Katika sura iliyotangulia kuhusu Mahubiri ya Yesu Mlimani, tulitazama baadhi ya maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi Wake kuhusu uwakili, au, usimamizi wa mali. Aliwaambia wasijiwekee hazina duniani, bali mbinguni. Akaonyesha ujinga wa wale wanaoshughulika na kujiwekea hazina mali za muda, pamoja na giza lililoko mioyoni mwao (ona Mathayo 6:19-24).
Fedha ni mungu kweli kwa wale wanaoweka hazina duniani, kwa sababu wanaitumikia, na itawala maisha yao. Yesu alitangaza kwamba haiwezekani kumtumikia Mungu na fedha, akionyesha wazi kwamba kama Mungu ni Bwana wetu kweli, basi ni Bwana wa fedha zetu pia. Fedha hushindana na Mungu kuteka mioyo ya watu, kuliko kitu kingine chochote. Bila shaka ndiyo sababu Yesu alifundisha kwamba hatuwezi kuwa wanafunzi Wake tusipotoa mali zetu zote (ktk Luka 14:33). Wanafunzi wa Kristo hawana kitu chochote. Wao ni wasimamizi tu wa kile ambacho ni mali ya Mungu, na Mungu hupenda kufanya vitu kwa fedha Zake, vinavyo-onyesha tabia Yake na kuendeleza ufalme Wake.
Yesu alisema mengi sana kuhusu uwakili au usimamizi wa mali, lakini inaonekana maneno Yake hupuuzwa mara nyingi na watu wanaodai kuwa wafuasi Wake. Wanachokipenda zaidi ni kubadili Maandiko ili kutengeneza “fundisho la mafanikio” la kisasa na namna zake nyingi, fundisho ambalo ni uongo na potofu. Ila, mtumishi anayefanya wengine kuwa wanafunzi, hutamani kuwafundisha watu kuyatii maagizo yote ya Kristo. Basi atafundisha uwakili au usimamizi wa mali KiBiblia, kwa mfano wa maisha yake na kwa maneno yake.
Hebu tutazame Maandiko yanafundisha nini kuhusu uwakili na usimamizi wa mali, na hapo hapo tuweke wazi baadhi ya mafundisho ya kisasa ambayo ni ya uongo kuhusu mafanikio. Hapa ni kwa kifupi tu, maana somo hili ni pana mno.
Mtoaji Wa Mahitaji
Tuanze vizuri. Bila shaka tunakumbuka kwamba Paulo, akiongozwa na Roho Mtakatifu, aliandika hivi: “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu” (Wafilipi 4:19). Ahadi hiyo maarufu husemwa sana na Wakristo, lakini, mantiki yake ni nini? Tukiisoma katika mantiki yake, tunagundua upesi sababu ya Paulo kuwa na ujasiri kiasi hicho kwamba Mungu angewapa Wafilipi mahitaji yao yote.
Lakini mlifanya vema, mlifanya vema, mliposhiriki nami katika dhiki yangu. Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa katika mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu. Kwa kuwa hata huko Thesalonike mliniletea msaada kw amahitaji yangu, wala si mara moja. Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali nayatamani mazao yanayozidi kuwa mengi, katika hesabu yenu. Lakini ninavyo vitu vyote na kuzidi, tena nimejaa tele; nimepokea kwa mkono wa Epafrodito vitu vile vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo Mungu. Na Mungu wangu atawajezeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu (Wafilipi 4:14-19. Maneno mepesi kukazia).
Paulo alikuwa na hakika kwamba Yesu angetimiza mahitaji ya Wafilipi kwa kuwa walikuwa wametimiza masharti ya Yesu. Walitafuta kwanza ufalme wa Mungu, kitu kilichothibitishwa kwa kumpa Paulo sadaka za kujitoa sana ili aweze kuendelea na shughuli ya kuanzisha makanisa. Katika Mahubiri Yake Mlimani, Yesu alisema hivi:
Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo mengine yote mtazidishiwa (Mathayo 6:32-33).
Basi, tunaona kwamba ahadi ya Paulo katika Wafilipi 4:19 haimhusu kila Mkristo anayesema na kupendezwa nayo. Badala yake inawahusu wale tu wanaotafuta kwanza ufalme wa Mungu.
Je, Tunahitaji Nini?
Kuna kitu kingine tunachoweza kujifunza kutokana na ahadi ya Yesu katika Mathayo 6:32, 33. Mara nyingi tunapata shida kutofautisha mahitaji yetu na matakwa. Yesu alifafanua mahitaji yetu ni nini aliposema, “Baba yenu wa mbinguni anajua kwamba mnahitaji hayo yote.”
“Hayo yote” ambayo Yesu anayataja kwamba yataongezwa kwa watakaotafuta kwanza ufalme Wake na haki ni yapi? Ni chakula, kinywaji na mavazi. Hakuna awezaye kupinga hilo kwa sababu hayo ndiyo Yesu aliyotaja kabla ya kutaja ahadi tunayotazama (ktk Mathayo 6:25-31). Chakula, kinywaji na mavazi ndiyo mahitaji yetu ya msingi. Tena, hivyo ndivyo vitu peke yake ambavyo Yesu na wanafunzi Wake walikuwa navyo wakati wakizunguka na kuhubiri.
Yaonekana Paulo alikubaliana pia na tafsiri ya Yesu kuhusu mahitaji yetu, maana alimwandikia hivi Timotheo:
Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi (1Timo. 6:6-10. Maneno mepesi kukazia).
Paulo aliamini kwamba chakula na mavazi ndiyo mahitaji yetu yote, vinginevyo asingesema kwamba tunapaswa kuridhika na hivyo. Hilo linatupelekea kuwa na mtazamo tofauti kidogo kuhusu ile ahadi yake kwa Wafilipi, kwamba Mungu angewapa mahitaji yao yote! Ukiwasikiliza wahubiri wengine wanapofafanua andiko hilo, utadhani linasema hivi: “Mungu wangu atawapa kila mnachokitamani!” Tena, ikiwa tunapaswa kuridhika na chakula na mavazi tu, mbona haturidhiki zaidi na vitu tulivyo navyo, ambavyo kwa wengi wetu ni zaidi ya chakula na mavazi?
Kutoridhika
Tatizo letu ni kwamba, tunadhani tunahitaji zaidi ya mahitaji yetu. Hebu fikiri kweli kwamba, wakati Adamu na Hawa walipoumbwa na Mungu, hawakuwa na chochote, lakini waliishi paradiso. Mungu hakukusudia sisi tupate furaha yetu kutokana na kukusanya vitu. Je, umewahi kufikiri kwamba Yesu hakuwahi kufungua bomba la maji, wala kuoga kwa maji yanayomwagka kutoka juu katika bafu? Hakuwahi kufua nguo Zake kwa mashine ya kufulia; hakuwahi kufungua friji. Hakuwahi kuendesha gari wala baiskeli. Hakuwahi kusikiliza redio, hakusema na mtu kwa simu, hakuwahi kupika chakula kwenye jiko, wala kuhubiri kwa kutumia kipaza sauti. Yeye hakuwahi kuangalia sinema wala video wala televisheni. Hakuwahi kuwasha taa ya umeme, au kupigwa na baridi ya kiyoyozi. Hakuwa na saa ya mkononi. Hakuwa na kabati lililojaa nguo. Tujiulize hivi: Aliwezaje kuwa na furaha?
Siku hizi tunasukumiwa matangazo mengi kwa njia mbalimbali, yenye kutuonyesha jinsi watu walivyo na furaha wanapofurahia mali zao mpya. Basi, akili zetu zinaingiziwa mawazo kwamba furaha hutokana na kujipatia zaidi, na hata kama tunapata vingapi, bado haturidhiki. Hicho ndicho kitu Yesu alichoita “udanganyifu wa mali” (Mathayo 13:22). Vitu huahidi furaha, lakini havileti. Na sisi tunapojiunga katika mbio za dunia hii za kujipatia vitu vingi, tunajikuta tumefikia kwenye kuabudu sanamu – tunakuwa watumwa wa mali – wanaomsahau Mungu na amri Zake muhimu sana za kumpenda kwa moyo wote na kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda wenyewe. Mungu alionya kuhusu jambo hilo alipozungumza na Waisraeli, hivi:
Jihadhari, usije ukamsahau BWANA, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake, ninazokuamuru leo. Angalia, utakapokuwa umekula na kushiba, na kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake;na makundi yako ya ng’ombe na kondoo yatakapo-ongezeka, na fedha yako na dhahabu yako itakapo-ongezeka, na kila kitu ulicho nacho kitakapo-ongezeka; basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau BWANA, Mungu wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa (Kumbu. 8:11-14).
Vivyo hivyo, Yesu pia alionya kwamba “udanganyifu wa mali” ungeweza kuzima uhai wa kiroho wa mwamini wa kweli anayekubali kupotoshwa (ona Mathayo 13:7, 22). Paulo alionya kwamba “kupenda fedha ni shina la maovu yote,” na kwamba “wengine kwa kuitamani hiyo wamekwenda mbali na imani, na kujichoma kwa maumivu mengi” (1Timo. 6:10). Tunashauriwa na mwandishi wa kitabu cha Waebrania hivi: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa Yeye Mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa” (Waebrania 13:5). Hiyo ni mistari michache tu yenye kutoa maonyo kuhusu hatari ya mali.
Fedha Zinapokuwa Bwana
Hakuna kipimo bora cha mahusiano yetu na Mungu kama jinsi tunavyoshughulika na fedha. Fedha – muda na njia tunazotumia kuipata, na kile tunachofanya nayo tukiisha ipata – hudhihirisha mengi kuhusu maisha yetu ya kiroho. Fedha huleta majaribu mengi sana tunapokuwa nayo, na tunapokuwa hatuna pia. Fedha inaweza kusimama kinyume kabisa na zile amri kuu mbili, kwa sababu inaweza kuwa mungu juu ya Mungu Mwenyewe, na inaweza kutushawishi kujipenda sisi zaidi na kuwapenda majirani kidogo sana. Kwa upande mwingine, fedha inaweza kutumiwa kama njia ya kuthibitisha upendo wetu kwa Mungu kwa jirani zetu.
Kuna wakati Yesu alitoa mfano juu ya mtu aliyeruhusu fedha kumtawala, badala ya kumruhusu Mungu.
Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi: nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulviyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe! Usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu (Luka 12:16-21).
Yesu alimwonyesha huyu tajiri kwamba ni mpumbavu sana. Japo alikuwa amebarikiwa na afya nzuri, ardhi yenye rutuba na ufundi wa kilimo, hakumjua Mungu maana angemjua, asingehifadhi ziara aliyopata na kujipumzisha kwa maisha ya starehe na anasa. Badal ayake, angemtafuta Mungu kwamba afanye nini na baraka zake, akijua kwamba yeye ni msimamizi tu wa mali za Mungu. Bila shaka Mungu angemtaka agawe ziada yake na kuendelea kufanya kazi ili aweze kuendelea kugawa ziada yake. Pengine kitu pekee ambacho kingekubalika kama mbadala ni yeye aache kulima na aingie katika huduma ya namna fulani, kama Mungu angemwita kufanya hivyo.
Yule mkulima tajiri katika mfano wa Yesu alikosea mahesabu kwa hali ya juu sana, kuhusu tarehe ya kufa kwake. Yeye alidhani ana miaka mingi bado, kumbe alikuwa amebakiza masaa tu aingie katika umilele. Hoja ya Yesu ni hii: Tunapaswa kuishi kila siku kana kwamba ndiyo ya mwisho kwetu, tukiwa tayari kusimama mbele za Mungu ili kutoa hesabu ya maisha yetu.
Mitazamo Miwili
Mtazamo wa Mungu ni tofauti kabisa na ule wa mwanadamu! Labda yule tajiri katika mfano wa Yesu alikuwa mtu wa kuonewa wivu na watu wote waliomfahamu, lakini kumbe Mungu alikuwa anamhurumia. Alikuwa tajiri machoni pa wanadamu, lakini mbele za Mungu alikuwa maskini. Angeweza kujiwekea hazina mbinguni, mahali ambapo ingekuwa yake milele, lakini yeye akachagua kujiwekea hapa duniani, ambapo haikuwa na faida kwake baada ya kufa. Na, kutokana na mafundisho ya Yesu kuhusu watu wenye choyo (au tamaa), sidhani kama Yesu alitaka tuone kwamba huyo mtu alikwenda mbinguni baada ya kufa.
Mfano huu unapaswa utusaidie sote kukumbuka kwamba kila kitu tulicho nacho ni zawadi tu kutoka kwa Mungu, naye anatutazamia tuwe wasimamizi waaminifu. Maana yake si kwa wale tu wenye mali, bali kwa kila mtu na yeyote atakayejaribiwa kufanya vitu kuwa muhimu sana. Yesu aliliweka hilo wazi alipoendelea kuzungumza na wanafunzi Wake.
Kwa sababu hiyo nawaambia [yaani, atakachosema kimejengwa juu ya aliyokwisha kusema], Msisumbuke maisha yenu, mtakula nini; wala miili yenu, mtavaa nini. Kw akuwa maisha ni zaidi ya chakula, na mwili ni zaidi ya mavazi. Watafakarini kunguru, ya kwamba hawapandi wala hawavuni; hawana ghala wa uchaga, na Mungu huwalisha. Bora ninyi mara nyingi kuliko ndege! Na yupi kwenu ambaye akijisumbua awez akujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Basi, ikiwa hamwezi hata neno lililo dogo, kwa nini kujisumbua kwa ajili ya yale mengine? Yatafakarini maua jinsi yameavyo; hayatendi kazi wala hayasokoti; nami nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huvika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo na kesho hutupwa kalibuni, je, hatawatendea ninyi zaidi, enyi wa imani haba? Ninyi msitafute mtakavyokula wala mtakavyokunywa; wala msifanye wasiwasi, kwa maana, hayo yote ndiyo watafutayo mataifa ya duniani, lakini Baba yenu anajua ya kuwa mna haja na hayo. Bali utafuteni ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa. Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme. Viuzeni mlivyo navyo, mtoe sadaka. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia mwivi, wala nondo haharibu. Kwa kuwa hazina yenu ilipo, ndipo itakapokuwapo na mioyo yenu (Luka 12:22-34).
Hayo maneno ya Yesu yako kinyume kabisa na mahubiri ya “mafanikio” ya kisasa! Siku hizi tunaambiwa kwamba Mungu anataka tupate zaidi na zaidi. Yesu aliwaambia wanafunzi Wake wauze walivyokuwa navyo tayari na kuwapa maskini! Hapa tena aliweka wazi upumbavu wa wale wanaojiwekea hazina zao duniani – mahali ambapo hazina hizo zimelengwa kuangamia tu, na mahali ambapo mioyo ya wenya hazina hizo ilipo.
Ona kwamba Yesu analifafanua somo la tajiri mpumbavu kwa wale waliokuwa na kidogo sana kiasi cha kujaribiwa kufikiri sana juu ya chakula na mavazi. Kuwa na wasiwasi kuhusu vitu kama hivyo huonyesha kwamba mtazamo wetu ni wa makosa. Kama tutamwamini Baba yetu anayejali kama inavyopasa, hatupaswi kuwa na wasiwasi; na hali hiyo ya kutokujali inatufungua ili tuelekeze macho yetu kwenye kuujenga ufalme wa Mungu.
Mfano Wa Kristo
Yesu alisema mengi kuhusu fedha. Ila, alifundisha – kama kila mtumishi anayefanya watu kuwa wanafunzi – kwa mfano wa maisha Yake Mwenyewe. Alihubiri kitu alichotenda Mwenyewe. Je, Yesu aliishije?
Yesu hakulundika mali za duniani, japo angeweza kutumia hali Yake na kuwa tajiri mno. Watumishi wengi wenye vipawa wamedhani – kwa makosa – kwamba, kama huduma zao zinasababisha fedha kuja kwao, bila shaka Mungu anawataka wawe matajiri. Yesu hakutumia upako Wake kwa ajili ya kufaidika kibinafsi. Fedha aliyopewa ilitumika kufanya watu kuwa wanafunzi. Hata aligharimia mahitaji ya kundi alilosafiri nalo, waliokuwa wanajifunza kutoka Kwake.[1] Katika siku zetu, wanafunzi vijana lazima wajilipie ili waweze kufundishwa na watumishi wazee katika vyuo vya Biblia. Yesu alionyesha tofauti!
Pia, Yesu aliishi maisha ya imani, akiamini kwamba Baba Yake angempa mahitaji Yake yote na kumbariki, ili Naye aweze kuwapa wengine mahitaji yao. Wakati mwingine alikaribishwa kwenye karamu za chakula, na wakati mwingine tunamwona akila nafaka mbichi shambani (ona Luka 6:1).
Kama mara mbili hivi aliwapa watu maelfu chakula, waliokuwa wamekuja kumsikiliza. Hii ni tofauti kabisa na makongamano ya kisasa ya Kikristo ambapo kila mtu anayetaka kumsikiliza msemaji lazima atoe kiingilio! Sisi wengine tunaotoa mpaka chakula bure kwa watu wanaohudhuria mikutano yetu ya wachungaji tunadhihakiwa kwamba “tunawalipa watu ili watusikilize.” Sivyo, bali tunachofanya ni kufuata mfano wa Yesu tu.
Vile vile, Yesu aliwajali maskini, maana kundi Lake lilikuwa na mfuko ambao ulitumiwa kutoa sadaka. Kuwasaidia maskini kilikuwa kitu cha kawaida kabisa kwa huduma ya Yesu kiasi kwamba, alipomwambia Yuda katika Chakula cha Mwisho kwamba alifanyalo alifanye haraka, wanafunzi wale wengine wote walidhani kwamba Yuda alikuwa ameambiwa akanunue chakula chao, au apeleke fedha kwa maskini (ona Yohana 13:27-30).
Kweli Yesu alimpenda jirani Yake kama nafsi Yake, hivyo, aliishi maisha rahisi tu, na aliwashirikisha watu vitu. Yeye hakuwa na haja ya kutubu kutokana na mahubiri ya Yohana Mbatizaji aliyesema, “Mwenye kanzu mbili ampe moja yeye asiyekuwa nayo” (Luka 3:11). Yesu alikuwa na kanzu moja tu. Lakini, wahubiri wengine wa mafanikio wanajaribu kutushawishi kwamba Yesu alikuwa tajiri sana kwa sababu alivaa kanzu isiyounganishwa popote (ona Yohana 19:23), kitu ambacho huvaliwa na watu matajiri. Inashangaza jinsi mtu anavyoweza kuweka maana kwenye andiko la Biblia kama akitaka kuthibitisha kitu kinachopingana na Maandiko mengine mengi! Nadhani ni vizuri hata tukisema kwamba Yesu alikuwa anajaribu kuficha utajiri Wake – wazo la kijinga – maana hakuvaa vazi la nje lisilounganishwa.
Yesu alisema mengi sana kuhusu fedha – hatuna nafasi ya kutosha kutazama kila kitu. Ila, tutatazama baadhi ya mafundisho ya kawaida ya hao wahubiri wa mafanikio ambao ni wajanja sana na mafundi katika kupindua maandiko ili kuwadanganya wajinga.
“ Mungu Alimtajirisha Sulemani”
Wahubiri wa mafanikio hutumia hili kama kificho cha hali yao ya tamaa. Wanashindwa kukumbuka kwamba Mungu alimpa Sulemani mali kwa sababu. Sababu I hii: Wakati Mungu alipomwahidi Sulemani kwamba angempa ombi lolote, Sulemani aliomba hekima ya kuwatawala watu. Mungu akafurahishwa sana kwamba Sulemani hakuomba mali (pamoja na vitu vingine). Basi, pamoja na hekima Mungu alimpa mali. Ila, Sulemani hakutumia hekima yake toka kwa Mungu kama Mungu alivyokusudia, na akaishia kuwa mpumbavu kuliko watu wote waliowahi kuishi. Angekuwa na hekima, angejali kile alichosema Mungu katika Torati kwa Waisraeli, miaka mingi kabla hajazaliwa.
Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo BWANA, Mungu wako ukaimiliki, na kukaa humo; nawe utakaposema, Nitaweka mfalme juu yangu mfano wa mataifa yote yaliyo kandokando yangu; usiache kumweka yule atakayechaguyliwa na BWANA, Mungu wako, awe mfalme juu yako; umweke mmoja katika ndugu zako awe mfalme juu yako; usimtawaze mgeni juu yako, ambaye si ndugu yako. Ila asifanye farasi wake kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi; kwa kuwa BWANA amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile. Wala asijizidishie wake, ili moyo wake usikengeuke; wala asifanye fedha zake na dhahabu kuwa nyingi mno (Kumbu. 17:14-17).
Hayo ni maandiko mengine ambayo wahubiri wa mafanikio hupuuza, wakifuata mfano wa Sulemani ambaye naye alilipuuza, akaharibikiwa. Halafu – sawa tu na yeye, wanakuwa waabudu sanamu. Kumbuka kwamba moyo wa Sulemani ulipotoshwa kuabudu sanamu kutokana na wake zake wengi – wake ambao aliweza kuwatunza kwa sababu ya jinsi alivyochezea mali yake.
Mungu alikusudia Sulemani atumie utajiri wake kutoka Kwake ili kuwapenda jirani zake kama nafasi yake, bali yeye aliutumia kujipenda mwenyewe. Alijiongezea dhahabu, fedha, farasi, na wake, kinyume kabisa na amri ya Mungu. Hatimaye alioa wake mia saba na kuwa na masuria mia tatu, akiwanyang’anya kabisa wanaume elfu moja nafasi ya kuoa. Badala ya kuwasaidia maskini, Sulemani alijihudumia. Ni ajabu kubwa sana kwamba wahubiri wa mafanikio wanamtumia Sulemani kama mfano kwa Wakristo wa Agano Jipya, ukizingatia ubinafsi wake na kuabudu sanamu kwake. Je, lengo letu si kufanana zaidi na Kristo?
“Mungu Alimtajirisha Ibrahimu, Nasi Tumeahidiwa Baraka Za Ibrahimu”
Hoja hii imetengenezwa kutokana na maneno ya Paulo katika sura ya tatu ya Wagalatia. Tutazame maneno hayo katika mantiki yake, japo wao huyatumia nje yake.
Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa. Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani. Kwa maana wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika yote yalyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye. Ni dhahiri ya kwamba hakuna mtu ahesabiwaye haki mbele za Mungu katika sheria; kwa sababu Mwenye haki ataishi kwa imani. Na torati haikuja kwa imani, bali, Ayatendaye hayo ataishi katika hayo. Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniw akila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Kristo Yesu, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani (Wagalatia 3:8-14. Maneno mepesi kukazia).
“Baraka ya Ibrahimu” ambayo Paulo anazungumzia katika mstari wa 14 ilikuwa ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu kwamba angebariki mataifa yote katika yeye (ambayo Paulo anaitaja katika mstari wa 8), au, kama Paulo anavyofafanua katika mistari ya mbele, katika uzao wa Ibrahimu, yaani Yesu Kristo (Wagalatia 3:16). Kulingana na tulichosoma, Yesu alileta hiyo baraka iliyoahidiwa kwa mataifa yote kwa kulaaniwa na Mungu – kufa kwa ajili ya dhambi za dunia pale msalabani. Hivyo basi, “baraka za Ibrahimu kuwafikilia mataifa” si jambo la Mungu kuwafanya Mataifa kuwa na mali kama Ibrahimu, bali ni kuhusu ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu kwamba angewabariki Mataifa kupitia uzao wake – na kutimizwa kwake na Yesu kwa njia ya kufa Kwake msalabani kwa ajili yao. (Kiini cha hoja ya Paulo hapo ni kwamba Mataifa wanaweza kuokolewa kwa imani – kama Wayahudi tu – kupitia kumwamini Yesu.)
Upotoshaji Mwingine
Fungu hili hutumiwa wakati mwingine kwa njia nyingine na hao wahubiri ili kuunga mkono itikadi yao. Wanasema kwamba, kwa kuwa Torati iliwaahidi wasioishika laana ya umaskini (ona Kumbu. 28:30, 31, 33, 38-40, 47, 48, 51, 68), na kwa sababu Paulo aliandika kwamba “Kristo alitukomboa kutokana na laana ya Torati” katika Wagalatia 3:13, basi sisi tulio ndani ya Kristo tumekombolewa kutokana na laana ya umaskini.
Kwanza – Hakuna uhakika kwamba Paulo alikuwa anafikiria kuhusu zile laana zinazotajwa katika Kumbukumbu la Torati 28 alipoandika juu ya “laana ya Torati” ambayo sisi tumekombolewa nayo na Kristo. Pengine Paulo alikuwa anaonyesha kwamba Torati nzima ilikuwa ni laana kwa wale waliojaribu kupata wokovu kwa kuitimiza. Tukiisha kombolewa na Kristo, hatuwezi tena kufanya kosa la kujaribu kujiokoa kwa kuishika Torati. Basi kwa hali hiyo kweli tunakuwa tume”kombolewa kutokana na laana ya Torati.”
Kama Paulo kweli alimaanisha kwamba Kristo ametukoboa kutokana na kila kitu kibaya kilichoandikwa katika Kumbukumbu sura ya 28, na kwa njia hiyo kutuhakikishia kwamba tunaingia katika mafanikio ya kupata vitu, inashangaza kwetu basi kwamba yeye mwenyewe aliandika hivi juu ya maisha yake: “Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao” (1Wakor. 4:11). Vile vile inashangaza kwamba aliandika hivi:
Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je ni dhiki aus hida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikw aya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa (Warumi 8:35, 36).
Si sawa kudhani kwamba Paulo angeandika maneno hayo kama Wakristo wote wameondokana na mateso, njaa, uchi, hatari au upanga kwa sababu ya Kristo kuwa ametukomboa kutokana na laana ya Torati.
Vile vile inabidi tushangazwe na maelezo ya Yesu kuhusu tukio la mbinguni lifuatalo.
Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena, ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na mfalme atajibu, akiwaambia, Amini nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi (Mathayo 25:34-40. Maneno mepesi kukazia).
Hakuna shaka basi kwamba baadhi ya waamini ambao wamekombolewa “kutoka laana ya Torati” watajikuta katika mazingira ambayo si ya mafanikio sana. Ila, tazama kwamba katika hayo mazingira magumu ambayo Yesu anaeleza, Mungu alikutana na mahitaji ya waamini hao wanaoteseka, tena kupitia waamini wengine waliokuwa na vitu vingi kuliko walivyohitaji. Tutazamie siku zote kwamba Mungu atakutana na mahitaji yetu, hata kama kwa muda itaonekana kama si hivyo.
Mwisho – hao wahubiri wa mafanikio wanaotaka kuwa matajiri kama Ibrahimu wanapaswa kujiuliza kwa dhati kabisa kama kweli watakuwa tayari kuishi katika hema bila umeme wala maji, maisha yao yote! Wale waliobarikiwa na Mungu kwa mali kiasi fulani katika Agano la Kale walitazamiwa kutumia mali yao kwa ajili ya utukufu wa Mungu, waigawana wingi wao na wenye mahitaji, na kuwasaidia wengine. Ibrahimu alifanya hivyo, akiajiri mamia ya watu na kwa njia hiyo kuwapa mahitaji yao (ona Mwanzo 14:14). Hata Ayubu pia alifanya hivyo, naye alishuhudia kwamba alitumia mali yake kutunza wajane na yatima (Ayubu 29:12, 13; 31:16-22). Wenye vipawa vya kuanzisha biashara wanapaswa kuhakikisha kwamba shughuli kubwa ya biashara yao ni kumtii Mungu na kuwapenda jirani zao kama wanavyojipenda wenyewe.
“Maandiko Yanasema Yesu Alifanyika Maskini Ili Sisi Tuwe Matajiri”
Ni kweli kabisa. Biblia inasema hivi:
Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake (2Wakor. 8:9).
Hoja hutolewa kwamba kwa kuwa andiko hilo linaonyesha kwamba Yesu alikuwa tajiri wa mali huko mbinguni, na akawa maskini wa mali hapa duniani, basi utajiri wa mali ndicho alichomaanisha Paulo wakati alipoandika kwamba wasomaji wake wawe matajiri kwa sababu ya umaskini wa Kristo. Wanasema hivi: Kama kweli Paulo alikuwa anazungumza juu ya utajiri wa mali na umaskini katika sehemu ya kwanza ya mstari, asingeweza kuzungumzia juu ya utajiri wa kiroho katika sehemu ya pili ya andiko.
Kama kweli Paulo alimaanisha kwamba tutakuwa matajiri wa mali kwa sababu ya umaskini wa mali wa Kristo, basi inashangaza kwamba katika sura chache baadaye, kwenye barua hiyo hiyo anaandika hivi:
[Nimekuwa] Katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi (2Wakor. 11:27).
Ikiwa katika 2Wakorintho 8:9 Paulo alimaanisha kwamba Kristo alifanyika maskini wa mali ili sisi tuwe matajiri wa mali, basi kusudi la Kristo halikuwa linatimia maishani mwa Paulo! Basi, Paulo hakumaanisha kwamba Kristo alifanyika maskini wa mali ili sisi tuwe matajiri wa mali hapa duniani. Bila shaka alimaanisha kwamba tungekuwa matajiri kiroho – “matajiri kwa Mungu” – tukitumia maneno ya Yesu (ktk Luka 12:21), na matajiri mbinguni, mahali ambapo hazina zetu na mioyo yetu vipo.
Je, ni halali kusema kwamba kwa kuwa Paulo alizungumza juu ya utajiri wa vitu katika sehemu moja ya andiko, asingeweza kuzungumzia juu ya utajiri wa kiroho katika sehemu ya pili ya andiko hilo, kama inavyodaiwa na wahubiri wa mafanikio? Hebu tufikiri kidogo maneno ya Yesu, anapozungumza na wafuasi Wake katika mji wa Smirna.
Naijua dhiki yako na umaskini wako (ingawa u tajiri) … (Ufunuo 2:9a).
Ni wazi kwamba Yesu alikuwa anazungumzia umaskini wa mali ambao waamini wa Smirna walikabiliana nao. Kisha, baadaye kidogo akasema juu ya utajiri wa kiroho wa waamini hao hao.
“Yesu Aliahidi Kwamba Tukitoa Tutapata Mara Mia”
Ni kweli Yesu alioahidi kurudishiwa mara mia kwa wale watakaojitolea kiasi fulani. Tuangalie maneno Yake hasa.
Amin nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu ake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao, uzima wa milele (Marko 10:29, 30).
Hii si ahadi kwa watu wanaowapa wahubiri fedha, kama inavyodaiwa na wahubiri wa mafanikio mara nyingi. Ni ahadi kwa wale wanaoacha nyumba zao, mashamba yao na ndugu zao ili kwenda kuhubiri Injili mbali. Yesu aliwaahidi watu hao “mara mia sasa wakati huu.”
Lakini je, Yesu alikuwa anawaahidi watu kama hao kwamba watakuwa wamiliki wa nyumba mia moja au mashamba mia moja kama wahubiri wengine wa mafanikio wanavyodai? Hapana. Kwani aliahidi kwamba watu hao watapata mama mia moja na watoto mia moja? Yesu alikuwa anasema kwamba wale wanaoacha nyumba zao na familia zao wangegundua kwamba waamini wenzao wangewakaribisha nyumbani kwao na kuwapokea kama wanafamilia miongoni mwa familia zao.
Ona pia kwamba Yesu aliahidi udhia na uzima wa milele kwa watu hao. Hii inatukumbusha mantiki ya fungu zima, ambalo wanafunzi walitazama kijana tajiri aliyetaka uzima wa milele akiondoka kwa masikitiko sana, huku Yesu akisema, “Ni rahisi zaidi kwa ngamia kupenya kwenye tundu la sindano kuliko kwa tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu” (Marko 10:25).
Wanafunzi wakashangazwa sana na maneno ya Yesu na kujiuliza juu ya uwezekano wao kuingia katika ufalme wa Mungu. Walimkumbusha Yesu kwamba wameacha vitu ili kumfuata Yeye. Ndipo akazungumzia hiyo ahadi Yake ya kupata “mara mia.”
Pamoja na hayo yote, inashangaza kwamba mhubiri wa mafanikio atajaribu kutushawishi kwamba Yesu alikuwa anaahidi kurudishiwa vitu mara mia, ambavyo vingetufanya kuwa matajiri haraka sana, ukizingatia kwamba muda mfupi tu kabla ya hapo alikuwa anamwambia mtu tajiri auze kila kitu na kuwapa maskini mauzo yote, ikiwa alitaka uzima wa milele!
Yapo maandiko mengine mengi sana ambayo wahubiri wa mafanikio huyapindua, licha ya hayo tuliyotazama kidogo, ila hatuna nafasi ya kutosha kuangalia kila kitu hapa. Wewe jihadhari tu!
Cha Kukumbuka
Mwanzilishi wa vuguvugu la Methodisti katika Kanisa Anglikana aitwaye John Wesley, alisema neno linalofaa sana kuhusu mtazamo sahihi wa fedha. Alisema hivi: “Pata kiasi unachoweza. Weka kiasi unachoweza. Toa kiasi unachoweza.”
Yaani – Wakristo wafanye kazi kwa bidii, wakitumia uwezo ambao Mungu amewapa na nafasi za kupata fedha, ila, wahakikishe kwamba wanafanya kwa uhalali pasipo kuvunja amri hata moja ya Kristo.
Pili – Waishi maisha rahisi ya uangalifu, wakitumia kiasi kidogo cha fedha iwezekanavyo kwa ajili yao wenyewe. Hilo litawawezesha “kuweka kiasi wanachoweza.”
Hatimaye – baada ya kufuata zile hatua mbili za kwanza, sasa “watoe kiasi wanachoweza.” Wasijifunge kwenye fungu la kumi tu, bali wajinyime kiasi wanachoweza ili wajane na yatima waweze kulishwa, na Injili itangazwe duniani kote.
Kanisa la mwanzo lilifanya hivyo, na tendo la kuwapa wahitaji lilikuwa la kawaida kabisa katika maisha ya watu wa Agano Jipya. Waamini wa kwanza walishika sana amri ya Yesu kwa wafuasi Wake, kwamba, “Viuzeni vyote mlivyo navyo, mwape maskini. Jifanyeni mikoba isiyochakaa, hazina isiyo na mwisho mbinguni, mahali ambapo mwizi wala nondo haviharibu” (Luka 12:33). Tunasoma maelezo ya Luka kuhusu kanisa la kwanza kama ifuatavyo:
Na wote walioamini walikuwa mahali pamoja, na kuwa na vitu vyote shirika, wakiuza mali zao, na vitu vyao walivyokuwa navyo, na kuwagawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja. … Na jamii ya watu walioamini walikuwa na moyo mmoja na roho moja; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu chochote alicho nacho ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote shirika. … Na neema nyingi ikawa juu yao wote. Wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa, wakaiweka miguuni pa mitume; kila mtu akagawiwa kwa kadiri ya alivyohitaji (Matendo 2:44-45; 4:32-35).
Maandiko pia yako wazi kwamba, kanisa la kwanza liliwalisha wajane maskini sana, na kuhudumia mahitaji yao makubwa (ona Matendo 6:1; 1Timo. 5:3-10).
Paulo, mtume mkuu kuliko wote waliopata kuishi, aliyekabidhiwa na Mungu kazi ya kuipeleka Injili kwa watu wa Mataifa, mwandishi wa nyaraka nyingi katika Agano Jipya, alihesabu kuhudumia mahitaji ya kawaida ya maskini kuwa sehemu muhimu sana ya huduma yake. Miongoni mwa makanisa aliyoanzisha, Paulo alikusanya fedha nyingi sana kwa ajili ya Wakristo maskini (ona Matendo 11:27-30; 24:17; Warumi 15:25-28; 1Wakor. 16:1-4; 2Wakor. Sura ya 8 na 9; Wagalatia 2:10). Miaka kama kumi na saba hivi baada ya kuokoka kwake, Paulo alisafiri kwenda Yerusalemu ili kueleza Injili aliyopokea, ikakaguliwe na Petro, Yakobo na Yohana. Hakuna yeyote kati yao aliyepata kasoro katika ujumbe aliokuwa anahubiri mpaka hapo, na anapoeleza tukio hilo katika barua yake kwa Wagalatia, anakumbuka hivi: “Ila neno moja tu walitutakia, tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii kulifanya” (Wagalatia 2:10). Katika akili za Petro, Yakobo, Yohana na Paulo, kuwaonyesha maskini fadhili kilikuwa kitu cha pili – cha kwanza ni kuitangaza Injili.
Hitimisho
Kwa mada hii, ushauri bora kwa watumishi wanaofanya wengine kuwa wanafunzi unatoka kwa mtume Paulo, ambaye, baada ya kumwonya Timotheo kwamba “shina moja la maovu yote ni kupenda fedha,” na kumwambia kwamba “wengine kwa kuitamani hiyo wamepotoka na kuiacha imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” anampa ushauri huu unaofuata.
Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi na upole (1Timo. 6:11. Maneno mepesi kukazia hoja!).
[1] Wahubiri wa mafanikio hutumia kweli hii kuthibitisha kwamba huduma ya Yesu ilikuwa ya mafanikio. Hakuna shaka kwamba Mungu alimpa Yesu mahitaji Yake yote ili aweze kufanikisha huduma Yake. Tofauti kati ya Yesu na hao wahubiri ni kwamba Yesu hakuwa mbinafsi, wala hakutumia fedha za huduma yake kujitajirisha Mwenyewe.