwa kupenya wakati Mikaeli, “mmoja wa hao wakuu wa mbele” alipofika kumsaidia.
Alipokaribia kuondoka, malaika alimwambia Danieli hivi:
Na sasa nitarudi ili nipigane na mkuu wa Uajemi; nami nitakapotoka huku, tazama, mkuu wa Uyunani atakuja. Lakini nitakuambia yaliyoandikwa katika maandiko ya kweli; wala hapana anisaidiaye juu ya hao ila huyo Mikaeli, mkuu wenu (Danieli 10:20, 21).
Zipo kweli kadhaa za kusisimua zipatikanazo katika fungu hili. Hapa tena tunaona kwamba malaika wa Mungu hawana nguvu zote, na wanaweza kuingia katika mapigano na malaika waovu.
Pili tunajifunza kwamba malaika wengine (kama vile Mikaeli) wana nguvu zaidi kuliko wengine (kama huyo aliyezungumza na Danieli).
Maswali Tusiyokuwa Na Majibu Yake
Tunaweza kuuliza hivi: “Kwa nini Mungu hakumtuma Mikaeli kupeleka huo ujumbe kwa Danieli moja kwa moja, ili kusiwe na kuchelewa kwa majuma matatu?” Ukweli ni kwamba Biblia haituambii sababu za Mungu kumtuma malaika ambaye alijua kabisa asingeweza kumpita “mkuu wa ufalme wa Uajemi” bila kusaidiwa na Mikaeli. Ukweli ni kwamba hatujui ni kwa nini Mungu atumie malaika yeyote ili kupeleka ujumbe kwa mtu! Mbona hakwenda Mwenyewe, au kusema na Danieli kwa sauti, au kumfikisha Danieli mbinguni kwa muda tu ili amwambie? Hatujui!
Sasa je! Maandiko haya yanathibitisha kwamba kuna vita za mara kwa mara katika ulimwengu wa roho kati ya malaika wa Mungu na wa Shetani? Hapana. Maandiko haya yanathibitisha tu kwamba, miaka elfu kadhaa iliyopita, kulikuwa na mapambano ya majuma matatu kati ya malaika moja dhaifu wa Mungu, na malaika mmoja mwenye nguvu wa Shetani, aitwaye “mkuu wa ufalme wa Uajemi.” Vita hiyo, kama Mungu angetaka, isingetokea kamwe. Vita nyingine ya malaika inayotajwa katika Biblia ni ile ya wakati ujao huko mbinguni, iliyoandikwa katika Kitabu cha Ufunuo. Basi. Pengine zimekuwepo vita zingine za malaika zilizotokea, lakini tukiamua hivyo tutakuwa tunakisia tu – hatuna ushahidi.
Hekaya Iliyojengwa Juu Ya Hekaya
Je, hii habari ya Danieli na mkuu wa ufalme wa Uajemi inathibitisha kwamba vita yetu ya kiroho inaweza kuamua matokeo ya vita za malaika? Hapa tena, wazo hili linadhania (kutokana na maandiko machache sana) kwamba zipo vita mara kwa mara kati ya malaika. Hebu tukisie tu na kukubali kwamba ndiyo, zipo vita za malaika mara kwa mara. Je, habari hii kuhusu Danieli inathibitisha kwamba vita yetu ya kiroho inaweza kuamua matokeo ya vita za malaika ambazo pengine zinakuwepo?
Mara nyingi, watu wenye kusambaza mawazo haya huuliza swali hili: “Ingekuwaje kama Danieli angekata tamaa baada ya siku moja?” Swali hilo halina jibu kutoka kwa yeyote, maana Danieli hakuacha kumtafuta Mungu katika maombi mpaka huyo malaika asiyejulikana alipofika. Ila, sababu ya kuliuliza ni kutushawishi tuamini kwamba, Danieli, kwa kuendelea katika vita ya kiroho, alikuwa funguo ya ushindi katika vita ya huyo malaika asiyetajwa jina. Kama Danieli angekata tamaa na kuacha kupambana kiroho, inadaiwa kwmaba huyo malaika asingempita yule mkuu wa ufalme wa Uajemi. Wanataka tuamini kwamba hata sisi, kama Danieli, lazima tudumu katika vita ya kiroho, la sivyo malaika fulani mwovu atawashinda malaika wema wa Mungu.
Sawa, lakini – Ni vizuri kwanza tujue kwamba Danieli hakuwa “kwenye vita ya kiroho” – yeye alikuwa anamwomba Mungu. Hatusomi popote kwamba alisema kitu kinyume cha mapepo, au kwamba aliwafunga, au kwamba “alipigana” nao. Ukweli ni kwamba, Danieli hakujua kwamba kulikuwa na vita baina ya malaika mpaka baada ya majuma matatu kupita, na yule malaika asiyetajwa jina kumtokea. Yeye alitumia majuma hayo matatu katika kufunga na kumtafuta Mungu.
Basi tuliseme swali hilo kwa namna nyingine: Kama Danieli angeacha kuomba na kumtafuta Mungu baada ya siku moja au mbili, je, huyo malaika asiyetajwa jina angeshindwa kumfikishia ujumbe wa Mungu? Hatujui, ila ni vizuri kusema kwamba yule malaika asiyetajwa jina hakumwambia Danieli hivi: “Ni vizuri uliendelea kuomba maana kama si hivyo, nisingefanikiwa.” Hapana! Malaika alimsifu Mikaeli kwa kufanikiwa kwake. Bila shaka Mungu ndiye aliyemtuma malaika huyo asiyetajwa jina, pamoja na Mikaeli, Naye aliwatuma kama itikio la maombi ya Danieli kutaka kuelewa mambo ambayo yangetokea katika siku zijazo za Israeli.
Ni mawazo tu kudhani kwamba kama Danieli angeacha kufunga au kumtafuta Mungu, Mungu angesema hivi: “Haya! Ninyi malaika wawili, Danieli ameacha kufunga na kuomba. Kwa hiyo, ingawa nilimtuma mmoja wenu kumpelekea ujumbe siku ile ya kwanza alipoanza maombi, achaneni na huo ujumbe. Kitabu chake hakitakuwa na sura ya kumi na moja wala ya kumi na mbili.”
Hakika Danieli alidumu katika maombi (si katika “vita ya kiroho”), na Mungu alimwitikia kwa kutuma malaika. Sisi nasi tunapaswa kudumu katika kumwomba Mungu, na kama Mungu atapenda, jibu letu linaweza kuja kwa njia ya malaika. Lakini usisahau kwamba kuna mifano mingi sana ya malaika kupeleka jumbe muhimu sana kwa watu katika Biblia, ambapo hapataji hata sala moja ya mtu yeyote, licha ya kuomba majuma matatu.[2] Tuwe na msimamo. Tena, kuna mifano mingi sana ya malaika kuwapa watu jumbe, na katika mifano hiyo hakuna kutajwa kwamba ilibidi wapambane na mapepo walipokuwa wanatoka mbinguni. Labda hao malaika walipambana na mapepo ili kuweza kufikisha jumbe zao, lakini kama ilikuwa hivyo, hatuna habari, maana Biblia haisemi.
Tunafikia kwenye hekaya ya tatu, inayoaminika sana.
Hekaya Ya Tatu: “Adamu Alipoanguka, Shetani Alipata Haki Ya Adamu Kutawala Ulimwengu.”
Je, ni kitu gani kilichotokea kwa Shetani wakati binadamu walipoanguka? Kuna
wanaodhani kwamba Shetani alipata cheo kikubwa sana Adamu alipoanguka. Wanasema mwanzoni Adamu alikuwa ndiye “mungu wa dunia hii,” lakini alipoanguka, Shetani akapata cheo hicho na kuwa na haki ya kufanya chochote alichotaka hapa duniani. Hata Mungu hakuweza kumzuia kuanzia wakati huo na kuendelea, kwa sababu Adamu alikuwa na ”haki kisheria” kumpa Shetani cheo chake na nafasi yake, na Mungu ilibidi aheshimu makubaliano kati Yake na Adamu, ambayo sasa yalikuwa kwa Shetani. Inasemekana kwamba sasa hivi Shetani ndiye mwenye “hati miliki ya Adamu”, na Mungu hawezi kumzuia kitu Shetani mpaka “hati miliki ya Adamu itakapofikia mwisho wake”.
Tunauliza hivi: Je, nadharia hiyo ni kweli? Je, Shetani alipata “hati miliki ya Adamu” wakati binadamu walipoanguka? Jibu ni HAPANA KABISA! Shetani hakupata chochote wakati binadamu walipoanguka isipokuwa laana kutoka kwa Mungu, na ahadi kuhusu kuangamizwa kwake kabisa.
Ukweli ni kwamba Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa ndiye “mungu wa dunia hii”. Tena, Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa na haki kisheria ya kumpa mtu mwingine mamlaka anayodhaniwa kuwa nayo juu ya dunia. Tena, Biblia haisemi kwamba Adamu alikuwa na hati miliki ambayo siku moja ingefikia mwisho. Mawazo hayo yote si ya KiBiblia.
Sasa basi: Adamu alikuwa na mamlaka gani? Tunasoma katika Mwanzo kwamba Mungu alimwambia Adamu na Hawa hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi” (Mwanzo 1:28. Maneno mepesi kukazia).
Mungu hakusema chochote kwa Adamu juu ya kuwa “mungu” duniani, au kwamba angeweza kutawala kila kitu, kama vile hali ya hewa na watu wote ambao wangezaliwa baadaye na kadhalika. Yeye alimpa Adamu na Hawa kama binadamu wa kwanza, utawala juu ya samaki, ndege na wanyama, na kuwaagiza waijaze dunia na kuitiisha.
Wakati Mungu alipotamka hukumu kwa mwanadamu, hakusema chochote kuhusu Adamu kupoteza inayodhaniwa kuwa nafasi yake kama “mungu wa dunia hii.” Tena, hakusema chochote kwa Adamu na Hawa kuhusu wao kutokuwa na mamlaka tena juu ya samaki, ndege na wanyama. Ni dhahiri kwamba bado binadamu wanatawala juu ya samaki na ndege na “kila kiendacho juu ya nchi”. Binadamu bado wanaijaza dunia na kuitiisha. Wakati wa kuanguka binadamu, Adamu hakupoteza mamlaka yake aliyopewa na Mungu.
Je, Shetani Si “Mungu Wa Dunia Hii”?
Lakini, mbona Paulo anamtaja Shetani kuwa “mungu wa dunia hii,” na Yesu kumtaja kuwa “mkuu wa dunia hii”? Ndiyo, lakini hakuna aliyesema kwamba Adamu aliwahi kuwa “mungu wa dunia hii” au kwamba Shetani alipata cheo hicho kutoka kwa Adamu, alipoanguka.
Tena, jina hilo la Shetani kwamba ni “mungu wa dunia hii” halithibitishi kwamba Shetani anaweza kufanya chochote atakacho hapa duniani, au kwamba Mungu hana uwezo wa kumzuia. Yesu alisema hivi: “Nimepwa mamlaka yote mbinguni na duniani” (Mathayo 28:18. Maneno mepesi kukazia). Kama Yesu ana mamlaka yote duniani, ni kwamba Shetani anaweza kutenda kazi kwa ruhusa Yake tu.
Nani aliyempa Yesu mamlaka yote mbinguni na duniani? Bila shaka ni Mungu Baba, ambaye alikuwa nayo Mwenyewe, ili ampe Yesu. Ndiyo sababu Yesu alisema juu ya Baba yake kwamba ni “Bwana wa mbingu na dunia” (Mathayo 11:25; Luka 10:21. Maneno mepesi kukazia). Mungu amekuwa na mamlaka yote duniani tangu alipoiumba. Alitoa mamlaka kidogo kwa binadamu mwanzoni, na hawajawahi kupoteza kile alichokitoa Mungu.
Biblia inaposema juu ya Shetani kuwa mungu au mtawala au mkuu wa dunia hii, maana yake hasa ni kwamba watu wa dunia (yaani, ambao hawajazaliwa mara ya pili) wanamfuata Shetani. Yeye ndiye wanayemtumikia, wajue au wasijue. Yeye ni mungu wao.
Je, Shetani Alifanya Toleo Lolote?
Nadharia hiyo ya Shetani kupata utawala imejengwa kwenye hadithi ya kujaribiwa kwa Yesu huko nyikani na Shetani, kama ilivyoandikwa katika Mathayo na Luka. Hebu tuchunguze maelezo atoayo Luka ili tuone tunachoweza kujifunza.
[Shetani] Akampandisha juu, akamwonyesha miliko zote za ulimwengu kwa dakika moja. Ibilisi akamwambia, ‘Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa yeyote kama nipendavyo. Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako.’ Yesu akajibu akamwambia, ‘Imeandikwa: Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake’ (Luka 4:5-8).
Je, tukio hili linathibitisha kwamba Shetani ana mamlaka juu ya kila kitu duniani, au kwamba Adamu alimpa kila kitu, au kwamba Mungu hana uwezo wa kumzuia? Hapana, na sababu zinafuata.
Kwanza: Tuwe makini sana kuhusu kujenga itikadi juu ya tamko lililofanywa na mtu ambaye Yesu anamwita “baba wa uongo” (Yohana 8:44). Wakati mwingine Shetani husema ukweli, lakini kat ika swala hili, tunapaswa kuwa macho kwa sababu kile alichosema Shetani kinapingana na kitu ambacho kilikwisha semwa na Mungu.
Katika sura ya nne ya kitabu cha Danieli, tunapata hadithi ya kunyenyekezwa kwa mfalme Nebukadneza. Huyu mfalme, akiwa amejaa kiburi juu ya cheo chake na nafasi yake na mafanikio yake, aliambiwa na nabii Danieli kwamba angepewa akili ya mnyama mpaka atakapotambua kwamba “Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa yeye amtakaye, awaye yote” (Danieli 4:25. Maneno mepesi kukazia). Tamko hilo linatolewa mara nne katika habari hii, kutilia mkazo umuhimu wake (tazama 4:17, 25, 32; 5:21).
Ona kwamba Danieli alisema hivi: “Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu.” Hiyo inaonyesha kwamba Mungu ana mamlaka kiasi fulani juu ya dunia, sivyo?
Ona vile vile kwamba anachosema Danieli ni kinyume kabisa na kile ambacho Shetani alimwambia Yesu. Danieli anasema “naye humpa yeye amtakaye, awaye yote”. Shetani akasema, “nami humpa yeyote, kama nipendavyo” (Luka 4:6).
Sasa, wewe utamwamini nani? Mimi nimeamua kumwamini Danieli.
Lakini – kuna uwezekano kwamba Shetani alikuwa anasema ukweli – tukitazama alichosema kutoka upande mwingine.
Shetani ni “mungu wa dunia hii” kama tulivyokwisha ona. Maana yake ni kwamba anatawala ufalme wa giza, ambao ni pamoja na watu katika kila taifa waliomwasi Mungu. Biblia inasema hivi: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu” (1Yohana 5:19). Wakati Shetani alipodai kwamba angeweza kumpa yeyote apendaye mamlaka juu ya falme za dunia, yawezekana alikuwa anazungumza juu ya enzi yake mwenyewe, yaani ufalme wa giza, ambayo inaundwa na falme ndogo ndogo ambazo zinakubaliana kwa sehemu na falme za duniani kijiografia. Tunajulishwa na Maandiko kwamba Shetani ana ngazi kadhaa za vyeo miongoni mwa pepo wake wabaya, ambazo kupitia hizo anatawala ufalme wake (ona Waefeso 6:12), na ni sawa tukikisia kwamba yeye ndiye mwenye kuwapandisha au kuwashusha vyeo hao pepo katika ngazi zao, maana ndiye mkuu. Kwa hali hiyo, Shetani alikuwa anampa Yesu kihalali kabisa nafasi ya kuwa pepo msaidizi, ili amsaidie kutawala katika ufalme wake wa giza. Kitu alichopaswa kufanya Yesu ni kumsujudia Shetani na kumwabudu. Shukuru kwa sababu Yesu hakukubaliana na nafasi hiyo ya “kupanda cheo”!
Nani Aliyempa Shetani Cheo Chake?
Sasa: Vipi kuhusu madai ya Shetani kwamba mamlaka juu ya falme hizo amepewa yeye?
Hapa tena lazima tujue kuna uwezekano mkubwa tu kwamba alikuwa anadanganya. Lakini hebu tuseme alikuwa anasema ukweli, tuone.
Ona kwamba Shetani hakusema Adamu ndiye alimpa mamlaka hayo. Kama tulivyokwisha ona mapema, Adamu asingeweza kuwa alimpa Shetani kwa sababu hakuwa na kitu cha kutoa. Adamu alitawala samaki, ndege na wanyama, si falme. (Ukweli ni kwamba wakati Adamu anaanguka, hakukuwepo falme za watu za kutawala.) Tena, kama Shetani alikuwa anampa Yesu utawala juu ya ufalme wa giza, ambao ni mapepo wote na watu ambao hawajaokoka, isingewezekana kabisa kwamba Adamu ndiye alimpa Shetani ufalme huo. Shetani alikuwa anatawala malaika walioanguka kabla Adamu hajaumbwa.
Yawezekana Shetani alimaanisha kwamba watu wote wa duniani walimpa yeye mamlaka juu yao, maana hawakujitolea kwa Mungu na kwa njia hiyo, kwa kujua au pasipo kujua, walikuwa wamejitolea kwake yeye.
Uwezekano bora zaidi ni kwamba Mungu ndiye alimpa mamlaka hayo. Inawezekana kabisa, kutokana na Maandiko, kwamba Mungu alimwambia Shetani, “Wewe na pepo wako waovu mna ruhusa Yangu kutawala juu ya kila mtu ambaye hajajitolea kwangu.” Unaweza kushindwa kulipokea hilo, lakini baadaye utaona kwamba pengine hayo ndiyo maelezo bora zaidi ya madai aliyotoa Shetani. Kama kweli Mungu ni “mtawala juu ya wanadamu wote” (Danieli 4:25), basi mamlaka yoyote ambayo Shetani anayo lazima awe alipewa na Mungu.
Shetani anatawala ufalme wa giza tu, ambao pia unaweza kuitwa “ufalme wa uasi.” Yeye alikuwa anatawala ufalme huo tangu siku ile alipofukuzwa mbinguni, kitu kilichotokea kabla ya kuanguka kwa Adamu. Mpaka wakati Adamu alipoanguka, ufalme wa giza ulikuwa na malaika waasi tu. Lakini wakati Adamu alipotenda dhambi, yeye naye akajiunga katika kundi la waasi, na ufalme wa Shetani tangu hapo ukawa na binadamu waasi, pamoja na malaika waasi.
Shetani alikuwa anatawala juu ya ufalme wake wa giza kabla hata Adamu hajaumbwa. Basi, tusije tukafikiri kwamba Adamu alipoanguka, Shetani alipata kitu ambacho Adamu alikuwa nacho. Hapana. Wakati Adamu alipotenda dhambi, alijiunga ufalme wa uasi ambao ulikuwepo kwa muda mrefu tu – ufalme uliotawaliwa na Shetani.
Je, Mungu Alishtushwa Na Anguko?
Hitilafu nyingine katika nadharia kwamba “Shetani Alifaidika” ni kwamba, inamfanya Mungu aonekane mpumbavu, kana kwamba alishtukizwa na matukio ya anguko, na kwa sababu hiyo, akajikuta katika hali ya kusikitisha. Je, Mungu hakujua kwamba Shetani angewajaribu Adamu na Hawa na kwamba binadamu wangeanguka kwa sababu hiyo? Ikiwa Mungu anajua yote – na ni kweli anajua yote – basi alikuwa anajua yatakayotokea. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kwamba alifanya mipango ya kukomboa wanadamu hata kabla ya kuwaumba (ona Mathayo 25:34; Matendo 2:2-23; 4:27, 28; 1Wakor. 2:7,8; Waefeso 3:8-11; 2Timo. 1:8-10; Ufunuo 13:8).
Mungualimwumba Shetani akijua ataanguka, na alimwumba Adamu na Hawa akijua wataanguka. Hakuna jinsi ambavyo Shetani angeweza kumdanganya Mungu na kupata kitu ambacho Mungu hakutaka awe nacho.
Je, maana yake ni kwamba Mungu anataka Shetani awe “mungu wa dunia hii?” Ndiyo, kwa muda wote ambao itatimiza makusudi Yake. Kama Mungu asingemtaka
Shetani afanye kazi, angemzuia tu mara moja kama atakavyofanya wakati mmoja, katika Ufunuo 20:1, 2.
Lakini, si kwamba Mungu anataka yeyote abaki chini ya utawala wa Shetani. Mungu anamtaka kila mmoja aokolewe na kuepukana na utawala wa Shetani (Matendo 26:18; Wakolosai 1:13; 1Timo. 2:3, 4; 2Petro 3:9). Lakini Mungu anamruhusu Shetani kutawala kila mtu anayependa giza (ona Yohana 3:19) – yaani, wale wote wanaoendelea kuwa kinyume Chake.
Je, hakuna chochote tunachoweza kufanya ili kuwasaidia watu waepukane na ufalme wa Shetani wa giza? Kipo. Tunaweza kuwaombea na kuwaita watubu na kuiamini Injili (kama tulivyoagizwa na Yesu). Wakifanya hivyo, watawekwa huru kutoka mamlaka ya Shetani. Lakini kudhani kwamba tunaweza “kuangusha” pepo wabaya wanaowashikilia watu ni makosa. Kama watu wanataka kukaa gizani, Mungu atawaruhusu. Yesu aliwaambia wanafunzi Wake kwamba kama watu katika miji fulani wasingepokea ujumbe wao, wakung’ute mavumbi ya miguu yao na kwenda mji mwingine (Mathayo 10:14). Hakuwaambia wakae na kuangusha ngome juu ya mji huo ili watu waweze kupokea zaidi. Mungu huruhusu pepo wabaya kuwafunga watu wanaokataa kutubu na kumrudia Yeye.
Ushahidi Zaidi Kuhusu Mamlaka Ya Mungu Juu Ya Shetani
Yapo maandiko mengine mengi yenye kuthibitisha vizuri sana kwamba Mungu hakupoteza mamlaka yoyote juu ya Shetani wakati mwanadamu alipoanguka. Biblia mara kwa mara inatuambia kwamba Mungu siku zote ana mamlaka juu ya Shetani, na atakuwa nayo. Shetani anaweza kufanya kile anachoruhusiwa kufanya na Mungu tu. Hebu tutazame kwanza mifano kadhaa kutoka Agano la Kale juu ya jambo hili.
Sura mbili za kwanza za kitabu cha Ayubu zinaeleza mfano wa mamlaka ya Mungu juu ya Shetani. Hapo tunasoma kuhusu Shetani mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, akimshtaki Ayubu. Ayubu alikuwa mtiifu kwa Mungu kuliko mtu mwingine yeyote duniani wakati huo. Basi, Shetani akamtafuta sana. Mungu alijua kwamba Shetani “ameweka moyo wake” juu ya Ayubu (1:8). Basi, alimsikiliza Shetani alipomshtaki kwa kumtumikia Mungu tu kwa sababu ya baraka zote ambazo alikuwa anazifurahia (ona Ayubu 1:9-12).
Shetani alisema Mungu alikuwa ameweka uzio kumzunguka Ayubu, na akamwomba aondoe baraka za Ayubu. Basi, Mungu alimruhusu Shetani kumtesa Ayubu kwa kiwango fulani. Mwanzoni, hakuruhusiwa kugusa mwili wa Ayubu, ila baadaye, Mungu alimruhusu Shetani kuutesa mwili wake. Lakini alimkataza kumwua (Ayubu 2:5, 6).
Fungu hili moja la Maandiko hakika linathibitisha kwamba Shetani hawezi kufanya chochote anachotaka. Hakuweza kugusa mali za Ayubu mpaka Mungu alipomruhusu. Hakuweza kuiba afya ya Ayubu mpaka Mungu alipomruhusu. Na hakuweza kumwua Ayubu kwa sababu Mungu alimkataza.[3] Ni hivi: Mungu anamtawala Shetani kikamilifu, hata tangu wakati wa anguko la Adamu.
Roho Mbaya Ya Sauli, “Kutoka Kwa Bwana”
Kuna mifano mingi ya Mungu akiwatumia pepo wabaya wa Shetani kama mawakala wa ghadhabu Yake katika Agano la Kale. Tunasoma hivi katika 1Samweli 16:14 – “Basi roho ya BWANA ilikuwa imemwacha Sauli, na roho mbaya kutoka kwa BWANA ikamsumbua.” Hali hii bila shaka ilitokea kwa sababu ya adhabu ya Mungu juu ya Sauli mfalme, aliyeacha kumtii Mungu.
Swali kubwa ni hili: Nini maana ya maneno yale, “roho mbaya kutoka kwa BWANA”? Je, maana yake ni kwamba Mungu alituma pepo anayekaa Naye huko mbinguni, au maana yake ni kwamba Mungu aliruhusu pepo mmoja mwovu wa Shetani kumsumbua Sauli? Nadhani Wakristo wengi watakubaliana na maana ya pili, kutokana na mengine yanayofundishwa na Biblia. Sababu ya Maandiko kusema kwamba huyo pepo alitoka “kwa BWANA” ni kutokana na ukweli kwamba kazi yake ya kumsumbua Sauli ilitokana na adhabu ya Mungu juu yake. Basi, tunaona kwamba hata pepo wako chini ya utawala wa enzi ya Mungu.
Tunasoma pia katika Waamuzi 9:23 hivi: “Kisha Mungu akapeleka roho mbaya kati ya Abimeleki na watu wa Shekemu”, ili hukumu ya Mungu iwajie kwa sababu ya matendo yao maovu. Hapo tena, huyu pepo hakutoka mbinguni kwa Mungu bali katika ufalme wa Shetani, na aliruhusiwa na Mungu kutekeleza mambo maovu dhidi ya watu fulani, waliostahili hayo. Pepo hawawezi kufanikiwa kutimiza mipango yao miovu dhidi ya mtu awaye yote bila ya ruhusa ya Mungu. Kama si hivyo, basi Mungu hana nguvu zote. Kwa hiyo, tunaweza kuhitimisha kwa kusema kwamba, wakati Adamu alipoanguka, Shetani hakupata mamlaka yaliyozidi mipaka aliyoweka Mungu.
Mifano Ya Agano Jipya Kuhusu Nguvu Za Mungu Juu Ya Shetani
Agano Jipya linatoa ushahidi wa ziada wenye kupingana na hoja kwamba Shetani alifaidika kutokana na Anguko la Adamu.
Kwa mfano: Tunasoma katika Luka 9:1 kwamba Yesu aliwapa wanafunzi wake kumi na mbili “mamlaka juu ya pepo wote”. Tena katika Luka 10:19, Yesu aliwaambia hivi: “Tazama, nimewapa mamlaka ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu chochote kitakachowadhuru” (maneno mepesi kukazia).
Kama Yesu aliwapa wao mamlaka juu ya nguvu zote za Shetani, ni kwamba Yeye alikuwa na hayo mamlaka. Shetani yuko chini ya mamlaka ya Mungu.
Baadaye katika Injili ya Luka tunasoma habari za Yesu akimwambia Petro hivi: “Simoni! Simoni! Tazama, Shetani ameomba ruhusa ili akupepete kama ngano” (Luka 22:33, TLR). Maandiko yanaonyeshakwamba asingeweza kumpepeta Petro bila ya kupata ruhusa kutoka kwa Mungu kwanza. Hapo tena, Shetani anaonyesha kuwa chini ya mamlaka ya Mungu.[4]
Kifungo Cha Shetani Cha Miaka Elfu Moja
Tunaposoma habari za kufungwa kwa Shetani na malaika mmoja tu katika Ufunuo 20, Adamu hatajwi hapo kwamba milki yake imefikia mwisho. Sababu itoleayo hapo ni kwamba, “ili asiwadanganye tena mataifa” (Ufunuo 20:3).
Ajabu ni hii: Baada ya Shetani kufungwa miaka elfu moja, atafunguliwa, “naye atatoka ili kuwadanganya mataifa, walio katika pembe nne za dunia” (Ufunuo 20:8). Hayo mataifa yatakayodanganywa yataandaa majeshi yao ili kushambulia Yerusalemu, mahali ambapo Yesu atakuwepo akitawala. Baada ya kuuzunguka mji, moto utatoka mbinguni na “kuwateketeza” (Ufunuo 20:9).
Je, kuna anayeweza kuwa mjinga kiasi cha kusema kwamba haki ya kumiliki ya Adamu ilihusu kipindi kifupi tu cha muda baada ya miaka elfu moja, na ndiyo maana Mungu ilibidi amwachie Shetani kwa sababu hiyo? Wazo kama hilo ni la kipuuzi!
Hapana! Tunachojifunza kwa mara nyingine tena kutoka fungu hili la Maandiko ni kwamba Mungu ana mamlaka kamili juu ya Shetani, na humruhusu afanye udanganyifu wake ili kutimiza makusudi Yake tu.
Katika ule utawala wa Yesu hapo baadaye wa miaka elfu moja, Shetani hatakuwa katika utendaji – atashindwa kumdanganya mtu yeyote. Ila, watakuwepo watu duniani watakaokuwa watiifu kwa utawala wa Kristo kwa nje tu, ambao ndani watapenda kumwona aking’olewa madarakani. Lakini hawatajaribu kufanya mapinduzi kwa sababu wanajua hawawezi kumpindua mtu “atakayetawala kwa fimbo ya chuma” (Ufunuo 19:15).
Lakini Shetani atakapofunguliwa, ataweza kuwadanganya wale ambao wanamchukia Kristo mioyoni mwao, nao watajaribu kufanya yasiyowezekana, kwa sababu ya upumbavu. Naye Shetani atakaporuhusiwa kuwadanganya waasi waliojificha, hali halisi ya mioyo yao itafunuliwa, ndipo Mungu kwa haki kabisa atakapowahukumu wale ambao hawastahili kuishi katika ufalme Wake.
Hiyo ndiyo sababu moja ya Mungu kumruhusu Shetani kuwadanganya watu siku hizi. Baadaye tutachunguza makusudi kamili ya Mungu kwa ajili ya Shetani, lakini kwa sasa yatosha tu kusema kwamba Mungu hataki mtu yeyote abaki amedanganywa. Ila, anataka kujua kilichomo mioyoni mwa watu. Shetani hawezi kuwadanganya wale wanaojua na kuamini kweli. Lakini Mungu anamruhusu Shetani kuwadanganya wale ambao, kwa sababu ya mioyo yao migumu, wanakataa ukweli.
Paulo anasema juu ya kipindi cha utawala wa mpingakristo, kama ifuatavyo:
Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake; yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu (2Wathes. 2:8-12. Maneno mepesi kukazia).
Ona kwamba anayetajwa kwamba atatuma “nguvu ya upotevu, wauamini uongo” ni Mungu. Lakini pia ona kwamba watu hao watakaodanganywa ni watu ambao “hawakuiamini kweli,” kuonyesha kwamba wao walipata nafasi, lakini bado walikataa Injili. Mungu atamruhusu Shetani kumtia nguvu mpingakristo kwa uwezo wa kufanya ishara za uongo na maajabu, ili wanaomkataa Kristo wadanganyike, na kusudi la Mungu hatimaye ni kwamba “wote wahukumiwe.” Kwa sababu hiyo hiyo, Mungu anamruhusu Shetani kuwadanganya watu siku hizi.
Kama Mungu hakuwa na sababu ya kumruhusu Shetani kufanya kazi hapa duniani, angekwisha mfukuza aende mahali pengine, wakati alipoanguka. Tunaambiwa katika 2Petro 2:4 kwamba kuna malaika fulani waliotenda dhambi ambao tayari Mungu amekwisha watupa kuzimu, na kuwafunga katika “vifungo vya giza, wakisubiri hukumu.” Mungu wetu mwenye nguvu zote angeweza kufanya hivyo hivyo kwa Shetani na kwa yeyote katika malaika zake kama ingefaa mapenzi Yake makamilifu. Lakini, kwa muda kidogo zaidi, Mungu ana sababu nzuri tu za kumruhusu Shetani na malaika zake kufanya kazi hapa duniani.
Hofu Ya Mapepo Kuteswa
Tunapomalizia mafunzo yetu kuhusu hekaya hii, tutazame mfano mmoja kutoka Maandiko, unaohusu watu wawili kutoka Gerasi, waliokuwa na pepo.
Naye [Yesu] alipofika ng’ambo katika nchi ya Wagerasi, watu wawili wenye pepo walikutana naye, wanatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kuipitia njia ile. Na tazama, wakapiga kelele wakisema, ‘Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?’ (Mathayo 8:28, 29. Maneno mepesi kukazia).
Mara nyingi habari hii hutumiwa na wale wenye kufundisha kwamba Shetani Alifaidika ili kuunga mkono mawazo yao. Wanasema hivi: “Unaona! Pepo walimwomba Yesu awatendee haki. Walijua hakuwa na haki ya kuwatesa kabla ya wakati wa kumalizika kwa haki ya umiliki nchi aliyokuwa nayo Adamu, yaani, wakati ambapo wao na Shetani wangetupwa katika ziwa la moto ili wateswe humo mchana na usiku hata milele.”
Ukweli ni tofauti kabisa. Wao walijua kwamba Yesu alikuwa na uwezo na haki zote kuwatesa wakati wowote aliotaka. Ndiyo sababu walimwomba awahurumie. Waliogopa san asana kwamba Mwana wa Mungu angewatuma wakateswe mapema zaidi. Luka anatuambia kwamba walimsihi “asiwaagize waende shimoni” (Luka 8:31). Kama Yesu hakuwa na haki hiyo kwa sababu ya haki fulani ambayo Shetani anadaiwa alikuwa nayo, wasingejali hata kidogo.
Hao pepo walitambua kwamba walikuwa wakitegemea rehema zsa Yesu kabisa, kama inavyo-onekana kwa wao kumwomba asiwatume nje ya nchi (Marko 5:10), na kumwomba awaruhusu kuwaingia kundi la nguruwe lililokuwepo (Marko 5:12), wao kumsihi wasitupwe “shimoni” (Luka 8:31), na kumwomba Kristo wasiteswe “kabla ya wakati”.
Tutazame hekaya nyingine inayoaminiwa sana, kuhusu Shetani.
Hekaya Ya Nne: “Shetani Kama ‘mungu wa dunia hii’ Anatawala Kila Kitu Duniani – Serikali Za Wanadamu, Majanga, Na Hali Ya Hewa.”
Katika Maandiko, Shetani anatajwa na mtume Paulo kwamba ni “mungu wa
dunia hii” (2Wakor. 4:4) na kuitwa na Yesu “mkuu wa dunia hii” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11). Kutokana na majina haya ya Shetani, wengi wamedhani kwamba anatawala kikamilifu kabisa dunia. Japo tumekwisha tazama maandiko ya kutosha kuweka wazi kosa la hekaya hii, itatusaidia kujifunza zaidi ili tuwe na ufahamu kamili kuhusu jinsi ambavyo nguvu za Shetani zilivyo na mipaka. Ni lazima tuwe makini kwamba ufahamu wetu kuhusu Shetani usiwe umejengwa kwenye maandiko manne tu yenye kumtaja kwamba ni mungu, au mkuu wa dunia hii.
Tunapochunguza Biblia zaidi tunaona kwamba zaidi ya Yesu kumtaja Shetani kwamba ni “mkuu wa dunia hii” alimtaja Baba Yake wa mbinguni kwamba ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Mathayo 11:25; Luka 10:21. Maneno mepesi kukazia). Tena, mtume Paulo hakumwita Shetani kuwa ni “mungu wa dunia hii” tu, bali pia aliongeza, kama Yesu, akamtaja Mungu kuwa ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Matendo 17:24. Maneno mepesi kukazia). Hii hututhibitishia sisi kwamba Yesu wala Paulo hawataki tudhani kwamba Shetani ana mamlaka kamili juu ya nchi. Lazima mamlaka ya Shetani yawe na mipaka.
Tofauti muhimu sana kati ya maandiko hayo yanayotofautiana inapatikana katika maneno mawili: dunia na nchi. Japo tunayatumia kwa pamoja, katika Kiyunani hayo mawili hayafanani. Tukiisha elewa jinsi yanavyotofautiana, ufahamu wetu kuhusu mamlaka ya Mungu na ya Shetani hapa duniani yanaongezeka sana.
Yesu alimwita Mungu Baba kuwa ni Bwana wa nchi. Neno la Kiyunani linalotafsiriwa nchi ni ge. Hili linamaanisha sayari hii tunayoishi, na neno la Kiingereza geography (au, jiografia) limetokana nalo.
Kinyume chake, Yesu alisema kwamba Shetani ni mtawala wa dunia hii. Neno la Kiyunani linalotafsiriwa dunia ni kosmos, ambalo kikawaida husema juu ya mpango au utaratibu. Linazungumzia watu badala ya sayari yenyewe. Ndiyo sababu Wakristo mara nyingi wanasema juu ya Shetani kama “mungu anayetawala taratibu za dunia hii.”
Kwa sasa hivi, Mungu hana mamlaka yote juu ya dunia kwa sababu hajawatawala watu wote wa dunia. Sababu yake ni kwamba, amewapa watu wote uchaguzi kuhusu nani awe bwana katika maisha yao, na wengi wamechagua kumpa Shetani nafasi hiyo. Tusisahau kwamba hiari ya mwanadamu ni sehemu ya mpango wa Mungu.
Paulo alitumia neno tofuati la Kiyunani kusema juu ya dunia, alipoandika juu ya mungu wa dunia hii. Ni neno aion, ambalo mara nyingi hutafsiriwa kama kipindi, majira, nyakati, yaani, wakati maalum uliopangwa au kuwekwa. Shetani ni mungu wa kipindi au wakati huu wa sasa.
Nini basi maana ya yote hayo? Nchi ni sayari tunayokaa. Dunia ni watu ambao wanakaa kwa sasa duniani, n asana sana wale ambao hawamfuati Yesu. Wao wanamfuata Shetani, na wamenaswa katika utaratibu wake uliopotoka, wa dhambi. Sisi kama Wakristo tunasemekana “tupo duniani” lakini si “wa dunia” (Yohana 17:11, 14). Tunakaa miongoni mwa raia wa ufalme wa giza, lakini ukweli ni kwamba tuko katika ufalme wa nuru – ufalme wa Mungu.
Basi, sasa tunalo jibu. Kwa ufupi tu ni hivi: Mungu anatawala dunia nzima kimamlaka. Ila, kwa ruhusa ya Mungu, Shetani anatawala “taratibu za dunia” tu, yaani, anawatawala wale raia wa ufalme wake wa giza. Kwa sababu hii, mtume Yohana aliandika kwamba “dunia nzima (sio nchi nzima) iko katika nguvu za yule mwovu” (1Yohana 5:19).
Hii haimaanishi kwamba Mungu hana mamlaka juu ya dunia au mipangilio ya dunia, au watu katika dunia hii. Kama Danieli alivyosema, Yeye ni “anatawala katika falme za wanadamu, naye humpa yule amtakaye” (Danieli 4:25). Bado anaweza kumwinua au kumshusha mtu yeyote amtakaye. Ila, kama “mtawala” mkuu “juu ya falme za wanadamu” amemruhusu Shetani kuwatawala wanadamu wote walio kinyume Chake, yaani, waasi.
Tutazame Toleo La Shetani
Hii tofauti kati ya dunia na nchi itatusaidia pia kuelewa jaribu la Yesu pale nyikani. Huko, Shetani alimwonyesha Yesu “falme zote za dunia kwa dakika moja.” Shetani asingempa Yesu nafasi ya kisiasa juu ya serikali za wanadamu duniani – yaani, kitu tunachoita urais au uwaziri mkuu. Si Shetani anayewainua na kuwashusha wanadamu wakuu wa dunia – ni Mungu.
Badala yake – Shetani bila shaka alimwonyesha Yesu falme zote ndogo ndogo katika ufalme wake wa giza duniani kote. Alimwonyesha Yesu mpangilio wa utawala wa kipepo, ambao, katika maeneo yao, wanatawala juu ya ufalme wa giza, pamoja na wale binadamu waasi ambao ni raia wao. Shetani akampa Yesu mamlaka juu ya utawala wake – kama Yesu angejiunga na uasi wa Shetani dhidi ya Mungu. Hapo, Yesu angekuwa makamu wake katika ufalme wa giza.
Utawala Wa Mungu Juu Ya Serikali Za Binadamu, Duniani
Hebu tuonyeshe vizuri zaidi mipaka ya mamlaka ya Shetani kwa kutazama maandiko kwanza, yenye kuthibitisha mamlaka ya Mungu juu ya serikali za duniani za wanadamu. Shetani anayo mamlaka kiasi katika serikali za duniani za wanadamu kwa sababu ana mamlaka juu ya watu ambao hawajaokoka, na serikali mara nyingi hutawaliwa na watu ambao hawajaokoka. Lakini, Mungu ndiye mwenye mamlaka yote juu ya serikali za wanadamu, na Shetani anaweza kuzitumia kwa kiwango ambacho Mungu ataruhusu tu.
Tayari tumekwisha tazama maneno ya Danieli kwa mfalme Nebukadneza, lakini kwa sababu ni kitu kinachosaidia, hebu tuyatazame tena.
Mfalme mkuu Nebukadneza alikuwa ameinuka sana kwa kiburi kutokana na uwezo wake na mafanikio yake makubwa. Basi, Mungu akatangaza kwamba atashushwa mpaka chini kabisa ili aweze kujifunza kwamba “Aliye Juu anatawala katika falme za wanadamu, naye humpa yeyote amtakaye” (Danieli 4:17). Ni dhahiri kwamba Mungu ndiye anahusika na kupanda kwa Nebukadneza kufikia ukuu kisiasa. Ndivyo ilivyo kwa kila kiongozi wa kidunia. Mtume Paulo, akisema juu ya watawala wa duniani, alitangaza kwamba “kila mamlaka hutoka kwa Mungu, na zilizoko zimewekwa na Mungu” (Warumi 13:1).
Mungu ndiye mamlaka kuu katika ulimwengu wote. Kama kuna mwenye mamlaka mwingine, ni kwa sababu Mungu amempa kidogo, au amemruhusu mwingine kuwa nayo kidogo.
Vipi basi kuhusu watawala waovu? Je, Paulo anamaanisha kwamba hata wao wanawekwa na Mungu? Ndiyo. Mapema kidogo katika barua hiyo hiyo, Paulo aliandika hivi: “Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao ya kwamba, ‘Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, Jina langu likatangazwe katika nchi yote’.” (Warumi 9:17). Mungu alimwinua Farao – mwenye moyo mgumu – kwa kusudi la kujitukuza Mwenyewe. Mungu angeonyesha nguvu Zake kuu kupitia miujiza Yake ya ukombozi – nafasi iliyopatikana kwa kuwepo mtu jeuri ambaye Yeye Mwenyewe alimwinua.
Kwani, jambo hili haliko wazi katika mazungumzo ya Yesu na Pilato? Pilato, akishangazwa na jinsi ambavyo Yesu hakumjibu maswali yake, alisema hivi: “Mbona huzungumzi nami? Hujui kwamba nina mamlaka ya kukuachia huru, na mamlaka ya kukusulubisha?” (Yohana 19:10).
Yesu akamjibu hivi: “Wewe usingekuwa na mamlaka juu Yangu, kama usingepewa kutoka juu” (Yohana 19:11. Maneno mepesi kukazia). Akijua tabia ya Pilato ya uoga, Mungu alimwinua ili mpango Wake kwa Yesu kufa msalabani uweze kufanikiwa.
Ukisoma vitabu vya historia katika Agano la Kale kwa haraka haraka, utaona kwamba wakati mwingine Mungu huwatumia watawala wanadamu ambao ni waovu kama mawakala wa hasira Yake juu ya watu wanaostahili hukumu. Nebukadneza alitumiwa na Mungu kuleta hukumu Yake juu ya mataifa mengi katika Agano la Kale.
Ipo mifano mingi sana ya watawala ambao Mungu aliwainua au kuwashusha katika Biblia. Kwa mfano: Katika Agano Jipya tunasoma juu ya Herode ambaye hakumpa Mungu utukufu wakati baadhi ya raia wake walipopiga kelele mbele zake na kusema, “Hiyo ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!” (Matendo 12:22).
Ikawaje? “Mara, malaika wa Bwana akampiga … naye akaliwa na funza, akafa” (Matendo 12:23).
Kumbuka hivi: Herode alikuwa raia katika ufalme wa Shetani, lakini hakuwa nje ya mamlaka ya Mungu. Basi, Mungu anaweza kumwangusha kiongozi yeyote wa duniani hata sasa, kama akitaka.[5]
Ushuhuda Binafsi Wa Mungu
Kwa kumalizia, hebu tusome kile ambacho Mungu Mwenyewe aliwahi kusema kupitia nabii Yeremia, kwa habari ya enzi na ukuu Wake juu ya falme za wanadamu, hapa duniani.
Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulvyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli. Wakati wowote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung’oa, na kuuvunja, na kuuangamiza; ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake, nitaghairi, nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda. Na wakati wowote nitakapotoa habari za taifa na habari za ufalme, kuujenga na kuupanda, ikiwa watatenda maovu mbele za macho yangu, wasiitii sauti yangu, basi nitaghairi, nisitende mema yale niliyoazimia kuwatendea (Yeremia 18:6-10).
Je, unaona sasa kwamba hakuna jinsi ambayo Shetani angeweza kumpa Yesu utawala halali juu ya falme za duniani za wanadamu za kisiasa, wakati alipokuwa anamjaribu pale nyikani? Kama alikuwa anamwambia kweli (kama ambavyo anafanya wakati mwingine), basi alichokuwa anampa Yesu ni utawala juu ya ufalme wake wa giza.
Lakini je, Shetani ana ushawishi katika serikali za wanadamu? Ndiyo, lakini ni kwa sababu yeye ndiye bwana wa kiroho juu ya watu ambao hawajaokoka, na watu ambao hawajaokoka wamo katika serikali za wanadamu. Ila, ana mamlaka kiasi cha ruhusa anayopewa na Mungu kuwa nayo, na Mungu anaweza kuvuruga mipango ya Shetani wakati wowote anaotaka. Mtume Yohana aliandika juu ya Yesu kwamba ni “mtawala wa wafalme wa dunia” (Ufunuo 1:5).
Je, Shetani Huleta Majanga Na Hali Mbaya Ya Hewa?
Kwa kuwa Shetani ni “mungu wa dunia hii,” wengi wamedhani kwamba
anatawala hali ya hewa, na ndiye mwenye kuleta majanga yote kama vile ukame, mafuriko, vimbunga, matetemeko, na kadhalika. Lakini je, hivyo ndivyo Maandiko yanavyotufundisha? Hapa tena inabidi tuwe makini kutokujenga itikadi yetu kuhusu Shetani kutokana na andiko moja tu linalosema hivi: “Mwivi haji isipokuwa aibe, kuua na kuharibu” (Yohana 10:10). Mara nyingi sana watu wametumia mstari huu kuthibitisha kwamba kila kitu kinachoiba, kuua au kuharibu hutoka kwa Shetani. Lakini, tukitazama Biblia zaidi tunajifunza kwamba Mungu Mwenyewe wakati mwingine huua na kuharibu. Hebu tazama mafungu haya matatu, kutoka katika mifano mingi tu iliyopo.
Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza (Yakobo 4:12. Maneno mepesi kukazia).
Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo! (Luka 12:5. Maneno mepesi kukazia).
Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum (Mathayo 10:28. Maneno mepesi kukazia).
Tukisema kwamba kila kitu kinachohusisha kuua au kuharibu ni kazi ya Shetani, tunakosea. Kuna mifano mingi sana ya Mungu kuua na kuharibu katika Biblia.
Tujiulize hivi: Wakati Mungu aliposema juu ya mwizi anayekuja kuua, kuiba na kuharibu, alikuwa anasema juu ya Shetani, au mwingine? Hapo tena, tunachohitaji ni kusoma maneno Yake katika mantiki yake. Mstari mmoja kabla hajasema aliyosema juu ya mwizi kuja kuiba, kuua na kuharibu, Yesu alisema hivi: “Wote walionitangulia ni wezi na wanyang’anyi, na kondoo hawakuwasikia” (Yohana 10:8). Tunaposoma maelezo yote ya Yesu katika Yohana 10:1-15 akisema Yeye ni Mchungaji mwema, inakuwa wazi zaidi kwamba maneno aliyotumia – mwizi na wezi – yanawahusu waalimu wa uongo na viongozi bandia wa dini.
Maoni Mbalimbali Kuhusu Hali Mbaya Ya Hewa Na Majanga
Kimbunga au tetemeko linapotokea, swali la kitheolojia hutokea katika akili za watu wanaomwamini Mungu. Ni hili: “Nani amesababisha hili?” Kwa Wakristo wanaoamini Biblia, ni mawili: Aidha ni Mungu, au ni Shetani.
Wengine wanaweza kupinga hivi: “Hapana! Mungu hahusiki! Watu ndiyo wanahusika. Mungu anawahukumu kwa ajili ya dhambi zao.”
Kama Mungu analeta kimbunga na matetemeko kwa sababu ya hukumu Yake juu ya dhambi, basi kweli tunaweza kuwalaumu binadamu waasi badala ya Mungu, lakini hata hivyo, Mungu bado anawajibika, kwa sababu majanga kama hayo yasingetokea bila ya agizo Lake.
Au kama ni kweli kwamba Mungu humruhusu Shetani kutuma vimbunga na matetemeko ili kuleta hukumu Yake juu ya wenye dhambi, basi tunaweza kusema ni Shetani anayesababisha, lakini bado Mungu anawajibika. Sababu ni kwamba, Yeye ndiye aliyemruhusu Shetani kusababisha uharibifu huo, na ni kwa sababu majanga hayo yanatokea kama itikio Lake kwa dhambi.
Kuna wanaosema si Mungu wala Shetani wanaohusika katika vimbunga na matetemeko, bali ni “matukio ya kawaida ya kiasili katika dunia yetu ya dhambi.” Hata hao wanajaribu kwa mbali kuweka lawama juu ya binadamu kwa majanga ya kiasili, lakini nao wanapotea. Maelezo hayo hayamwondoi Mungu katika picha. Kama vimbunga ni “tukio la kawaida kiasili katika dunia yetu ya dhambi”, nani aliyeamua iwe hivyo? Ni dhahiri kwamba vimbunga havitengenezwi na mwanadamu. Yaani, havitokei kwa sababu kiasi fulani cha uongo kimejaa katika anga. Matetemeko hayatokei wakati kiasi fulani cha watu wanapozini.
Hapana. Ni hivi: Kama kuna mahusiano kati ya kimbunga na dhambi, basi Mungu anahusika, kwa sababu vimbunga ni madhihirisho ya hukumu Yake juu ya dhambi. Hata kama vinatokea bila mpangilio, ni lazima iwe kwa amri ya Mungu, na kwa hali hiyo, anahusika.
Hata kama hakuna mahusiano yoyote kati ya dhambi na majanga, na iwe kwamba Mungu alikosa alipoitengeneza dunia na kusababisha udhaifu katika umbo la dunia mpaka kuna nyakati linasogea, na iwe kwamba taratibu za hali ya hewa mara kwa mara huondoka kwenye mpango, bado Mungu angebeba wajibu kwa ajili ya matetemeko na vimbunga, kwa sababu Yeye ndiye Mwumbaji, na makosa Yake yanawadhuru watu.
Hakuna Kitu Kinachoitwa “Asili Mama”
Basi, tuna majibu mawili yanayoweza kutolewa kuhusu swala la majanga. Aidha Mungu au Shetani wanahusika. Kabla hatujatazama Maandiko fulani ili kuamua jibu sahihi, hebu tufikiri zaidi majibu hayo mawili.
Kama Shetani ndiye mwenye kuleta majanga, basi Mungu anaweza au hawezi kumzuia. Kama Mungu anaweza kumzuia Shetani asilete majanga na hamzuii, basi hapo tena anawajibika. Janga lisingetokea bila ruhusa Yake.
Twende upande wa pili. Hebu tudhani kwamba Mungu hawezi kumzuia Shetani, lakini angetaka. Je, kitu kama hicho kipo?
Ikiwa Mungu hawezi kumzuia Shetani asilete janga, basi ni kwamba Shetani ana nguvu zaidi ya Mungu, au Shetani ni mjanja kuliko Mungu. Kimsingi, hicho ndicho kinachosemwa na wale wanaosema kwamba “Shetani alipata utawala wa dunia wakati Adamu alipoanguka.” Wanadai kwamba Shetani ana haki kisheria kufanya chochote anachotaka hapa duniani kwa sababu yeye aliiba hati miliki ya Adamu. Sasa – tuseme kwamba Mungu angependa kumzuia Shetani lakini hawezi kwa sababu inabidi aheshimu hati miliki ya Adamu ambaye sasa iko mikononi mwa Shetani. Maana yake ni kwamba, Mungu alikuwa mjinga kiasi cha kutoweza kuona mambo ambayo yangetokea wakati wa anguko la mwanadamu, lakini Shetani, kwa sababu ana akili kuliko Mungu, sasa amepata zile nguvu ambazo Mungu alitaka asiwe nazo. Haiwezekani kuwa hivyo. Shetani hana akili kuliko Mungu!
Kama nadharia kwamba “Shetani Alifaidika” ni ya kweli, tungetaka kujua ni kwa nini Shetani hasababishi matetemeko na vimbunga zaidi kuliko vlivyoko sasa, na kwa nini halengi idadi kubwa ya Wakristo. (Ukisema “ni kwa sababu Mungu ha tamruhusu alenge idadi kubwa ya Wakristo”, tayari umekubali kwamba Shetani hawezi kutenda chochote bila ruhusa ya Mungu.)
Tukifupisha mambo, majibu mawili tu yanayowezekana ni haya: Aidha (1) Mungu husababisha matetemeko na vimbunga, au (2) Shetani hufanya hivyo kwa ruhusa ya Mungu.
Ona hapo kwamba bila ya kujali jibu gani ni sahihi, Mungu bado ndiye mwenye kuwajibika? Watu wanaposema, “Mungu hakutuma kimbunga hicho – ni Shetani aliyefanya kwa ruhusa ya Mungu,” hawamwondolei Mungu wajibu kama wanavyodhani. Kama Mungu angeweza kumzuia Shetani asisababishe kimbunga, bila ya kujali kama alitaka au hakutaka, bado anawajibika. Binadamu waasi wanaweza kuwa wa kulaumiwa kwa sababu ya dhambi zao (ikiwa kimbunga kilitumwa na Mungu au kuruhusiwa na Mungu kama hukumu), lakini bado itakuwa upuuzi kusema Mungu hahusiki kwa njia yoyote ile, au hawajibiki.
Ushuhuda wa Maandiko
Je, Maandiko yanasema nini hasa kuhusu “majanga”? Je, Biblia inasema kwamba yanaletwa na Mungu au na Shetani? Tuanze kwa kutazama matetemeko kwa sababu Biblia inataja mengi.
Kulingana na Maandiko, matetemeko yanaweza kutokea kama hukumu ya Mungu juu ya wenye dhambi wanaostahili. Tunasoma hivi katika Yeremia: “Mbele ya ghadhabu yake [Mungu] nchi yatetemeka, wala mataifa hawawezi kustahimili hasira yake” (Yeremia 10:10. Maneno mepesi kukazia).
Isaya anatoa onyo lifuatalo:
Naye atajiliwa na BWANA wa majeshi kwa ngurumo, na tetemeko la nchi, na sauti kuu, na chamchela, na tufani, na mwali wa moto uteketezao (Isaya 29:6. Maneno mepesi kukazia).
Utakumbuka bila shaka katika siku za Musa kwamba nchi ilifunuka na kuwameza akina Kora na wafuasi wake waasi (ona Hesabu 16:23-34). Hili lilikuwa tendo la hukumu ya Mungu kabisa. Mifano mingine ya hukumu ya Mungu kwa matetemeko inapatkana katika Ezekieli 38:19; Zaburi 18:7; 77:18; Hagai 2:6; Luka 21:11; Ufunuo 6:12; 8:5; 11:13; 16:18.
Matetemeko mengine yanayotajwa katika Maandiko si matendo ya hukumu ya Mungu, ila yalisababishwa na Mungu. Kwa mfano: Kulingana na injili ya Mathayo, kulikuwa na tetemeko wakati Yesu alipokufa (Mathayo 27:51, 54) na lingine wakati alipofufuka (Mathayo 28:2). Je, Shetani alisababisha hayo?
Wakati Paulo na Sila walipokuwa wanaimba sifa kwa Mungu usiku wa manane katika gereza huko Filipi, “mara kukatokea tetemeko kubwa la nchi, misingi ya gereza ikatikiswa, na mara ile ile milango yote ikafunguliwa, na minyororo ya kila mmoja ikalegezwa” (Matendo 16:26. Maneno mepesi kukazia). Je, Shetani ndiye alisababisha tetemeko hilo? Hapana. Hata mkuu wa gereza aliokoka baada ya kuona nguvu za Mungu. Na hilo si tetemeko la pekee lililosababishwa na Mungu katika kitabu cha Matendo (ona Matendo 4:31).
Hivi karibuni nilisikia kuhusu Mkristo mwenye nia njema tu, ambaye, baada ya kusikia juu ya uwezekano wa kutokea kwa tetemeko katika sehemu fulani, alisafiri hadi hapo kwenda kufanya “vita ya kiroho” dhidi ya Shetani. Unaona kosa katika dhana hiyo? Ingekuwa sawa kimaandiko kwake kumwomba Mungu awarehemu hao watu walioishi katika eneo hilo. Na kama angefanya hivyo, asingekuwa na haja ya kupoteza muda wake na fedha kwenda kwenye eneo lenyewe – Mungu angeombwa pale pale nyumbani kwake. Ila, kufanya vita na Shetani ili kuzuia tetemeko si kitu kinachoungwa mkono na maandiko.
Vipi Kuhusu Vimbunga?
Neno kimbunga halipo katika Maandiko, lakini tunaweza kupata mifano ya upepo mkali. Kwa mfano:
Washukao baharini katika merikebu, wafanyao kazi yao katika maji mengi, hao huziona kazi za BWANA, na maajabu yake vilindini. Maana husema, akavumisha upepo wa dhoruba, ukayainua juu mawimbi yake (Zaburi 107:23-25. Maneno mepesi kukazia).
Lakini BWANA alituma upepo mkuu baharini, ikawa tufani kubwa baharini, hata merikebu ikawa karibu na kuvunjika (Yona 1:4. Maneno mepesi kukazia).
Baada ya hayo nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wowote (Ufunuo 7:1).
Ni dhahiri kwamba Mungu anaweza kuanzisha dhoruba za upepo mkali, na kuzizuia.[6]
Katika Biblia nzima, kuna mstari mmoja tu unaotaja kwamba Shetani alituma upepo. Ni katika majaribu ya Ayubu. Mjumbe alimletea taarifa hivi: “Upepo mkali ulikuja kutoka nyikani, ukaipiga nyumba pande zote, nayo ikawaangukia vijana, nao wamekufa” (Ayubu 1:19).
Kutokana na kusoma sura ya kwanza ya kitabu cha Ayubu tunajua kwmaba Shetani ndiye aliyesababisha matatizo kwa Ayubu. Lakini, tusisahau kwamba asingeweza kufanya chochote kumdhuru Ayubu au watoto wake bila ya ruhusa ya Mungu. Basi, hapo tena tunaona kwamba Mungu anatawala upepo.
Tufani Ya Galilaya
Vipi kuhusu ile “tufani kali” iliyowavamia Yesu na wanafunzi Wake wakati fulani walipokuwa wanavuka Bahari ya Galilaya? Bila shaka ilisababishwa na Shetani, maana Mungu asingeweza kutuma upepo ambao ungepindua mtumbwi wenye Mwana Wake! “Ufalme ukifitinika juu yake wenyewe utaanguka.” Basi, kwa nini Mungu atume upepo ambao ungeweza kumdhuru Yesu na wanafunzi Wake kumi na wawili?
Hizo ni hoja nzuri, lakini hebu tufikiri kidogo. Kama Mungu hakutuma upepo, na iwe ni Shetani, basi lazima tukubali bado kwamba Mungu alimruhusu Shetani autume. Hivyo, swali lile lile bado linahitaji kujibiwa: Kwa nini Mungu amruhusu Shetani kutuma tufani ambayo ingeweza kumdhuru Yesu na wale kumi na wawili?
Je, kuna jibu? Pengine Mungu alikuwa anawafundisha wanafunzi kuhusu imani. Pengine alikuwa anawapima. Pengine alikuwa anampima Yesu, ambaye ilibidi “ajaribiwe katika mambo yote kama sisi, ila yeye hakutenda dhambi” (Waebrania 4:15). Ili aweze kujaribiwa kikamilifu, Yesu ilibidi apitie katika tukio la kumfanya ahofu. Pengine Mungu alitaka kumtukuza Yesu. Pengine alitaka kufanya hayo yote yaliyotajwa hapo juu.
Mungu aliwaongoza wana wa Israeli ukingoni mwa Bahari ya Shamu akijua kabisa kwamba walikuwa wamenaswa na jeshi la Farao lililowafuatia. Lakini je, hakuwa anawakomboa Waisraeli? Kama ndivyo, mbona alikuwa anajipinga kwa kuwaongoza kwenye sehemu ambapo wangeuawa kabisa? Je, huo si mfano wa “ufalme kufitinika juu yake wenyewe”?
Hapana kwa sababu, Mungu hakukusudia kuwaachia Waisraeli waangamizwe. Naye hakukusudia kuwaacha Yesu na wanafunzi Wake kuzama, wakati alipotuma au alipomruhusu Shetani kusababisha tufani katika Bahari ya Galilaya.
Pamoja na hayo – Biblia haisemi kwamba Shetani alituma tufani hiyo katika Bahari ya Galilaya, wala haisemi Mungu ndiye alituma. Kuna wanaosema kwamba ni Shetani kwa sababu Yesu aliikemea ikatulia. Sawa, lakini si hoja yenye nguvu. Yesu hakumkemea Mungu – Yeye alikemea upepo. Mungu Baba angeweza kufanya vivyo hivyo. Yaani, angeweza kusababisha tufani kwa neno, kisha akautuliza kwa kuukemea. Kwa kuwa Yesu alikemea tufani si uthibitisho kwamba Shetani ndiye aliyeileta.
Hapa tena tusijenge theolojia yetu juu ya mstari mmoja ambao hauthibitishi kitu chochote. Tayari tumetaja maandiko mengi yenye kuthibitisha kwamba Mungu ndiye anayetawala upepo, na mara nyingi inasemekana kwamba Yeye ndiye aliyeutuma. Hoja ni kwamba, Shetani, hata ingawa ndiye “mungu wa dunia hii,” hana mamlaka huru juu ya upepo, wala hana haki ya kusababisha tufani au kimbunga wakati wowote au mahali popote anapotaka.
Basi – wakati vimbunga vinapotokea, tusione kana kwamba ni kitu ambacho kiko nje ya uwezo wa Mungu – kitu ambacho angependa kukizuia lakini hawezi. Yesu alipokemea ule upepo na tufani katika Bahari ya Galilaya ni ushahidi tosha kwamba Mungu anaweza kusimamisha tufani akitaka.
Na kama Mungu anatuma (au anaruhusu) tufani, basi lazima awe na sababu fulani, na jibu linalofaa zaidi kwa habari ya kutuma au kuruhusu tufani yenye kuleta uharibifu mkubwa kabisa ni kwamba, anawaonya na kuwahukumu watu wasiotii.
“Lakini, Wakati Mwingine Vimbunga Hudhuru Wakristo”
Ila sasa – vipi kuhusu Wakristo ambao wanaathiriwa na majanga ya kawaida? Kimbunga kinapopiga mahali, hakibomoi nyumba za wasiokuwa Wakristo tu. Je, Wakristo hawaepushwi na ghadhabu ya Mungu kutokana na kifo cha Yesu kama dhabihu kwa ajili yao? Tunawezanje basi kusema kwamba Mungu ndiye anayehusika na majanga, wakati yanaweza kuwadhuru watoto Wake Mwenyewe?
Kwa kweli hayo ni maswali magumu. Ila, tunapaswa kutambua kwamba majibu yake hayatakuwa rahisi kama tutayajenga kwenye dhana potofu kwamba Shetani husababisha majanga. Kama Shetani anasababisha majanga yote, inakuwaje Mungu amruhusu kufanya mambo yatakayodhuru watoto wa Mungu Mwenyewe? Bado tatizo ni lile lile.
Lakini Biblia inasema wazi kabisa kwamba walio katika Kristo “si watoto wa ghadhabu” (1Wathes. 5:9). Pia, inasema kwamba “ghadhabu ya Mungu inawakalia” wale wasiomtii Yesu (Yohana 3:36). Sasa – ghadhabu ya Mungu inawezaje kukaa juu ya wasiookoka bila ya kuwaathiri walio-okoka, na huku wote wanaishi pamoja? Jibu ni kwamba, wakati mwingine haiwezekani, na huo ndiyo ukweli.
Siku zile za Waisraeli kutoka Misri, Waisraeli wote walikuwa wanakaa mahali pamoja, na mapigo ambayo Mungu alituma juu ya Wamisri kama hukumu hayakuwa-athiri (ona Kutoka 8:22, 23; 9:3-7; 24-26; 12:23). Lakini kwa habari yetu, tunaishi na kufanya kazi pamoja na “Wamisri”. Kama Mungu atawahukumu kwa njia ya janga, tutaepukaje?
Kuepuka ndiyo neno muhimu hapa, katika kuelewa jibu la swali letu. Ingawa Nuhu aliepuka ghadhabu ya Mungu wakati gharika ilipofunika dunia, bado aliathirika, maana ilimbidi afanye kazi kujenga safina, kisha alikaa mwaka mzima na wanyama wengi tu katika safina. (Tusisahau: Agano la Kale pamoja na Agano Jipya humtaja Mungu kuwa ndiye aliyeleta gharika ya Nuhu, si Shetani. Ona Mwanzo 6:17; 2Petro 2:5).
Lutu pia aliponya maisha yake wakati hukumu ya Mungu ilipokuja juu ya Sodoma na Gomora, lakini alipoteza kila kitu katika moto ulioshuka. Hukumu ya Mungu juu ya waovu ilimwathiri mtu mwenye haki.
Miaka ya baadaye tunaona Yesu akiwaonya waamini waliokuwa Yerusalemu kwamba wakimbie watakapoona mji wao umezungukwa na majeshi, maana hizo zitakuwa siku “za ghadhabu” (Luka 21:22, 23) – kuonyesha wazi kabisa makusudi ya ghadhabu ya Mungu kwa kuruhusu Warumi kuuzingira Yerusalemu mwaka wa 70 B.K. Sifa kwa Mungu kwa Wakristo waliojali maonyo ya Kristo, maana waliponya maisha yao, lakini bado walipoteza kila kitu walichotakiwa kuacha Yerusalemu.
Katika hiyo mifano yote mitato, tunaona kwamba watu wa Mungu wanaweza kuteseka kiasi fulani, wakati hukumu ya Mungu inaposhuka juu ya waovu. Basi, hatuwezi kuamua tu kwamba kwa kuwa wakati mwingine Wakristo huathirika na majanga, Mungu hahusiki kuyaleta.
Sasa – Tufanye Nini?
Tunaishi katika dunia iliyolaaniwa na Mungu – ambayo inakumbwa na ghadhabu ya Mungu wakati wote. Paulo aliandika hivi: “Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa [ sio “itadhihirishwa”] kutoka mbinguni dhidi ya uovu wote na uasi wa wanadamu” (Warumi 1:18). Kama wanaoishi katika dunia ovu, iliyolaaniwa na Mungu, hatuwezi kuepuka kabisa matokeo ya ghadhabu ya Mungu juu yake, hata ingawa hiyo ghadhabu haielekezwi kwetu.
Tukijua hayo, tufanyeje? Kwanza: Tumwamini Mungu. Yeremia anaandika hivi:
Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea BWANA, ambaye BWANA ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bishi; wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaaacha kuzaa matunda (Yeremia 17:7, 8).
Angalia – Yeremia hakusema kwamba mtu anayemtegemea Bwana hatakabiliwa na hari. Hapana. Wakati hari na mwaka wa uchache wa mvua vinapokuja, yule mtu anayemtegemea Bwana ni sawa na mti wenye kueneza mizizi yake pembeni ya kijito. Yeye anakuwa na mahali pengine pa kupatia, wakati dunia inayomzunguka inahangaika. Habari za Eliya kulishwa na kunguru wakati wa njaa huko Israeli ni mfano mmoja (ona 1Wafalme 17:1-6). Daudi aliandika hivi kuhusu wenye haki: “Katika siku za njaa watajazwa na vingi” (Zaburi 37:19).
Lakini – njaa haziletwi na Shetani? Hapana – Maandiko hayasemi hivyo. Kwenye hilo, Mungu anawajibika, na njaa mara nyingi husemwa kwamba ni matokeo ya ghadhabu Yake kwa watu wanaostahili. Kwa mfano:
Kwa sababu hiyo BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Tazama, nitawaadhibu watu hawa; vijana watakufa kwa upanga; wana wao na binti zao watakufa kwa njaa’ (Yeremia 11:22. Maneno mepesi kukazia).
BWANA wa majeshi asema hivi, ‘Tazama, nitaleta juu yao upanga, na njaa, na tauni, nami nitawafanya kuwa kama tini mbovu zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu’ (Yeremia 29:17).
Mwanadamu! Nchi itakapofanya dhambi na kuniasi kwa kukosa, nikaunyosha mkono wangu juu yake na kulivunja tegemeo la chakula chake, na kuipelekea njaa, na kukatilia mbali mwanadamu na mnyama … (Ezekieli 14:13. Maneno mepesi kukazia).
Mlitazamia vingi, kumbe vikatokea vichache; tena mlipovileta nyumbani nikavipeperusha. Ni kwa sababu gani? Asema BWANA wa majeshi. Ni kwa sababu ya nyumba yangu inayokaa hali ya kuharibika, wakati ambapo ninyi mnakimbilia kila mtu nyumbani kwake. Basi, kwa ajili yenu mbingu zimezuiliwa zisitoe umande, nayo nchi imezuiliwa isitoe matunda yake. Nami nikaita wakati wa joto uje juu ya nchi, na juu ya milima, na juu ya nafaka, na juu ya divai mpya, na juu ya mafuta, na juu ya kila kitu itoacho nchi, na juu ya wanadamu, na juu ya wanyama, na juu ya kazi zote za mikono (Hagai 1:9-11. Maneno mepesi kukazia).
Katika mfano huu wa mwisho, tunasoma kwamba Waisraeli walilaumiwa kwa sababu ya ukame uliotokana na dhambi yao, lakini bado, Mungu anasema Yeye ndiye ameutuma.[7]
Mungu anapotuma njaa kwa watu waovu, nasi tuwe tunakaa katikati yao, tunachopaswa kufanya ni kuamini kwamba atatupa mahitaji yetu. Paulo alithibitisha kwamba njaa haiwezi kututenga na upendo wa Kristo! “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je, ni dhiki, au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?” (Warumi 8:35. Maneno mepesi kukazia). Ona kwamba Paulo hakusema Wakristo hawatakabiliwa na njaa kamwe. Anaonyesha kwamba wanaweza, japo yeye, kama mwanafunzi wa Maandiko, alijua kwmaba njaa inaweza kutumwa na Mungu kuwahukumu waovu.
Utii Na Hekima
Pili – Tunapaswa kuwa watii na kutumia hekima ya Mungu kuepuka kunaswa katika tukio lolote la ghadhabu ya Mungu linalolengwa duniani. Nuhu alijenga safina yake, Lutu alielekea vilimani, Wakristo wa Yerusalemu walitoroka mji wao; wote hao ilibidi kumtii Mungu ili kuepuka kunaswa katika hukumu Yake juu ya waovu.
Kama ningekuwa naishi katika eneo linalokumbwa na vimbunga, ningejenga nyumba yenye nguvu ambayo haiwezi kubomolewa, au nyumba ya bei rahisi ambayo ni rahisi kuijenga tena! Kisha, ningeomba. Kila Mkristo anapaswa kuomba na kuwa msikivu kwa Yule ambaye Yesu aliahidi kwamba “atawajulisha mambo yatakayokuja” (Yohana 16:13), ili aweze kuepuka ghadhabu ya Mungu juu ya dunia.
Tunasoma katika Matendo 11 kuhusu nabii Agabo ambaye alionya juu ya njaa kubwa ambayo ingewaathiri Wakristo waliokaa Uyahudi. Matokeo ni kwamba Paulo na Barnaba walianza kukusanya sadaka ili kuwasaidia (ona Matendo 11:28-30).
Je, mambo kama hayo yanaweza kutokea leo? Hakika, maana Roho Mtakatifu hajabadilika, wala upendo wa Mungu haujapungua. Ila, ni bahati mbaya sana kwamba baadhi ya watu katika mwili wa Kristo siku hizi hawako wazi kwa karama na madhihirisho ya aina hiyo ya Roho Mtakatifu, na kwa sababu hiyo, “wanamzimisha Roho” (1Wathes. 5:19) na kukosa mambo bora ya Mungu.
Katika kitabu kuhusu maisha yake, Marehemu Demos Shakarian, mkuu na mwanzilishi wa huduma ya Full Gospel Businessmen, anaeleza jinsi ambavyo Mungu alizungumza na Wakristo waliokaa nchi ya Armenia mwishoni mwa miaka ya 1800, kwa kupitia nabii mvulana aliyekuwa hajui kusoma wala kuandika. Aliwaonya juu ya mauaji makubwa yanayokuja, na matokeo ni kwamba, Wakristo Wapentekoste ambao waliamini mambo ya namna hiyo walikimbia nchi, pamoja na babu zake Shakarian. Muda mfupi baadaye, Waturuki walivamia Armenia, na WaArmenia zaidi ya milioni moja waliuawa, ikiwa ni pamoja na wale Wakristo waliokataa kusikia maonyo ya Mungu.
Tutakuwa na busara sana tukidumu kuwa wasikivu kwa Roho Mtakatifu na kumtii Mungu, la sivyo tutajikuta tunapitia katika ghadhabu ya Mungu ambayo Yeye hakutaka tuipitie. Kuna wakati Elisha alimwambia mwanamke mmoja hivi: “Ondoka, ukaende wewe na jamaa yako, ukae hali ya kigeni utakakoweza kukaa; kwa sababu BWANA ameiita njaa; nayo itakuja juu ya nchi hii muda wa miaka saba” (2Wafalme 8:1). Ingekuwaje kama huyo mwanamke angepuuzia ushauri wa nabii?
Tunasoma katika kitabu cha Ufunuo onyo la ajabu sana kwa watu wa Mungu, kwamba watoke “Babeli” wasije wakanaswa katika hukumu ya Mungu juu yake.
Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni ikisema, ‘Tokeni kwake [Babeli] enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake … Kwa sababu hiyo mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti na huzuni na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana Bwana Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu (Ufunuo 18:4, 5, 8. Maneno mepesi kukazia).
Tunapohitimisha, tuseme hivi: Mungu ni mwenyezi – anatawala hali ya hewa na majanga. Amejithibitisha Mwenyewe kama Bwana juu ya nguvu za asili katika Biblia – kuanzia kusababisha mvua siku arobaini wakati wa Nuhu, hadi aliponyesha mvua yam awe pamoja na kutuma mapigo mengine juu ya adui za Israeli, hadi kusababisha kwake upepo mkali dhidi ya merikebu ya Yona, hadi kukemea Kwake ile tufani katika Bahari ya Galilaya. Kama Yesu alivyosema, Yeye ni “Bwana wa mbingu na nchi” (Mat hayo 11:25). Ukitaka ushahidi zaidi wa Maandiko kuhusu mamlaka na ukuu wa Mungu juu ya nguvu za asili, angalia katika Yoshua 10:11; Ayubu 38:22-38; Yeremia 5:24; 10:13; 31:35; Zaburi 78:45-49; 105:16; 107:33-37; 135:6, 7; 147:7, 8, 15-18; Mathayo 5:45; Matendo 14:17.
Majibu Kwa Maswali Machache
Kama Mungu anawahukumu watu kwa njia ya njaa, gharika na matetemeko, je, ni makosa kwetu sisi kama wawakilishi wa Mungu, kusaidia na kupunguza makali ya mateso ya wale watu ambao Mungu anawahukumu?
Hapana, kamwe. Tunapaswa kutambua kwamba Mungu anampenda kila mtu, pamoja na wale watu anaowahukumu. Japo litashangaza masikio yetu, hukumu Yake kwa njia ya majanga ni onyesho la upendo Wake. Inawezekanaje? Ni hivi: Kupitia matatizo na magumu ambayo yanaletwa na majanga, Mungu anawaonya watu anaowapenda kwamba Yeye ni mtakatifu na mwenye kuhukumu, na kwamba kuna malipo kwa ajili ya dhambi. Mungu anaruhusu mateso ya muda ili kuweza kuwasaidia watu waamke na kuona hitaji lao la Mwokozi – ili waepuke ziwa la moto. Huo ni upendo!
Muda wote ambapo watu wanapumua, Mungu bado anawaonyesha rehema wasiyostahili, na unakuwepo bado wakati wao kutubu. Kupitia huruma yetu na msaada, tunaweza kuonyesha upendo wa Mungu kwa watu wanaopitia ghadhabu Yake ya muda, lakini ambao wanaweza kuokoka na ghadhabu Yake ya milele. Majanga ni nafasi nzuri tu za kuwafikia watu wa dunia ambao Yesu aliwafia.
Je! Kitu muhimu kuliko vyote maishani si kuwafikishia watu ujumbe wa Injili? Tunapokuwa na mtazamo wa milele, mateso ya wale walionaswa katika majanga si kitu ukilinganisha na mateso ya wale watakaotupwa katika ziwa la moto.
Ni kweli pia kwamba watu huwa wasikivu kwa Injili wanapokuwa katika mateso. Kuna mifano mingi sana katika Biblia kuhusu ajabu hii, kuanzia toba ya Israeli wakati wa mateso kutoka kwa mataifa jirani, mpaka habari ya Yesu kuhusu mwana mpotevu. Wakristo wanapaswa kutazama majanga kama nyakati ambapo mavuno yamekwisha kuiva, tayari kuvunwa.
Hebu Tuseme Ukweli
Sasa – ujumbe wetu uweje, kwa watu wanaojaribu kurejelea hali ya kawaida kimaisha baada ya kimbunga au tetemeko? Tutawajibuje kama watataka jibu la kitheolojia kuhusu yaliyowapata? Hebu tuseme kweli inayofundishwa na Biblia, na kuwaambia watu kwamba Mungu ni mtakatifu na kwamba dhambi yao ina malipo. Tuwaambie kwamba ile kelele kubwa sana ya kimbunga ni mfano mdogo tu wa nguvu ambazo Mwenyezi Mungu anazo, na hofu waliyosikia wakati nyumba yao ilipotikiswa si kitu ukilinganisha na hofu itakayowashika watakapotupwa jehanamu. Na, tuwaambie kwamba, ingawa sisi sote tunastahili kutupwa jehanamu, Mungu anaturehemu na kutupa sisi muda wa kutubu na kumwamini Yesu, ambaye kwa njia Yake tutaokolewa na ghadhabu ya Mungu.
Wengine watasema, “Tusiwatishe watu kuhusu Mungu.” Jibu linatoka katika Maandiko, hivi: “Kumcha Bwana ni mwanzo wa maarifa” (Mithali 1:7). Watu wasipomcha (au kumwogopa, kumheshimu) Mungu, hawajui kitu chochote.
Itakuwaje Kama Watu Watamkasirikia Mungu?
Je, watu hawatamkasirikia Mungu kwa sababu ya mateso yao? Labda, lakini tunahitaji kuwasaidia waone kiburi chao, kwa upole. Hakuna mwenye haki ya kumlalamikia Mungu kwa mambo anayomtendea, kwa sababu sote tunastahili kutupwa katika ziwa la moto tangu zamani. Badala ya kumlaani Mungu kwa yanayowapata, watu wanatakiwa kumsifu kwa kuwapenda kiasi hicho, cha kuwaonya. Mungu ana kila haki ya kumpuuza kila mtu, na kuwaacha wote wafuate njia zao wenyewe kuelekea jehanamu. Lakini Mungu anawapenda watu, Naye anawaita kila siku. Anawaita kimya kimya kwa maua yanayochanua kwenye miti ya matunda, kwa nyimbo za ndege, kwa ukuu wa milima, na kwa kung’aa kwa nyota nyingi kila siku. Anawaita kupitia dhamiri zao, kupitia mwili Wake yaani Kanisa, na kwa njia ya Roho Mtakatifu. Lakini, wanapuuza mwito Wake.
Kwa hakika si mapenzi ya Mungu kwa watu kuteseka, lakini wanapoendelea kumpuuza, anawapenda kiasi cha kutosha kutumia njia zingine kali zaidi ili kuwafanya wamsikilize. Vimbunga, matetemeko, gharika, na njaa ni baadhi ya njia zingine kali. Mungu hutazamia kwamba majanga kama hayo yatashusha viburi vya watu na kuwafikisha mahali pa kuwa na akili ya kuelewa.
Je, Mungu Anakuwa Hajatenda Haki?
Tunapomtazama Mungu na dunia yetu kwa mtazamo wa KiBiblia, hapo ndipo tunapokuwa tukifanya sahihi. Mtazamo wa KiBiblia ni kwamba kila mtu anastahili ghadhabu ya Mungu, ila, Yeye ni mwenye rehema. Wakati watu wanaoteseka wanaposema kwamba wanatazamia kutendewa vizuri zaidi na Mungu kuliko inavyokuwa wakati huo, Mungu hujisikia vibaya. Ni kwamba kila mtu anapokea rehema nyingi zaidi sana kuliko anavyostahili.
Katika kufafanua zaidi jambo hili, Yesu wakati mmoja alisema kitu kuhusu majanga mawili yaliyotokea katika siku Zake. Tunasoma hivi katika Injili ya Luka:-
Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao. Akawajibu akawaambia, ‘Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo. Lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo. Lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo’ (Luka 13:1-5).
Ni hivi: Wagalilaya waliokufa kwa mkono wa Pilato wasingeweza kusema, “Mungu hajatutendea haki, maana hajatuokoa na Pilato!” Hapana. Wao walikuwa wenye dhambi waliostahili kufa. Tena, kulingana na Yesu, wale Wagalilaya waliopona wangekosea sana kama wangefikia uamuzi kwamba wao hawana dhambi nyingi sana kama jirani zao waliouawa. Hawakuwa wamefanya kazi ili kupata upendeleo mkubwa kutoka kwa Mungu – ni kwamba walipewa rehema zaidi.
Ujumbe wa Kristo ulikuwa wazi kabisa: “Ninyi nyote ni wenye dhambi. Dhambi ina matokeo yake. Kwa sasa, mnaishi kutokana na rehema za Mungu. Basi, tubuni kabla muda haujawaishia na ninyi.”
Akamalizia maelezo Yake kuhusu majanga hayo kwa kutoa mfano juu ya rehema za Mungu, kama ifuatavyo:
Akanena mfano huu: Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate. Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, ‘Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu. Uukate, mbona hata nchi unaiharibu?’ Akajibu akamwambia, ‘Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La usipozaa, ndipo uukate’ (Luka 13:6-9).
Hapa, haki na rehema za Mungu vinaonekana. Haki ya Mungu inasema, “Ukate mti usio na faida!” Lakini rehema Zake zinasema, “Hapana! Upe muda zaidi wa kuzaa matunda.” Kila mtu asiye na Kristo ni kama mti huo.
Je, Tunaweza Kukemea Vimbunga Na Gharika?
Swali moja la mwisho kuhusu majanga. Hivi, tukiwa na imani ya kutosha, hatuwezi kukemea na kuzuia majanga kutokea?
Kuna na imani maana yake kuamini mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa. Basi, imani lazima ijengwe juu ya Neno la Mungu. Bila hivyo inakuwa si imani, bali ni tumaini au tarajio tu. Katika Biblia, hatupati mahali penye kutuahudi kwamba tunaweza kukemea na kutuliza vimbunga. Basi, hakuna jinsi mtu anavyoweza kuwa na imani ya kufanya hivyo (isipokuwa kama Mungu atampa imani hiyo kwa enzi Yake na mamlaka Yake).
Tufafanue zaidi. Njia ya pekee ya mtu kuwa na imani ya kukemea kimbunga ni kama ana uhakika kwamba Mungu hatai kimbunga hicho kipige eneo fulani. Kama tulivyojifunza katika Maandiko, Mungu ndiye mwenye kutawala upepo, Naye anahusika kabisa na vimbunga. Basi, ni kitu kisichowezekana kwa mtu kuwa na imani thabiti kwamba anaweza kuzuia kimbunga wakati Mungu Mwenyewe ameagiza kiwepo. Labda tofauti kwa hilo ni kama Mungu angebadilisha mpango Wake juu ya kimbunga hicho, ambayo inawezekana kama itikio Lake kuhusu maombi ya mtu kwamba awe na rehema, au itikio Lake kwa t oba ya watu wale ambao alikuwa anataka kuwahukumu (habari za Ninawi katika siku za Yona ni mfano rahisi). Lakini, hata kama Mungu angebadilisha mawzo Yake, bado si rahisi mtu awe na imani ya kukemea na kutuliza kimbunga bila mtu huyo kujua kwamba Mungu kabadilisha mawazo Yake na pia kwamba Mungu alitaka yeye akemee na kuzuia kimbunga hicho.
Mtu pekee aliyekemea na kuzuia upepo mkali alikuwa Yesu. Njia ya pekee kwetu sisi kufanya hivyo ni kama Mungu angetupa “karama ya imani” (au karama ya “imani maalum” kama inavyoitwa wakati mwingine), ambayo ni mojawapo katika zile karama tisa za Roho zinazotajwa katika 1Wakorintho 12:7-11. Sawa na karama zingine zote za kiroho, karama ya imani hutenda kazi kama Roho apendavyo, si kama sisi tupendavyo (ona 1Wakor. 12:11). Basi, Mungu asipokupa wewe imani maalum ya kukemea kimbunga kinachokuja, usisimame katika njia yake, ukijifanya kwamba unatenda hivyo kwa imani. Ondoka njiani – kipishe kabisa! Pia, omba ulinzi wa Mungu na umwombe awe na rehema kwa watu wale wanaohukumiwa, ukimwomba aponye maisha yao ili wapate muda zaidi wa kutubu.
Tazama: Wakati Paulo alipokuwa amefungwa kwenye merikebu kuelekea Rumi, na merikebu hiyo ikasukumwa na tufani kali baharini kwa majuma mawili, hakukemea ili bahari itulie (Matendo 27:14-44). Ni kwa sababu asingeweza. Ona pia kwamba Mungu aliwahurumia watu wote waliokuwa merikebuni, maana wote 276 waliokoka baada ya merikebu kuvunjika (ona Matendo 27:24, 34, 44). Ni dhahiri kwamba Mungu aliwahurumia kwa sababu Paulo alimwomba awahurumie.
[1] Hoja mbili pinzani zinajibiwa hivi: (1) Yuda anataja mashindano kati ya Mikaeli na Shetani juu ya mwili wa Musa, lakini hakuna vita inayotajwa. Tunachoambiwa na Yuda ni kwamba Mikaeli “hakuthubutu hata kumshtaki kwa kumlaumu [Shetani], bali alisema, ‘Bwana na akukemee’ “ (Yuda ms. 9). (2) Wakati Elisha na mtumishi wake walipozungukwa na jeshi la Shamu katika mji wa Dothani, Elisha alimwomba Mungu afungue macho ya mtumishi wake (2Wafalme 6:15-17). Basi, mtumishi wake akaona “farasi na magari ya moto” ambayo ni sawa tukisema yalikuwa yamepandwa na kuongozwa na jeshi la malaika katika ulimwengu wa roho. Lakini, huo si ushahidi kwamba walikuwa wamejiandaa kupambana na majeshi ya pepo. Wakati mwingine malaika hutumiwa na Mungu kutekeleza hasira Yake dhidi ya binadamu waovu, kama ilivyoandikwa katika 2Wafalme 19:35, ambapo malaika mmoja tu aliua askari 185,000 wa Ashuri.
[2] Baadhi ya mifano hiyo ni Mathayo 1:20; 2:13, 19; 4:11; Luka 1:11-20, 26-38.
[3] Fungu hili zima pia ni ushahidi kwamba Ayubu “hakumfungulia Shetani mlango kwa sababu ya hofu yake,” kitu kinachoaminiwa na wengine. Mungu Mwenyewe alimwambia Shetani hivi kuhusu Ayubu, katika 2:3 – “Naye [Ayubu] hata sasa anashikamana na utimilifu wake, ujapokuwa ulinichochea juu yake, ili nimwangamize pasipokuwa na sababu” (maneno mepesi kukazia).
[4] Ona pia 1Wakorintho 10:13, mahali panapo-onyesha kwamba Mungu huweka mipaka ya kujaribiwa kwetu. Hiyo inamaanisha kwamba humwekea mipaka mwenye kutujaribu pia!
[5] Je, maana yake ni kwamba tusiwaombee viongozi wa kiserikali, au tusipige kura kwa kuwa tunajua Mungu humwinua yeyote amtakaye kuwa juu yetu? Hapana. Katika demokrasia, hasira ya Mungu iko ndani kwa ndani. Tunampata tunayemchagua, na watu waovu kwa kawaida huchagua waovu wenzao. Kwa sababu hii, wenye haki wanapaswa kupiga kura. Tena, katika Agano la Kale na Jipya, tunashauriwa kuwaombea viongozi wetu wa kiserikali (Yeremia 29:7; 1Timo. 2:1-4). Maana yake ni kwamba tunaweza kumshawishi Mungu anapofanya maamuzi Yake juu ya nani atawale. Kwa kuwa hukumu ya Mungu wakati mwingine huja kwa kupitia viongozi waovu wa serikali, na kwa sababu mataifa mengi yanastahili hukumu hata hivyo, tunaweza kuomba na kupata reheme Zake, ili nchi yetu isipatikane na kila kitu inachostahili kupata.
[6] Maandiko mengine yenye kuthibitisha kwamba Mungu anatawala upepo ni haya: Mwanzo 8:11; Kutoka 10:13, 19; 14:21; 15:10; Hesabu 11:31; Zaburi 48:7; 78:76; 135:7; 147:18; 148:8; Isaya 11:15; 27:8; Yeremia 10:13; 51:16; Ezekieli 13:11, 13; Amosi 4:9, 13; Yona 4:8; Hagai 2:17. Katika hiyo mifano mingi, Mungu alitumia upepo kama kifaa cha kuhukumu.
[7] Ukitaka kusoma zaidi kuhusu Mungu kuleta njaa, angalia Kumbu. 32:23, 24; 2Samweli 21:1; 24:12, 13; 2Wafalme 8:1; Zaburi 105:16; Isaya 14:30; Yeremia 14:12, 15, 15; 16:3, 4; 24:10; 27:8; 34:17; 42:17; 44:12, 13; Ezekieli 5:12, 16, 17; 6:12; 12:16; 14:21; 36:29; Ufunuo 6:8; 18:8). Yesu Mwenyewe alisema kwamba Mungu “hunyesha mvua juu ya wenye haki na waovu” (Mathayo 5:45). Mungu anatawala mvua!